Hamia kwenye habari

Mashahidi wa Yehova Hutumiaje Michango?

Mashahidi wa Yehova Hutumiaje Michango?

 Tunatumia michango kutegemeza utendaji wa kidini na wa kutoa msaada unaosimamiwa na tengenezo letu. Utendaji huo unatusaidia kutimiza kazi yetu kuu, yaani, kuwasaidia watu kuwa wanafunzi wa Kristo Yesu.—Mathayo 28:19, 20.

 Hatutumii michango kuwatajirisha watu wowote. Hatuwalipi mshahara wazee au watumishi wowote, na Mashahidi wa Yehova hawalipwi ili kwenda nyumba kwa nyumba. Wale wanaotumikia katika ofisi zetu za tawi na kwenye makao makuu ya ulimwenguni pote, kutia ndani wale wanaofanyiza Baraza Linaloongoza, hawalipwi mshahara wowote.

Mifano Kadhaa ya Utendaji Wetu

  •   Utangazaji: Tunatafsiri, kuchapisha, kusafirisha, na kusambaza mamilioni ya Biblia na machapisho mengine ya Kikristo kila mwaka, bila malipo. Vivyo hivyo, tovuti ya jw.org na programu ya JW Library huwawezesha watu kupata machapisho yetu kielektroni, bila malipo au matangazo ya kibiashara.

  •   Ujenzi na Udumishaji: Tunajenga na kudumisha sehemu za ibada zenye kiasi ulimwenguni pote ili kuwezesha makutaniko kuwa na maeneo yanayofaa ya kukutana na kumsifu Mungu pamoja. Tunafanya vivyo hivyo na ofisi za tawi na ofisi za utafsiri. Sehemu kubwa ya kazi hiyo hufanywa na wajitoleaji, na hilo husaidia kupunguza gharama.

  •   Usimamizi: Utendaji katika makao yetu makuu ya ulimwenguni pote, ofisi za tawi, na ofisi za utafsiri, kutia ndani utendaji wa wale wanaotumikia wakiwa waangalizi wanaosafiri, hutegemezwa na michango inayotolewa kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote.

  •   Kuhubiri: Mashahidi hawalipwi ili kuhubiri habari njema au kuwafundisha wengine “neno la Mungu.” (2 Wakorintho 2:17) Hata hivyo, kama ilivyokuwa kwa utendaji wa Wakristo wa karne ya kwanza, wahudumu walioteuliwa na kuzoezwa wanatumia muda wao mwingi katika kazi ya kuhubiri huandaliwa makao yenye kiasi na mahitaji ya msingi ya maisha.—Wafilipi 4:16, 17; 1 Timotheo 5:17, 18.

  •   Kufundisha: Makusanyiko yetu ya mzunguko na ya eneo hutegemezwa kwa michango. Mbali na hilo sisi hutayarisha programu za sauti na video zinazotegemea Biblia. Pia, tunaendesha shule ambazo huwazoeza wazee na wahudumu wa wakati wote kuwa wenye matokeo zaidi katika migawo yao.

  •   Msaada Wakati wa Misiba: Tunaandaa chakula, maji, na makao kwa wale ambao wameathiriwa na misiba ya asili au iliyosababishwa na wanadamu. Kazi hiyo ya kutoa msaada inawanufaisha “wale ambao ni ndugu zetu katika imani” na pia wale ambao si Mashahidi.—Wagalatia 6:10.