Hamia kwenye habari

Ni Nini Hutendeka Katika Harusi za Mashahidi wa Yehova?

Ni Nini Hutendeka Katika Harusi za Mashahidi wa Yehova?

 Kwa kawaida, harusi za Mashahidi wa Yehova huwa programu fupi yenye staha ambapo hotuba fupi inayotegemea Biblia hutolewa. Baada ya programu hiyo kunaweza kuwa na kikusanyiko cha kirafiki, au karamu, ambayo inaweza kutia ndani mlo. * Yesu alihudhuria karamu kama hiyo mwanzoni mwa huduma yake katika mji wa Kana.—Yohana 2:1-11.

 Nini nini hutendeka katika programu ya harusi?

 Jambo kuu katika programu hiyo ni hotuba ya harusi, iliyo na urefu wa dakika 30 hivi ambayo hutolewa na mhudumu wa Mashahidi wa Yehova. Hotuba hiyo yenye kujenga inakazia jinsi Biblia inavyoweza kuwasaidia wenzi hao kuwa na ndoa inayodumu, yenye upendo, na furaha.—Waefeso 5:33.

 Katika nchi nyingi, serikali huwaruhusu wahudumu wa Mashahidi wa Yehova kusajili ndoa. Ikiwa inaruhusiwa, wenzi hao hutoa viapo hivyo baada ya hotuba. Wakipenda wanaweza kuvishana pete. Baada ya hapo, mhudumu huyo hutangaza kwamba wamekuwa mume na mke.

 Katika nchi nyingine, sheria inasema kwamba ndoa inapaswa kusajiliwa katika ofisi ya serikali. Wenzi hao hufanya hivyo muda mfupi kabla ya hotuba ya harusi. Ikiwa bwana na bibi harusi hawatoi kiapo kwenye ofisi ya serikali, wanaweza kufanya hivyo kuelekea mwishoni mwa hotuba. Ikiwa tayari wametoa viapo vyao, wanaweza kuamua kuvirudia, lakini kwa kutumia njeo ya wakati uliopita. Hotuba itamalizika kwa sala ya kumwomba Mungu abariki wenzi hao wapya wa ndoa.

 Harusi za Mashahidi wa Yehova hufanyiwa wapi?

 Mashahidi wengi huchagua kufanyia programu hiyo katika Jumba la Ufalme ikiwa lipo. * Ikiwa wenzi hao wanapenda kuwa na karamu baada ya programu hiyo, wataifanyia mahali pengine.

 Ni nani wanaoweza kuhudhuria?

 Kwa kawaida, ikiwa harusi inafanywa katika Jumba la Ufalme, mtu yeyote anaweza kuhudhuria—wale ambao ni Mashahidi na wale ambao si Mashahidi. Ikiwa wenzi hao watakuwa na karamu, wanaamua ni nani watakaokaribishwa.

 Watu walioalikwa wanapaswa kuvalia kwa njia gani?

 Ingawa hakuna mavazi hususa yanayopaswa kuvaliwa katika Jumba la Ufalme, Mashahidi wa Yehova wanajitahidi kufuata viwango vya Biblia kuhusu kuvalia kwa kiasi na kwa heshima. Wanathamini sana wengine wanapozingatia kanuni hizo. (1 Timotheo 2:9) Bila shaka, ikiwa wenzi hao wanachagua kuwa na karamu, kanuni hizo pia zinahusika.

 Je, zawadi zitatolewa?

 Biblia inatia moyo watu waonyeshe ukarimu. (Zaburi 37:21) Mashahidi wa Yehova wanafurahi kutoa na kupokea zawadi za harusi. (Luka 6:38) Hata hivyo, Mashahidi huepuka kuomba zawadi na kutangaza majina ya watu walioleta zawadi. (Mathayo 6:3, 4; 2 Wakorintho 9:7; 1 Petro 3:8) Licha ya kwamba mambo hayo hayaungwi mkono na Maandiko, mazoea hayo yanaweza kufanya wengine walioalikwa wajihisi vibaya.

 Je, glasi za vinywaji zitainuliwa ili kuwatakia heri?

 Hapana. Mashahidi wa Yehova hawafanyi hivyo kwa kuwa zoea hilo lina chimbuko katika desturi za dini za uwongo. * Mashahidi wa Yehova huwatakia heri wenzi hao kwa njia nyingine.

 Je, watu watawatupia mchele?

 La. Katika maeneo fulani, watu huwatupia maharusi mchele, chengachenga fulani za rangirangi, au vitu vingine kama hivyo. Wanaamini kufanya hivyo kutawaletea wenzi hao bahati nzuri, furaha, na maisha marefu. Lakini Mashahidi wa Yehova huepuka mazoea yoyote yanayohusiana na ushirikina. Hilo linatia ndani mazoea ya kuomba bahati nzuri, jambo linalopingana na kanuni za Biblia.—Isaya 65:11.

 Je, kutakuwa na chakula na vinywaji?

 Programu ya harusi inayofanywa katika Jumba la Ufalme haitii ndani chakula na vinywaji. Wenzi fulani huamua kufanya karamu baada ya programu hiyo, ambako kunakuwa na mlo au viburudisho. (Mhubiri 9:7) Ikiwa wataamua kuwe na kileo, wanahakikisha kinatolewa kwa kiwango chenye kiasi na kinapewa tu wale walio na umri unaoruhusiwa kisheria.—Luka 21:34; Waroma 13:1, 13.

 Je, kutakuwa na muziki au kucheza dansi?

 Ikiwa wenzi hao watakuwa na karamu, watachagua ikiwa kunaweza kuwa na muziki na dansi. (Mhubiri 3:4) Muziki watakaochagua unapaswa kuwa wenye kufaa, kupatana na mapendezi yao na utamaduni. Programu ya harusi inayofanywa katika Jumba la Ufalme huambatana na muziki ambao una msingi wa Kimaandiko.

 Je, Mashahidi wa Yehova huadhimisha ukumbusho wa kila mwaka wa harusi?

 Kwa kuwa kanuni za Biblia hazikatazi au kuunga mkono miadhimisho hiyo, Mashahidi wa Yehova hujiamulia wenyewe ikiwa wataisherehekea au la. Wakiamua kuisherehekea, wanafanya hivyo wakiwa peke yao au pamoja na familia na marafiki.

^ Desturi, mazoea fulani na taratibu za kisheria zinaweza kutofautiana katika eneo moja na lingine.

^ Mhudumu anayetoa hotuba hiyo hadai malipo kwa kufanya hivyo, na hakuna malipo yoyote ya kutumia Jumba la Ufalme.

^ Ili kujua mengi zaidi kuhusu chanzo cha kipagani cha kuinua glasi ya kinywaji, ona “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika toleo la Februari 15, 2007 la Mnara wa Mlinzi.