Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuharibiwa kwa mali zao hakukuwafanya ndugu na dada waache kumtumikia Yehova

GEORGIA | 1998-2006

Vitisho Havikuwazuia Kumtumikia Yehova

Vitisho Havikuwazuia Kumtumikia Yehova

Akina ndugu na dada hawakuogopa, waliendelea kukutana pamoja. Kwa hekima, wazee walichukua hatua za kuwalinda wahubiri. Ndugu André Carbonneau, wakili kutoka Kanada ambaye aliwatetea ndugu zetu katika miaka hiyo anakumbuka hivi: “Kwa kawaida kungekuwa na ndugu aliyesimama karibu na eneo la mkutano akiwa na simu ya mkononi. Ikiwa angeona umati wa watu ukija, angewaonya wazee mara moja kuhusu uwezekano wa kushambuliwa.”

Wapinzani waliteketeza nyumba ya familia ya Shamoyan (kushoto) na depo ya machapisho (kulia)

Baada ya kila shambulizi, wawakilishi wawili wa ofisi ya tawi waliwatembelea akina ndugu ili kuwaimarisha. André anasema, “Jambo la kustaajabisha ni kwamba kwa kawaida wawakilishi wa ofisi ya tawi wangekuta jumba limejaa ndugu na dada wenye furaha na wanaotabasamu.”

Akina ndugu walikabiliana na watu waliowatesa ndani na nje ya mahakama

Hata wale ambao hawakushambuliwa, kutia ndani wanafunzi wa Biblia, waliazimia kumtumikia Yehova. André anakumbuka akizungumza na mwanamke mmoja ambaye alikuwa karibu kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa. Mwanamke huyo alimwambia hivi, “Nilipoona mashambulizi hayo kwenye televisheni, nilitambua tofauti kati ya Wakristo wa kweli na wa uwongo, nami ninataka kuwa Mkristo wa kweli.”

Kuwatetea Waabudu Wenzetu kwa Ujasiri

Katika miaka hiyo migumu, wahubiri walionyesha imani na ujasiri mwingi kwa kuendelea kuhubiri kwa bidii. Wale waliohusika katika kuwatetea waabudu wenzao mahakamani walionyesha imani kama hiyo.

Mara nyingi, habari za uwongo kuwahusu Mashahidi zilirushwa katika vyombo vya habari. Mashahidi walisemwa kuwa ni watu wanaovunja familia, wanaokataa matibabu, na wanaoipinga serikali. Mawakili waliowatetea walihatarisha sifa na kazi yao.

Ndugu wenye ujasiri wa Idara ya Sheria nchini Marekani waliwatetea waamini wenzao mahakamani

John Burns, wakili kutoka katika ofisi ya tawi ya Kanada aliyewasaidia akina ndugu wa Georgia katika miaka hiyo, anakumbuka hivi: “Ndugu na dada wenyeji waliokuwa mawakili walijitolea kufanya kazi hiyo. Licha ya matatizo ambayo wangepata, hawakuogopa kwenda mahakamani na kujitambulisha kuwa Mashahidi wa Yehova.” Mashahidi hao wenye ujasiri walichangia sana katika “kutetea na kuithibitisha kisheria habari njema.”—Flp. 1:7.

Watu wa Georgia Washutumu Jeuri

Hata hivyo, Mashahidi waliendelea kushambuliwa. Hivyo, kuanzia Januari 8, 2001, Mashahidi walisambaza ombi la kutaka walindwe dhidi ya mashambulizi na wale waliowashambulia wafikishwe mahakamani.

Ndugu Burns anaeleza kusudi la ombi hilo: “Lengo letu lilikuwa kuonyesha kwamba watu wengi wa Georgia hawaungi mkono jeuri dhidi ya Mashahidi wa Yehova na kwamba jeuri hiyo inaendelezwa na kikundi kidogo tu cha watu wenye msimamo mkali wa kidini.”

Baada ya majuma mawili tu, watu 133,375 kutoka maeneo yote ya Georgia walitia sahihi zao kwenye ombi hilo. Wengi kati ya wale waliotia sahihi walikuwa waumini wa Kanisa Othodoksi. Ingawa ombi hilo lilifikishwa kwa Rais Shevardnadze, jeuri haikuisha. Watu hao wenye msimamo mkali wa kidini waliendelea kuwashambulia Mashahidi.

Maelfu ya watu wa Georgia walitia sahihi ombi lililopinga jeuri dhidi ya Mashahidi wa Yehova

Wakati huohuo, Yehova aliendelea kuwabariki watu wake. Huku watu hao wenye msimamo mkali wa kidini wakiendelea kuwasumbua watu wa Mungu, Yehova Mungu alikuwa akiwavuta watu wengi wanyoofu watoke katika dini ya uwongo.

Kutoka Katika Dini ya Uwongo

Kwa muda mrefu, Babilina Kharatishvili alikuwa mshiriki wa dhati wa Kanisa Othodoksi la Georgia. Alipokuwa na umri wa miaka 30 na kitu, alisafiri kutoka mji hadi mji na kijiji hadi kijiji, akiwafundisha watu kuhusu maisha ya watakatifu.

Lakini Babilina alitaka kujua mengi zaidi kumhusu Mungu. Kwa hiyo, aliamua kuhudhuria hotuba zilizotolewa katika seminari ya Kanisa Othodoksi la Georgia. Pindi moja, kasisi aliwaonyesha wasikilizaji wake kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uzima wa Milele na akawatia moyo wajipatie nakala kutoka kwa Mashahidi wa Yehova. Aliwaambia hivi, “Kitabu hiki kinaweza kuwafundisha mambo mengi kuhusu Biblia.”

Babilina alishangaa. Sikuzote aliwaepuka Mashahidi, lakini sasa kasisi alikuwa akipendekeza wasome vitabu vyao! Akajiambia hivi, ‘Ikiwa Mashahidi wa Yehova ndio wanaopaswa kunifundisha kumhusu Mungu, ninafanya nini hapa?’ Mara moja aliwasiliana na Mashahidi katika jiji la Poti na akaanza kujifunza Biblia.

Kadiri Babilina alivyoendelea kujifunza mengi kutoka katika Biblia, ndivyo alivyofanya mabadiliko maishani mwake. Alisema hivi: “Nilipojionea kwamba Biblia inasema ni kosa kuabudu sanamu, niliepuka aina zote za ibada ya sanamu. Nilisadiki kwamba hilo ndilo jambo linalofaa zaidi.” Aliamua kuwa Shahidi wa Yehova, wakati huo akiwa na umri wa karibu miaka 80.

Babilina alimweleza mjukuu wake, Izabela, kuhusu kweli ya Biblia

Kwa kusikitisha, mnamo 2001, Babilina akawa mgonjwa na kufa kabla ya kubatizwa. Lakini baadaye mjukuu wake, Izabela, alibatizwa na sasa anamtumikia Yehova kwa uaminifu.

Alitaka Kuwa Mtawa wa Kike

Eliso Dzidzishvili alikuwa na umri wa miaka 28 alipoamua kuwa mtawa wa kike. Katika mwaka wa 2001 alihamia Tbilisi, kwa kuwa hakukuwa na makao ya watawa karibu na nyumbani kwao, Tkibuli. Alipokuwa akitafuta nafasi ya kuandikishwa katika makao ya watawa, alifanya kazi ya muda akiwa mwalimu aliyejiajiri. Mmoja wa wanafunzi wake alikuwa binti ya dada anayeitwa Nunu.

Eliso anasema hivi: “Mara nyingi tulizungumza kuhusu Biblia. Niliitetea dini ya Othodoksi kwa bidii, lakini Nunu alinionyesha kwa subira mstari mmoja baada ya mwingine. Siku moja, alipendekeza anisomee broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? Tulipokuwa tukisoma mafungu na mistari ya Biblia, nilitambua kwamba kuabudu sanamu kunapingana moja kwa moja na amri ya Mungu.”

Baadaye, Eliso alienda kanisani na kumuuliza kasisi maswali kadhaa. Kutokana na majibu yake, ilikuwa wazi kwamba mafundisho ya kanisa hayakutegemea Biblia. (Marko 7:7, 8) Akisadiki kwamba alikuwa amepata kweli, mara moja alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova na upesi akabatizwa.

Eliso Dzidzishvili (kushoto), aliyetaka kuwa mtawa wa kike, na Nunu Kopaliani (kulia)

Kujenga Majumba ya Ufalme Licha ya Upinzani

Kufikia mwaka wa 2001, makutaniko mengi sana yalihitaji mahali panapofaa pa ibada. Kulingana na makadirio fulani, ilionekana kwamba Majumba 70 hivi ya Ufalme yalihitajika. Kwa hiyo, licha ya upinzani uliokuwepo nchini, mpango wa ujenzi wa Majumba ya Ufalme ulianzishwa.—Ezra 3:3.

Upesi kikosi cha ujenzi kikaanza kurekebisha jengo ambalo lilikuwa limetumiwa na makutaniko kadhaa ya Tbilisi. Baada ya hapo, miradi mingine miwili ya ujenzi ikaanza—mmoja jijini Tbilisi na mwingine katika eneo la Chiatura, magharibi mwa Georgia.

Jumba la Ufalme lililotumiwa awali jijini Tbilisi (kushoto) na jumba jipya lililojengwa badala yake (kulia)

Ndugu Tamazi Khutsishvili, aliyefanya kazi katika mradi wa ujenzi kule Chiatura, anakumbuka hivi: “Kila siku akina ndugu na dada kumi na watano walijitolea kufanya kazi kwenye mradi huo. Baada ya muda mfupi, kila mtu katika eneo hilo alijua tulikuwa tukijenga jumba jipya. Nyakati fulani tulisikia fununu kwamba wapinzani wetu walitaka kuja kubomoa Jumba hilo la Ufalme.”

Kukiwa na upinzani wa aina hiyo, je, kazi ya ujenzi ingefanikiwa? Tamazi anasema hivi: “Tuliendelea na kazi yetu hadi Jumba hilo la Ufalme lilipokamilika baada ya miezi mitatu. Licha ya vitisho, hakuna hata mpinzani mmoja aliyekuja.” *

Utulivu Baada ya Muda Mrefu

Washiriki wa kikundi chenye msimamo mkali cha Kanisa Othodoksi na kiongozi wao, Vasili Mkalavishvili, wakiwa wamekamatwa

Mnamo Oktoba 2003, mradi wa ujenzi ulianza katika jiji la Samtredia. Kwa mara nyingine, watu wenye msimamo mkali wa kidini waliwatisha akina ndugu. Baada tu ya kuta kusimamishwa na hata kabla ya saruji kukauka wapinzani walifika na kubomoa kuta hizo.

Hata hivyo, mnamo Novemba 2003, jambo jipya liliwaletea ndugu na dada zetu nchini Georgia kitulizo. Serikali mpya ilipochukua mamlaka ilifanya kuwe na uhuru wa ibada. Kwa sababu ya badiliko hilo, washiriki kadhaa wa kikundi chenye msimamo mkali wa Kanisa Othodoksi waliokuwa wamewashambulia Mashahidi wa Yehova walikamatwa.

Watu wa Mungu Wapata Baraka Nyingi

Muda fulani baada ya mateso kuisha, watu wa Yehova nchini Georgia walipata baraka nyingi za kiroho. Kwenye kusanyiko la wilaya la 2004, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ilitolewa katika Kigeorgia.

Kisha katika Kusanyiko la Wilaya la “Ukombozi Unakaribia!” la mwaka wa 2006, tukio lingine lisilosahaulika lilitokea. Wote waliohudhuria walisisimuka sana kusikia kwamba Geoffrey Jackson, mshiriki wa Baraza Linaloongoza angetoa hotuba. Walishangilia kumsikia Ndugu Jackson akitangaza kutolewa kwa Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kigeorgia!

Kutolewa kwa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kigeorgia mnamo 2006

Wajumbe wengi walijawa na machozi ya shangwe wakiwa na shukrani. Dada mmoja alisema hivi: “Siwezi kueleza shangwe niliyohisi tulipopokea Biblia nzima. . . . Lilikuwa tukio la kihistoria.” Zaidi ya watu 17,000 walifurahia karamu hiyo ya kiroho. Hilo lilikuwa tukio la pekee katika historia ya watu wa Yehova nchini Georgia.

^ fu. 29 Kuanzia mwaka wa 2001 hadi 2003, Majumba saba ya Ufalme yalijengwa kotekote nchini.