Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

JINSI MICHANGO YAKO INAVYOTUMIWA

Kutoa Msaada Katika 2022—Upendo wa Kindugu Unaonyeshwa kwa Matendo

Kutoa Msaada Katika 2022—Upendo wa Kindugu Unaonyeshwa kwa Matendo

JANUARI 1, 2023

 Biblia ilitabiri kwamba katika siku zetu kungekuwa na mambo kama vile vita, matetemeko ya ardhi, magonjwa na mambo mengine “yenye kuogopesha.” (Luka 21:10, 11) Maneno hayo ya kinabii yameendelea kutimia katika mwaka wa utumishi wa 2022. a Kwa mfano, vita nchini Ukrainia vimeendelea na hilo limeathiri maisha ya mamilioni ya watu. Sehemu kubwa ya ulimwengu bado ilikuwa ikijaribu kupambana na madhara ya janga la COVID-19. Kwa kuongezea, watu wengi sana waliathiriwa na majanga ya asili, kama vile matetemeko ya ardhi nchini Haiti na vimbunga vilivyosababisha madhara katika Amerika ya Kati, Filipino, na kusini mashariki mwa Afrika. Mashahidi wa Yehova wamewasaidiaje walioathiriwa?

 Katika mwaka wa utumishi wa 2022, tengenezo letu lilitoa msaada kwa watu walioathiriwa na misiba 200 hivi! Kwa ujumla, tulitumia dola milioni 12 hivi kutoa msaada. b Ona jinsi michango ilivyotumiwa kuwasaidia waathiriwa wa misiba miwili.

Matetemeko ya Ardhi Nchini Haiti

 Agosti 14, 2021, tetemeko la ardhi lenye ukubwa wa 7.2 lilipiga eneo la kusini la Haiti. Kwa kusikitisha, Mashahidi watatu walikufa—dada wawili na ndugu mmoja. Waliookoka wamelazimika kukabiliana na maumivu ya kimwili na kihisia yaliyosababishwa na tetemeko hilo. Ndugu anayeitwa Stephane alisema: “Katika jiji lote watu wengi sana walikufa hivyo kulikuwa na mazishi kadhaa kila juma kwa zaidi ya miezi miwili.” Ndugu mwingine anayeitwa Éliézer alisema hivi: “Mashahidi wengi hawakuwa na makao, nguo, viatu, na mahitaji mengine muhimu. Kwa miezi kadhaa, wengi waliishi kwa hofu kwa sababu ya matetemeko madogo yaliyoendelea kutokea tena na tena.”

 Tengenezo letu lilichukua hatua haraka. Ofisi ya tawi ya Haiti iligawa zaidi ya tani 53 za chakula, na pia mahema, maturubai, magodoro, na chaja za simu zitumiazo nguvu ya jua. Kwa kuongezea, katika mwaka wa utumishi wa 2022, zaidi ya nyumba 100 zilijengwa upya au kukarabatiwa. Zaidi ya dola milioni moja zilitumika katika kazi ya kutoa msaada.

Msaada wa chakula ukifika nchini Haiti

 Ndugu na dada zetu wanashukuru sana. Lorette anasema: “Tetemeko la ardhi liliharibu kabisa nyumba yetu na biashara yetu. Hatukuwa na chakula. Lakini tengenezo la Yehova lilitusaidia, lilitupatia kila kitu tulichohitaji.” Micheline anasema: “Tetemeko hilo la ardhi liliharibu nyumba ambayo mimi na wana wangu wawili tuliishi. Sikujua jambo la kufanya isipokuwa tu kuomba msaada kupitia sala, kisha Yehova alinijibu kupitia tengenezo lake. Sasa tuna nyumba imara. Nimeazimia kufanya yote niwezayo ili kuonyesha shukrani zangu kwa Yehova.”

 Wenye mamlaka walitambua jitihada zetu za kutoa msaada. Mkuu wa manispaa ya jiji la L’Asile alisema hivi: “Ninawapongeza kwa jinsi mlivyotenda haraka ili kusaidia. Ninawasifu kwa kuwaonyesha wenye mamlaka heshima kubwa. Ninafurahi kuona kwamba kusudi lenu si kujitafutia pesa. Badala yake, mnataka kuwasaidia watu. Mnachochewa na upendo.”

Malawi na Msumbiji Zakumbwa na Dhoruba ya Kitropiki Ana

 Januari 24, 2022, Dhoruba ya Kitropiki Ana iliipiga Msumbiji kisha ikaelekea upande wa magharibi na kuipiga Malawi. Dhoruba hiyo ilitokeza mvua kubwa na upepo mkali, ambao ulivuma kwa kasi ya kilomita 100 kwa saa. Dhoruba hiyo iliangusha nguzo za umeme, ikavunja madaraja, na kusababisha mafuriko makubwa.

 Dhoruba hiyo iliathiri zaidi ya Mashahidi 30,000 nchini Malawi na Msumbiji. Charles, ndugu aliyesaidia katika kazi ya kutoa msaada, alisema hivi: “Nilipoona jinsi akina ndugu walivyokuwa wakiteseka na vitu walivyopoteza, nilihuzunika sana na nikahisi sikuwa na uwezo wa kuwasaidia.” Hali ilikuwa mbaya sana kwa sababu walikuwa na akiba ndogo sana ya chakula na mazao yao yalifagiliwa mbali na mafuriko. Wengi walipoteza nyumba zao. Kwa kusikitisha, ndugu mmoja alimpoteza mke wake na binti zake wawili waliozama wakati ambapo mashua iliyokuwa ikiwaokoa ilipinduka.

Nyumba ya wenzi wa ndoa Mashahidi iliyoharibiwa nchini Msumbiji

Nyumba yao iliyojengwa upya

 Dhoruba hiyo ilikuwa yenye kuogopesha. Saa 7:00 usiku huko Nchalo, Malawi, familia ya Sengeredo ilisikia sauti yenye kutisha ya maji mengi yakisonga kwa kasi. Mito miwili ilikuwa imefurika! Ndugu Sengeredo aliamua kwamba walihitaji kuondoka katika nyumba yao. Ulikuwa uamuzi wa hekima kwa sababu baada ya muda mfupi mafuriko yaliangusha nyumba hiyo. Mali zao ziliharibiwa au zikafagiliwa. Familia hiyo iliamua kwenda kwenye Jumba la Ufalme, ambalo kwa kawaida ni mwendo wa dakika 30 kutoka nyumbani kwao. Hata hivyo, wakati huu iliwachukua saa mbili. Walifika wakiwa wamelowa maji na wamechoka, lakini wakiwa salama.

 Ofisi za tawi nchini Malawi na Msumbiji zilianza mara moja kutoa msaada. Waliwaomba waangalizi wa mzunguko na wazee wachanganue mahitaji ya akina ndugu walioathiriwa na kuandaa msaada wa kiroho na wa kihisia. Halmashauri kadhaa za Kutoa Msaada (DRC) zilipewa mgawo wa kusimamia kazi ya kutoa msaada, na halmashauri hizo zilianza mara moja kuwasaidia ndugu zetu kupata chakula na mahitaji mengine. Zaidi ya dola 33,000 zilitumika kuandaa msaada wa kibinadamu na zaidi ya dola 300,000 zilitumiwa katika kukarabati na kujenga upya nyumba zilizoharibiwa.

 Halmashauri hizo zilitumia pesa hizo kwa hekima, jambo muhimu sana wakati wa mfumuko wa bei. Kwa mfano, katika miezi saba ya kwanza ya kutoa msaada, bei ya unga wa mahindi, ambacho ndicho chakula kikuu nchini Malawi, iliongezeka kwa asilimia 70. Pia, bei ya petroli iliongezeka. Ili kuokoa pesa, akina ndugu walinunua chakula na vifaa vya ujenzi katika eneo na kwa bei ya jumla. Hivyo, walipata punguzo la bei na kuepuka gharama kubwa ya usafirishaji.

 Kazi hiyo ya kutoa msaada imegusa mioyo ya watu wa Yehova. Felisberto, ndugu nchini Msumbiji anasema: “Sijawahi kuona tengenezo kama hili, lilitoa vitu vingi sana: vifaa vya ujenzi, usafiri, wajenzi, chakula, na mwongozo wenye upendo. Msaada huo ni uthibitisho ulio wazi wa upendo wa kindugu ambao Yesu alifafanua katika Yohana 13:34, 35.” Ester, mjane nchini Malawi ambaye nyumba yake iliharibiwa, anasema: “Nilikuwa nimekata tamaa kwa sababu sikuwa na pesa za kujenga nyumba nyingine. Hata hivyo, ndugu walipokuja na kunijengea, nilihisi kana kwamba tayari niko katika paradiso.”

 Kadiri tunavyokaribia kuingia katika ulimwengu mpya, ndivyo tunavyotarajia kuona majanga mengi zaidi. (Mathayo 24:7, 8) Hata hivyo, kwa sababu ya michango yenu ya ukarimu, tuna uhakika kwamba watu wa Yehova wataendelea kupata msaada wanaohitaji. Njia za kutoa michango zimefafanuliwa kwenye donate.isa4310.com. Asante sana kwa ukarimu wako.

a Mwaka wa utumishi wa 2022 ulianza Septemba 1, 2021, na kuisha Agosti 31, 2022.

b Makala hii inapotaja dola inarejelea dola za Marekani.