Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

JINSI MICHANGO YAKO INAVYOTUMIWA

Kutetea Uhuru wa Ibada wa Jamii za Wenyeji wa Asili

Kutetea Uhuru wa Ibada wa Jamii za Wenyeji wa Asili

MEI 1, 2021

 Miongoni mwa mamia ya mamilioni ya watu wanaoishi katika nchi za Amerika ya Latini, kuna mamilioni ambao wana lugha na desturi za kienyeji. Wenyeji hao wa asili ni ndugu na dada zetu wa kiroho ambao wanathamini utamaduni wao. Ili kuwasaidia watu kiroho, wanatafsiri na kusambaza machapisho ya Mashahidi wa Yehova katika lugha 130 za kienyeji huko Amerika ya Latini. a Hata hivyo, baadhi yao wamekabili upinzani kwa sababu ya kuchagua kumtumikia Yehova na kwa kukataa kushiriki desturi zisizo za kimaandiko ambazo ni za kawaida katika jamii hizo. Michango yako imetumiwaje kuwasaidia?

Wamesaidiwa Kurudi Nyumbani

 Nchini Mexico, ndugu na dada zetu wa jamii ya Huichol katika milima ya Jimbo la Jalisco walikataa kwa heshima kushiriki katika mazoea ya kidini yaliyokiuka dhamiri zao. b Kufanya hivyo kuliwakasirisha watu fulani katika jamii. Desemba 4, 2017, umati wenye ghasia ulishambulia kikundi fulani cha Mashahidi na watu fulani waliokuwa pamoja nao. Umati huo uliwafukuza kutoka kwenye jamii hiyo, ukaharibu mali zao, na wakatisha kuwaua wowote ambao wangejaribu kurudi.

 Mashahidi katika miji ya karibu walishughulikia mahitaji ya ndugu na dada zetu. Lakini, ni nini ambacho kingeweza kufanywa ili warudi nyumbani? Ndugu mmoja anayeitwa Agustín anaeleza hivi: “Hatukuwa na pesa za kutosha kumlipa wakili, na hatukujua twende wapi ili kupata ushauri wa kisheria.”

 Kwa kuwa uhuru wa ibada wa ndugu zetu ulikuwa umeshambuliwa, ofisi ya tawi ya Amerika ya Kati ilichukua hatua upesi. Kwanza waliwasiliana na maofisa wa eneo hilo ili wafanye uchunguzi kuhusu uhalifu huo. Kisha, wakapata idhini kutoka kwa Halmashauri ya Waratibu ya Baraza Linaloongoza ya Mashahidi wa Yehova ili kushirikiana na Idara ya Kisheria ya makao makuu ya ulimwenguni pote na kuwasilisha mashtaka kwa niaba ya ndugu na dada zetu katika eneo la Huichol. Hatimaye, kesi hiyo ilifika kwenye Mahakama Kuu ya Haki ya Taifa, yaani, mahakama kuu ya Mexico.

 Kikundi cha mawakili kutoka nchi mbalimbali kilitayarisha hoja za wazi na wakaeleza kwamba kama wengine wanavyopaswa kuheshimu tamaduni za jamii za wenyeji, jamii hizo pia zinapaswa kuheshimu na kulinda uhuru wa washiriki wao wote. Haki za kibinadamu hazina mipaka.

 Julai 8, 2020, mahakimu wote wa mahakama kuu ya Mexico walitoa uamuzi ambao haukupingwa wa kuwaunga mkono Mashahidi wa Yehova. Waliagiza kwamba wale ambao walikuwa wamefukuzwa waruhusiwe kurudi katika jamii yao. Agustín aliyenukuliwa awali anaeleza jinsi yeye na wengine wanavyohisi: “Tunashukuru sana na kufurahi kwa yote ambayo akina ndugu wametufanyia. Ikiwa hawangetusaidia, hakuna kitu ambacho tungeweza kufanya.”

“Kufanya Mengi kwa Ajili ya Watu Wachache”

 Wakati huohuo ndugu zetu katika kijiji cha San Juan de Ilumán, Ekuado ambacho ni makao ya wenyeji wa Bonde la Otavalo, walikabili upinzani kama huo. Mnamo 2014, baada ya kupata vibali vilivyohitajika, walianza kujenga Jumba la Ufalme. Hata hivyo, kasisi fulani aliongoza umati wa zaidi ya watu 100 na kukomesha ujenzi huo kwa nguvu. Jamii hiyo iliwaamuru Mashahidi wa Yehova wasikutane tena kwa ajili ya ibada.

 Idara ya sheria ya Ekuado iliwasiliana na idara ya makao makuu ya ulimwenguni pote na kufanya kazi pamoja ili kutetea kutaniko hilo dhidi ya ukiukwaji wa uhuru wao wa ibada. Ndugu hao walipeleka kesi hiyo mahakamani. Hilo lilifanya jamii hiyo iache upinzani huo na kuruhusu kutaniko hilo kuendelea na mikutano na kumaliza ujenzi wa Jumba la Ufalme. Lakini ili kulinda haki za ndugu zetu wakati ujao, wawakilishi wetu waliomba mahakama za juu zitoe uamuzi kuhusu suala la msingi: Je, jamii za wenyeji zinapaswa kuheshimu haki za kibinadamu za kimataifa?

 Julai 16, 2020, Mahakama ya Kikatiba ya Ekuado, ambayo ndiyo mahakama kuu nchini humo, ilisikiliza kesi hiyo. Ndugu ambao ni mawakili nchini Ekuado waliwakilisha kutaniko hilo. Mbali na hilo, ndugu wanne ambao ni mawakili wa kimataifa wenye uzoefu walizungumza mbele ya mahakama hiyo. Kwa sababu ya vizuizi vya ugonjwa wa virusi vya corona (COVID-19), walizungumza kutoka nchi zao kupitia video iliyounganishwa kwenye mtandao. Hiyo ilikuwa ndiyo mara ya kwanza kwa mahakama yoyote ile kuruhusu kikundi cha wanasheria wanaowakilisha Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote kuwasilisha hoja zao kwa njia hiyo. c Kikundi hicho kilitaja mamlaka za kisheria za kimataifa ili kuthibitisha kwamba wenyeji hawawezi kupuuza haki za kibinadamu kwa msingi tu wa kwamba wao ni sehemu ya jamii ya kienyeji.

Kupitia video iliyounganishwa kwenye mtandao, kikundi cha mawakili kutoka mataifa mbalimbali kilitetea haki za ndugu zetu

 Ndugu zetu katika Bonde la Otavalo wanasubiri uamuzi kutoka kwenye Mahakama ya Kikatiba. Kwa sasa, wameguswa moyo sana na msaada ambao wamepata. César, anayetumikia akiwa mzee katika Kutaniko la Ilumán Quichua, anasema hivi: “Ni Yehova tu, kupitia tengenezo lake, anayeweza kufanya mengi kwa ajili ya watu wachache.”

 Mawakili wote waliohusika katika kesi hiyo ni Mashahidi wa Yehova, na walifurahi kutoa ujuzi wao wa kisheria bila malipo. Hata hivyo, kufungua kesi hizo, kuzitayarisha, na kuziwasilisha mahakamani kunagharimu wakati na pesa. Mawakili wetu na ndugu wengine waliokuwepo walitumia zaidi ya saa 380 kutayarisha hoja za kisheria na saa nyingine 240 kutafsiri hati kwa ajili ya kesi iliyofanywa nchini Mexico. Zaidi ya mawakili 40 ulimwenguni pote walitumia mamia ya saa kwa ajili ya kesi iliyofanywa nchini Ekuado. Tulifauluje kulipia gharama zote zilizohusika katika kuwatetea ndugu zetu? Ni kupitia michango ambayo wewe umetoa kupitia mbinu mbalimbali zinazotajwa kwenye donate.isa4310.com. Asante sana kwa ukarimu wako.

a Mashahidi wa Yehova hutafsiri pia katika lugha nyingi za Amerika ya Latini na lugha kadhaa za ishara za eneo hilo.

b Watu wa jamii ya Huichol wanajulikana pia kuwa Wixáritari na mara nyingi lugha yao inaitwa Wixárika.

c Ingawa tengenezo letu la ulimwenguni pote halikuwa sehemu ya kesi hiyo, mahakimu waliwaruhusu ndugu zetu wazungumze mbele ya mahakama wakiwa amicus curiae, yaani, “rafiki wa mahakama.”