Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

JINSI MICHANGO YAKO INAVYOTUMIWA

Kufurahia Kusanyiko Kupitia Vituo vya Habari

Kufurahia Kusanyiko Kupitia Vituo vya Habari

AGOSTI 1, 2021

 Kusanyiko la eneo la 2020 lilikuwa la kihistoria. Kwa mara ya kwanza kusanyiko lilirekodiwa na kupatikana kwenye Intaneti ulimwenguni pote! Hata hivyo, nchini Malawi na Msumbiji, wengi kati ya ndugu na dada zetu walifurahia kusanyiko bila kutumia Intaneti. Hilo liliwezekanaje?

 Halmashauri ya Waratibu na Halmashauri ya Ufundishaji ya Baraza Linaloongoza zilitoa idhini ya pekee kwamba kusanyiko lipeperushwe kupitia televisheni na redio nchini Malawi na Msumbiji. Kwa nini idhini hiyo ilihitajika? Gharama ya huduma za Intaneti nchini Malawi ni kubwa sana kuliko sehemu nyingine ulimwenguni, hivyo ni Mashahidi wachache tu wanaoweza kupata Intaneti. Ndugu William Chumbi, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Malawi alisema hivi: “Redio na televisheni ndiyo njia pekee ya kuwasilisha chakula hicho cha kiroho kwa akina ndugu na dada.” Luka Sibeko, ambaye pia ni mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Malawi aliongezea hivi: “Ikiwa hatungeweza kulipeperusha kupitia TV na redio, ni ndugu wachache tu katika eneo letu la ofisi ya tawi ambao wangeweza kufaidika na kusanyiko.” Nchini Msumbiji vilevile, mbali tu na uwezo wa kupata huduma za Intaneti, ni ndugu wachache tu ambao wana uwezo wa kununua vifaa vya kielektroni.

Kufanya Mipango

 Kwa sababu ya janga la COVID-19, tayari baadhi ya vituo vya televisheni na redio vilikuwa vikipeperusha mikutano ya kutaniko. a Ndugu zetu waliwasiliana na vituo hivyo na kuomba muda wa ziada wa kupeperusha kusanyiko la eneo.

 Nchini Malawi, ndugu zetu walikabili changamoto. Kwa kawaida, vituo vya televisheni na redio huwaruhusu wateja muda wa saa moja tu hewani. Vituo hivyo huogopa kwamba programu zinazozidi muda huo haziwezi kunasa uangalifu wa watu. Lakini ndugu zetu walieleza kwamba kazi yetu ni utumishi kwa umma. Hata wakati huu ambapo watu hawaruhusiwi kuchangamana kwa sababu ya janga la corona, tunawasaidia watu wote kupata ujumbe wenye kufariji wa habari njema kutoka katika Biblia, ambao unaweza kuwasaidia watu kuwa raia wazuri na kuwa na maisha ya familia yenye furaha. Waliposikia hilo, walikubali ombi la ndugu zetu la kupata muda zaidi.

 Nchini Malawi, kusanyiko lilipeperushwa kwenye kituo kimoja cha televisheni na kimoja cha redio. Vituo vyote viwili vinaweza kuwafikia mamilioni ya watu nchini kote. Nchini Msumbiji, kusanyiko lilipeperushwa kwenye kituo kimoja cha televisheni na vituo 85 vya redio.

 Katika nchi zote mbili, jumla ya dola 28,227 b zilitumiwa kupeperusha kusanyiko la eneo kupitia televisheni na dola 20,000 hivi zilitumiwa kulipeperusha kupitia redio. Kituo kidogo zaidi cha redio kiligharimu dola 15 na kituo kinachofikia nchi yote kiligharimu dola 2,777.

 Ndugu zetu walijitahidi sana kutumia michango kwa njia bora zaidi. Kwa mfano, nchini Malawi, walifaulu kupata punguzo la bei katika vituo hivyo, na kituo kimoja hata kiliwapa punguzo la asilimia 30. Punguzo zote zilisaidia kuokoa dola 1,711. Nchini Msumbiji, baadhi ya vituo vilikubali kutupatia punguzo kwa sababu ya sifa yetu nzuri ya kuwa wanyoofu katika malipo na kulipa kwa wakati.

Maneno ya Shukrani

 Ndugu zetu wanathamini sana kutazama au kusikiliza kusanyiko la eneo katika vituo vya kwao. Patrick, mzee nchini Malawi, anasema hivi: “Tunawashukuru ndugu wa Baraza Linaloongoza kwa ufikirio wao wa pekee wakati wa janga hili.” Isaac, ambaye pia anaishi nchini Malawi anasema hivi: “Hatuna vifaa vingine vya kielektroni kwa hiyo, tulishukuru sana kwa uandalizi wa pekee wa tengenezo kutuwezesha kusikiliza kusanyiko kupitia redio. Kwa sababu ya uandalizi huo, familia yangu yote ilinufaika na kusanyiko. Tuliuona kuwa uthibitisho wa upendo wa Yehova kwa watu wake.”

 Mhubiri mmoja nchini Msumbiji alihudhuria kusanyiko la eneo kwa mara ya kwanza mwaka wa 2020. Alisema hivi: “Mpango wa kutazama kusanyiko kwenye TV ulinikumbusha kwamba Yehova ndiye Mungu Mweza-Yote. Janga hili halikumzuia kutupatia chakula cha kiroho kukileta sebuleni mwangu. Niliona uthibitisho wa upendo uliopo miongoni mwa watu wa Yehova. Ninasadiki kwamba hii ndiyo dini ya kweli.”

 Mzee anayeitwa Wyson anasema hivi: “Ningependa kutoa shukrani zangu kwa jinsi mtumwa mwaminifu ametutunza wakati wa janga hili. Uandalizi huu wa kusanyiko la eneo kupeperushwa kupitia redio na TV umewasaidia wengi wetu ambao tuna hali ngumu ya kiuchumi katika sehemu hii maskini ya ulimwengu kupata programu hiyo na kunufaika kutokana nayo.”

 Kwa mara nyingine, Halmashauri ya Waratibu na Halmashauri ya Ufundishaji zimetoa idhini ya pekee kwamba kusanyiko la eneo la 2021 lipeperushwe kupitia televisheni na redio katika maeneo fulani. Hata hivyo, tunafauluje kushughulikia gharama za kupeperusha kusanyiko kwa njia hiyo? Ni kupitia michango ya kazi ya ulimwenguni pote, ambayo mingi inatolewa kupitia njia mbalimbali zinazopatikana kwenye donate.isa4310.com. Asante sana kwa michango yako ya ukarimu.

a Mapema katika mwaka wa 2020, Halmashauri ya Waratibu iliidhinisha mikutano ya kutaniko ipeperushwe kupitia televisheni na redio katika maeneo fulani wakati wa janga la COVID-19. Uandalizi huo umewasaidia wale ambao hawawezi kupata mikutano katika kutaniko lao au kupitia JW Stream kwa kuwa wanaishi katika maeneo ambako huduma za Intaneti na za simu hazipatikani kwa urahisi au kwa gharama nafuu. Hata hivyo, mpango huo haujakusudiwa kwa ajili ya maeneo ambayo yanaweza kuunganisha mikutano ya kutaniko lao.

b Gharama zote za dola katika makala hii zinarejelea dola ya Marekani.