Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uhai Ulianzaje?

Uhai Ulianzaje?

Kamilisha sentensi ifuatayo kwa kuchagua mojawapo ya mambo yaliyotajwa.

UHAI ULITOKANA NA . . .

  1. MAGEUZI

  2. UUMBAJI

 Huenda watu fulani wakafikiri kwamba mtu mwenye akili ya kisayansi atachagua “mageuzi” na kwamba mtu wa kidini atachagua “uumbaji.”

 Lakini haiwi hivyo nyakati zote.

 Ukweli ni kwamba watu wengi wenye elimu​—kutia ndani wanasayansi fulani​—wanatilia shaka usahihi wa nadharia ya mageuzi.

 Fikiria kuhusu Gerard, profesa wa wadudu ambaye alifundishwa mageuzi chuoni. Anasema hivi: “Nilipokuwa nikifanya mitihani, niliwapa maprofesa wangu majibu ambayo walitaka​—lakini sikuamini mambo niliyokuwa nimefundishwa.”

 Kwa nini inakuwa vigumu kwa baadhi ya watu walio na akili ya kisayansi kukubali kwamba uhai ulitokana na mageuzi? Ili kujibu swali hilo, fikiria maswali mawili ambayo huwachanganya wachunguzi wengi: (1) Uhai ulianzaje? na (2) Viumbe hai vilitokeaje?

Uhai Ulianzaje?

 WATU FULANI WANASEMA: Uhai ulijitokeza wenyewe kutokana na vitu visivyo na uhai.

 KWA NINI JIBU HILO HALIWARIDHISHI WATU WENGINE. Leo wanasayansi wanajua mengi kuhusu kemia na muundo wa molekuli zinazofanyiza uhai kuliko wakati mwingine wowote, lakini bado hawawezi kufafanua kwa uhakika uhai ni nini hasa. Chembe ndogo zaidi iliyo hai inatofautiana kwa njia kubwa sana na vitu visivyo hai.

 Wanasayansi wanaweza tu kukisia jinsi hali zilivyokuwa duniani mabilioni ya miaka iliyopita. Wana maoni yanayotofautiana kuhusu mahali ambapo uhai ulianzia​—kwa mfano, wengine wanasema ulianzia ndani ya mlima wa volkano, wengine kwenye sakafu ya bahari. Wengine wanafikiri kwamba vitu vilivyoungana kutokeza uhai vilifanyizwa kwanza katika sehemu nyingine ya ulimwengu kisha vikafikishwa hapa kupitia vimondo. Lakini wazo hilo halionyeshi jinsi uhai ulivyoanza; linaonyesha tu kwamba haukuanzia duniani bali ulianzia angani.

 Wanasayansi wanakisia kwamba kulikuwepo na molekuli nyingine kabla ya molekuli zilizofanyiza chembe za urithi tunazofahamu leo. Wanadai kwamba molekuli hizo zinaweza kujitokeza kutokana na vitu visivyo hai na zina uwezo wa kujigawanya na kutokeza nyingine zinazofanana nazo. Hata hivyo, sayansi haijaweza kupata uthibitisho unaoonyesha kwamba molekuli kama hizo zimewahi kuwepo, wala wanasayansi hawajaweza kutokeza molekuli yoyote kama hiyo katika maabara.

 Viumbe hai huhifadhi na kuchanganua habari kwa njia ya pekee sana. Chembe huwasilisha, kuchanganua, na kutekeleza maagizo yaliyo ndani ya chembe za urithi. Wanasayansi fulani hulinganisha maagizo ya chembe za urithi na programu ya kompyuta, na wanalinganisha muundo wa kikemikali wa chembe na kompyuta yenyewe. Lakini nadharia ya mageuzi haiwezi kueleza habari yote hiyo iliyo ndani ya chembe za urithi ilitoka katika chanzo gani.

 Molekuli za protini zinahitajika ili chembe ziweze kufanya kazi. Molekuli ya protini imefanyizwa kwa mamia ya asidi-amino zilizounganishwa kwa mfuatano uliopangwa kihususa kabisa. Isitoshe, lazima molekuli ya protini iwe na umbo hususa kabisa ili iweze kutumika. Wanasayansi fulani wamefikia mkataa kwamba huenda kusiwe na uwezekano wowote wa molekuli hata moja ya protini kujitokeza yenyewe. Paul Davies, mtaalamu wa fizikia, anaandika hivi: “Kwa kuwa chembe hai inahitaji maelfu ya protini tofauti-tofauti, haipatani na akili kudai kwamba zilijitokeza zenyewe.”

 MKATAA. Baada ya utafiti wa miaka mingi katika nyanja zote za kisayansi, imebainika kwamba uhai unaweza tu kutokezwa na uhai mwingine.

Viumbe Hai Vilitokeaje?

 WATU FULANI WANASEMA: Kiumbe cha kwanza kilibadilika hatua kwa hatua na kutokeza viumbe mbalimbali, kutia ndani wanadamu, kupitia mabadiliko yasiyodhibitiwa ya chembe za urithi na uteuzi wa asili.

 KWA NINI JIBU HILO HALIWARIDHISHI WATU WENGINE. Chembe fulani ni tata kuliko nyingine. Kulingana na kitabu kimoja, inasemekana kwamba kueleza jinsi chembe ambazo si tata sana zilivyobadilika na kuwa tata ni “fumbo kwa wanamageuzi, kama tu ilivyo vigumu kueleza uhai ulianzaje.”

 Wanasayansi wamegundua kwamba katika kila chembe kuna molekuli fulani za pekee zinazofanyizwa na molekuli za protini ambazo hushirikiana ili kutimiza kazi tata sana. Kazi hizo zinatia ndani kusafirisha na kubadili chakula kuwa nishati, kurekebisha sehemu mbalimbali za chembe, na kuwasilisha habari katika sehemu zote za chembe. Je, mabadiliko yasiyodhibitiwa ya chembe za urithi na uteuzi wa asili ungeweza kutokeza chembe na kuzitendesha kwa njia ya pekee kama hiyo? Watu wengi huona kwamba wazo hilo halipatani na akili.

 Uhai wa wanadamu na wanyama huanza chembe mbili zinapoungana, ya kiume na ya kike. Ndani ya kiini-tete hicho, chembe hizo huongezeka, hugawanyika, hujipanga, na kutokeza maumbo tofauti-tofauti na viungo mbalimbali vya mwili. Watu wanaoamini mageuzi hawawezi kueleza jinsi kila chembe “inavyojiambia” kitu cha kutokeza na mahali pa kujipanga ndani ya kiumbe.

 Sasa wanasayansi wanatambua kwamba ili mnyama wa aina fulani abadilike kuwa mnyama wa aina nyingine, mabadiliko hayo lazima yaanzie ndani ya chembe, kwenye molekuli. Kwa kuwa wanasayansi hawawezi kuonyesha jinsi mageuzi yanavyoweza kutokeza hata chembe moja isiyo tata, je, inapatana na akili kwamba wanyama wa aina mbalimbali walio duniani walitokea kupitia mabadiliko yasiyodhibitiwa ya chembe za urithi na uteuzi wa asili? Michael Behe, profesa wa biolojia, alisema hivi kuhusu maumbile ya wanyama: “Ingawa utafiti umeonyesha utata usiotarajiwa na wenye kustaajabisha, hakuna maendeleo yoyote ambayo yamefanywa katika kutuelewesha jinsi utata huo ungetokea kupitia mageuzi na utendaji usio na akili.”

 Wanadamu wanajitambua, wanaelewa mazingira yao, na wana uwezo wa kufikiri na kuchanganua mambo. Vilevile, wana sifa kama vile ukarimu, kujidhabihu, na uwezo wa kutofautisha kati ya mema na mabaya. Mabadiliko yasiyodhibitiwa ya chembe za urithi na uteuzi wa asili hauwezi kueleza kwa nini akili ya mwanadamu ina sifa hizo za pekee.

 MKATAA. Ingawa watu wengi wanasisitiza kwamba nadharia ya kwamba uhai ulitokana na mageuzi ni jambo hakika lisiloweza kupingwa, wengine hawaridhishwi na majibu yanayotolewa na nadharia hiyo kuhusu chanzo cha uhai na jinsi viumbe hai vilivyoenea.

Jibu Linaloridhisha

 Baada ya kuchunguza uthibitisho, watu wengi wanafikia mkataa kwamba uhai ulitokana na mtu mwenye akili nyingi. Fikiria mfano wa Antony Flew, profesa wa falsafa ambaye pindi moja alikuwa mtetezi wa imani ya kwamba hakuna Mungu. Alipojifunza kuhusu utata uliopo katika uhai na sheria za asili za ulimwengu, Flew alibadili maoni yake. Akitumia msemo wa wanafalsafa wa kale, aliandika hivi: “Tunapaswa kukubali mkataa unaotegemea uthibitisho, hata ikiwa hatutarajii mkataa huo.” Profesa Flew aliona kwamba uthibitisho unaonyesha kwamba kuna Muumba.

 Gerard, aliyetajwa mwanzoni mwa makala hii, alifikia mkataa kama huo. Licha ya elimu yake ya juu na kazi yake akiwa mtaalamu wa wadudu, alisema hivi: “Sikupata uthibitisho wowote unaoonyesha kwamba uhai ulijitokeza wenyewe kutoka kwa vitu visivyo hai. Mpangilio na utata uliopo katika viumbe hai ulinisadikisha kwamba lazima kuwe na Mbuni ambaye pia alipanga vitu vyote.”

 Kama tu mtu anavyoweza kujifunza kumhusu msanii kutokana na picha alizochora, Gerard alikuja kugundua sifa za Muumba kwa kuchunguza vitu vya asili. Pia Gerard alitenga wakati kuchunguza kitabu kinachosemekana kilitoka kwa Muumba, yaani, Biblia. (2 Timotheo 3:16) Alipata majibu yenye kuridhisha katika Biblia kuhusu historia ya wanadamu na suluhisho la matatizo ambayo wanadamu wanakabili leo. Hivyo alisadikishwa kwamba Biblia pia ilitokana na mtu mwenye akili kuliko mwanadamu.

 Kama Gerard alivyojifunza, Biblia ina majibu yanayoridhisha. Tunakutia moyo ujichunguzie majibu hayo.