Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jilinde Dhidi ya Habari za Uwongo

Jilinde Dhidi ya Habari za Uwongo

Leo ni rahisi kupata habari kuliko wakati mwingine wowote, kutia ndani habari inayoweza kukusaidia kuwa salama na kudumisha afya nzuri. Hata hivyo, unapotafuta habari unapaswa kuwa mwangalifu dhidi ya habari za uwongo, kama vile:

 Kwa mfano, wakati wa janga la corona (COVID-19), katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa alionya dhidi ya habari za uwongo zinazosambazwa kuhusu janga hilo. Alisema hivi: “Kuna ongezeko la ushauri kuhusu tiba na mbinu za uwongo za kibiashara. Kuna uwongo mwingi unaosambazwa kwenye vyombo vya habari. Fununu zisizo na msingi zinaenezwa kwenye Intaneti. Chuki na ubaguzi unaenezwa kwa kasi dhidi ya watu na jamii mbalimbali.”

 Bila shaka, habari za uwongo hazijaanza kuenezwa juzi. Hata hivyo, Biblia ilitabiri kwamba katika siku zetu, “watu waovu na wajanja wataendelea kutoka ubaya mpaka ubaya zaidi, wakipotosha na kupotoshwa.” (2 Timotheo 3:1, 13) Sasa Intaneti inaturuhusu kupokea—na kueneza bila kukusudia—habari za uwongo kwa urahisi na haraka zaidi kuliko wakati mwingine wowote. Kwa sababu hiyo, barua-pepe yetu, mtandao wa kijamii, taarifa fupi za habari zinaweza kuwa na mambo mengi yaliyopotoshwa na kweli nusunusu.

 Unaweza kufanya nini ili kujilinda dhidi ya habari za uwongo na fununu zisizo na msingi? Fikiria kanuni fulani za Biblia.

  •   Usiamini kila kitu unachoona au kusikia

     Biblia inasema nini: “Mjinga huamini kila neno, lakini mwerevu hutafakari kila hatua.”—Methali 14:15.

     Tusipokuwa waangalifu tunaweza kudanganywa kwa urahisi. Kwa mfano, fikiria picha au video fupi zilizo na maandishi zinazoenezwa sana mtandaoni, hasa kupitia mitandao ya kijamii. Vitu hivyo, ambavyo vinajulikana kama meme, mara nyingi hukusudiwa kuwa vyenye kuchekesha. Hata hivyo, picha na video hizo fupi zinaweza kubadilishwa au kutumiwa kubadili maana ya maneno au tukio fulani kwa sababu hazionyeshi tukio lote. Hata watu wanaweza kutokeza video inayoonyesha watu halisi wakifanya au kusema mambo ambayo hawakuwahi kufanya au kusema.

     “Habari ya uwongo ambayo watafiti wamepata kwenye mitandao ya kijamii inahusisha picha na video zinazopotosha muktadha wa tukio halisi, kama vile meme.”—Axios Media.

     Jiulize: ‘Je, habari hii ni taarifa halisi au ni meme tu?’

  •   Chunguza chanzo na habari yenyewe

     Biblia inasema nini: “Hakikisheni mambo yote.”—1 Wathesalonike 5:21.

     Kabla ya kuamini hadithi fulani na kuisambaza, hata ikiwa inajulikana sana au imerudiwa katika habari, hakikisha ikiwa ni kweli. Jinsi gani?

     Chunguza chanzo chake kinategemeka kadiri gani. Kampuni za vyombo vya habari na mashirika mengine yanaweza kusimulia hadithi fulani kwa njia ambayo inaunga mkono masilahi yao wenyewe ya kibiashara au ya kisiasa. Linganisha kile unachoona katika kituo kimoja cha habari na vyanzo vingine. Nyakati nyingine, huenda marafiki wakashiriki habari za uwongo kupitia barua-pepe au mitandao ya kijamii. Hivyo, usiamini habari fulani isipokuwa uwe unaweza kuchunguza chanzo chake.

     Hakikisha kwamba habari yote ni ya karibuni na ni sahihi. Angalia tarehe, mambo hakika, na uthibitisho wenye nguvu unaounga mkono habari inayozungumziwa. Uwe mwangalifu hasa kuhusu habari tata inayozungumziwa kwa njia nyepesi au ikiwa ripoti yenyewe imekusudiwa kuamsha hisia.

     “Inaonekana kwamba siku hizi kuchunguza mambo hakika kumekuwa muhimu kama tu kunawa mikono.”—Sridhar Dharmapuri, Ofisa wa Ngazi za Juu wa Shirika la Usalama wa Chakula na Lishe la Umoja wa Mataifa.

     Jiulize: ‘Je, ripoti hii ya habari inaficha tofauti kati ya mambo hakika na maoni ya mtu au kutoa upande mmoja tu wa habari?’

  •   Ongozwa na mambo hakika, si mapendezi ya kibinafsi

     Biblia inasema nini: “Yeyote anayeutumaini moyo wake mwenyewe ni mpumbavu.”—Methali 28:26.

     Kwa kawaida tuna mwelekeo wa kuamini habari inayounga mkono jambo tunalotaka kuamini. Mara nyingi kampuni za Intaneti huchanganua habari kuhusu mapendezi yetu na historia yetu ya utafutaji na kuzipatanisha na habari tunazotafuta au zinazojitokeza kwenye mitandao ya kijamii. Hata hivyo, si nyakati zote ambazo kile tunachotaka kusikia ndicho tunachohitaji kusikia.

     “Wanadamu wana uwezo wa kufikiri na kuchanganua mambo, lakini mara nyingi mapendezi, matarajio, woga, na nia yetu hubadili mambo na kufanya iwe rahisi zaidi kukubali kitu kuwa ni kweli maadamu kinaunga mkono tunachotaka kuamini.”—Peter Ditto, mwanasaikolojia wa jamii.

     Jiulize: ‘Je, ninaamini habari hii kwa sababu tu inasema ninachotaka kuamini?’

  •   Komesha kuenea kwa habari za uwongo

     Biblia inasema nini: “Usieneze habari za uwongo.”—Kutoka 23:1.

     Kumbuka kwamba habari unayowapitishia wengine ina uwezo wa kuathiri mawazo na matendo yao. Hata ikiwa unapitisha habari ya uwongo bila kukusudia, inaweza kutokeza madhara.

     “Sheria Na. 1 ni kupunguza mwendo, kutua, na kujiuliza, ʻNina uhakika kadiri gani kuhusu habari hii ili niwaeleze wengine?’ Ikiwa kila mtu angejiuliza swali hilo, kungekuwa na habari chache zaidi za uwongo mtandaoni.”— Peter Adams, naibu msimamizi wa Shirika la Kuwaelimisha Wanahabari.

     Jiulize: ‘Je, ninawaeleza wengine habari hii kwa sababu ninajua ni ya kweli?’