Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 HABARI KUU | UWONGO UNAOFANYA WATU WASIMPENDE MUNGU

Uwongo Unaomfanya Mungu Asiwe na Jina

Uwongo Unaomfanya Mungu Asiwe na Jina

MAONI YA WATU WENGI

“Hatujafikia muafaka ikiwa Mungu ana jina, na ikiwa analo, hatulijui.”—Profesa David Cunningham, Theological Studies.

UKWELI WA BIBLIA

Mungu alisema: “Mimi ni Yehova. Hilo ni jina langu.” (Isaya 42:8) Yehova ni jina la Kiebrania linalomaanisha “Yeye Husababisha Kuwa.”Mwanzo 2:4.

Yehova anataka tutumie jina lake. “Liitieni jina lake,” Biblia inasema. “Tangazeni matendo yake kati ya vikundi vya watu. Semeni kwamba jina lake limeinuliwa juu.”Isaya 12:4.

Yesu alilitumia jina la Mungu. Yesu alisali hivi kwa Yehova: “Nimewajulisha [wanafunzi wa Yesu] jina lako nami nitalijulisha.” Kwa nini Yesu aliwajulisha wanafunzi wake jina la Mungu? Aliendelea kusema hivi: “Ili upendo ulionipenda nao upate kuwa ndani yao nami katika muungano pamoja nao.”Yohana 17:26.

KWA NINI NI MUHIMU?

Mwanatheolojia Walter Lowrie aliandika hivi: “Mtu asiyelijua jina la Mungu hawezi kumwona Mungu kuwa mtu halisi na pia hawezi kumpenda ikiwa anafikiri Mungu ni nguvu isiyo na utu.”

Kuficha au kubadili jina la Mungu ni kama kuliondoa kwenye Biblia

Mwanamume mmoja anayeitwa Victor alienda kanisani kila juma, lakini hakuhisi kwamba anamjua Mungu vizuri. Anasema: “Kisha nilijifunza kwamba Mungu anaitwa Yehova, na hivyo nikamjua rasmi. Nilihisi kama hatimaye nimekutana na Mtu niliyemsikia kwa muda mrefu. Nilianza kumuona kama Mtu halisi na kuanzisha urafiki pamoja naye.”

Yehova huwakaribia wale wanaotumia jina lake. Mungu anawaahidi “wale wanaolifikiria jina lake” hivi: “Nitawaonyesha huruma, kama vile mwanamume anavyomwonyesha huruma mwana wake ambaye anamtumikia.” (Malaki 3:16, 17) Pia, Mungu huwathawabisha wale wanaoliitia jina lake. Biblia inasema hivi: “Kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokolewa.”Waroma 10:13.