Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwisho wa Mateso Umekaribia!

Mwisho wa Mateso Umekaribia!

Wazia ukiishi katika ulimwengu usio na mateso kama vile uhalifu, vita, magonjwa, na misiba ya asili. Wazia ukiamka asubuhi bila kuwa na wasiwasi kuhusu ubaguzi, ukandamizaji, au hali ya uchumi. Bila shaka sote tungependa kuishi katika ulimwengu huo. Hata hivyo, hakuna shirika la kibinadamu linaloweza kuleta hali hizo. Lakini Mungu ameahidi kuondoa mateso yote yanayowapata wanadamu, kutia ndani yale ambayo yamezungumziwa katika makala iliyotangulia. Ona ahadi zifuatazo zilizo katika Neno la Mungu, Biblia:

SERIKALI NZURI

“Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe. Na ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote, nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.”Danieli 2:44.

Ufalme wa Mungu ni serikali ya mbinguni. Yesu Kristo, Mtawala aliyeteuliwa, atatawala dunia yote na atahakikisha kwamba mapenzi ya Mungu yanafanywa duniani kama ilivyo mbinguni. (Mathayo 6:9, 10) Hakuna serikali nyingine itakayochukua mahali pake kwa sababu serikali hiyo ni “ufalme wa milele wa Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo.” Kutakuwa na amani ya kudumu.2 Petro 1:11.

HAKUTAKUWA NA DINI YA UWONGO

“Shetani mwenyewe huendelea kujigeuza mwenyewe kuwa malaika wa nuru. Kwa hiyo si jambo kubwa kama wahudumu wake wakiendelea pia kujigeuza wenyewe kuwa wahudumu wa uadilifu. Lakini mwisho wao utakuwa kulingana na matendo yao.”—2 Wakorintho 11:14, 15.

Dini ya uwongo itafichuliwa na hatimaye kuondolewa kabisa. Hakutakuwa tena na umwagaji wa damu wala ubaguzi wa kidini. Hilo litawezesha wale wanaompenda “Mungu aliye hai na wa kweli” kumtumikia katika “imani moja” na “kwa roho na kweli.” Kutakuwa na amani na umoja kwelikweli!1 Wathesalonike 1:9; Waefeso 4:5; Yohana 4:23.

WANADAMU WATAKUWA WAKAMILIFU

“Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”Ufunuo 21:3, 4.

 Yehova Mungu atafanya yote hayo yawezekane kupitia fidia ya Mwana wake, Yesu, aliyetoa uhai wake kwa ajili ya wanadamu. (Yohana 3:16) Chini ya utawala wa Yesu, wanadamu watakuwa wakamilifu. Hakutakuwa na mateso kwa sababu “Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao” na atafuta “kila chozi kutoka katika macho yao.” Hivi karibuni kutokamilika kwa wanadamu pamoja na mateso yatakuwa mambo ya zamani; “waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”Zaburi 37:29.

HAKUTAKUWA NA MASHETANI

“Naye [Yesu Kristo] akamkamata yule joka mkubwa, yule nyoka wa zamani, ambaye ni Ibilisi na Shetani, na kumfunga kwa miaka elfu. Naye akamtupa ndani ya abiso na kuifunga na kuitia muhuri juu yake, ili asipotoshe mataifa tena.”Ufunuo 20:2, 3.

Uvutano wa Shetani pamoja na roho wake waovu utaisha watakapofungwa na kutupwa ndani ya “abiso,” yaani hali ya kutotenda. Hawatawapotosha tena wanadamu. Itafurahisha sana kuishi katika ulimwengu usio na Shetani wala roho waovu!

“SIKU ZA MWISHO” ZITAKWISHA

“Siku za mwisho” zitafikia kikomo wakati wa kipindi ambacho Yesu alikiita “dhiki kuu.” Yesu alisema hivi: “Ndipo kutakapokuwa na dhiki kuu ya namna ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, hapana, wala haitatukia tena.”Mathayo 24:21.

Dhiki hiyo itakuwa kubwa katika maana ya kwamba kutakuwa na matukio yasiyo ya kawaida. Matukio hayo yatafikia kilele wakati wa “vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote,” inayoitwa “Har–Magedoni.”Ufunuo 16:14, 16.

Watu wanaopenda haki wanatazamia kwa hamu mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo. Acheni tuchunguze baadhi ya baraka zitakazoletwa na Ufalme wa Mungu.

MUNGU ATATIMIZA MAMBO MENGI!

“Umati mkubwa” utaokolewa na kuingia katika ulimwengu mpya wenye amani: Neno la Mungu husema kwamba “umati mkubwa” usioweza kuhesabiwa ‘utatoka katika ile dhiki kuu,’ na kuingia katika ulimwengu mpya wenye uadilifu. (Ufunuo 7:9, 10, 14; 2 Petro 3:13) Watamshukuru Yesu Kristo, “Mwana-Kondoo wa Mungu ambaye huondolea mbali dhambi ya ulimwengu.”Yohana 1:29.

Kutakuwa na faida nyingi kutokana na elimu ya kiroho: Katika ulimwengu mpya, “dunia hakika itajawa na kumjua Yehova.” (Isaya 11:9) Elimu hiyo itatia ndani maagizo ya jinsi ya kuishi kwa amani pamoja na watu na kutunza mazingira. Mungu anaahidi hivi: “Mimi, Yehova, ni Mungu wako, Yeye anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe, Yeye anayekufanya uende katika njia unayopaswa kutembea ndani yake.”Isaya 48:17.

Wapendwa wetu waliokufa watafufuliwa: Alipokuwa duniani, Yesu alimfufua Lazaro, rafiki yake aliyekuwa amekufa. (Yohana 11:1, 5, 38-44) Hivyo Yesu alionyesha yale ambayo atafanya kwa kiwango kikubwa akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu.Yohana 5:28, 29.

Kutakuwa na amani na uadilifu milele: Chini ya utawala wa Yesu, hakutakuwa tena na uasi sheria. Kwa nini tunasema hivyo? Kwa sababu Yesu anaweza kusoma moyo, na atatumia uwezo huo kuhukumu kati ya waadilifu na waovu. Wale ambao watakataa kuacha tabia zao mbaya hawataruhusiwa kuendelea kuishi katika ulimwengu mpya wa Mungu.Zaburi 37:9, 10; Isaya 11:3, 4; 65:20; Mathayo 9:4.

Mambo ambayo tumezungumzia ni baadhi tu ya unabii mwingi wa Biblia ambao utatimizwa wakati ujao. Ufalme wa Mungu utakapoitawala dunia, kutakuwa na “wingi wa amani.” (Zaburi 37:11, 29) Mateso yote ambayo yamewasumbua wanadamu kwa miaka mingi yatakuwa yameondolewa. Neno la Mungu linatuhakikishia hivi: “Tazama! Ninafanya vitu vyote kuwa vipya. . . . Maneno haya ni ya uaminifu na ya kweli.”Ufunuo 21:5.