Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Misiba Itakwisha Hivi Karibuni!

Misiba Itakwisha Hivi Karibuni!

Misiba Itakwisha Hivi Karibuni!

IKIWA mtu fulani angekuambia, “Misiba itakwisha hivi karibuni,” ungetendaje? Huenda ukamjibu, “Wewe unaota. Misiba ni sehemu ya maisha.” Au huenda ukawaza, ‘Anafikiri anaweza kunidanganya?’

Ingawa inaonekana kuwa misiba itaendelea kuwepo, kuna msingi wa kuwa na tumaini hakika kwamba mambo yatabadilika. Hata hivyo, mabadiliko hayo hayataletwa na wanadamu. Wanadamu hawawezi kuelewa kikamili jinsi mambo yanavyotokea au kwa nini yanatokea kiasili, na pia hawawezi kuyazuia au kuyabadili. Mfalme Sulemani wa Israeli la kale, ambaye alijulikana kwa sababu ya hekima yake na kuchunguza mambo kwa makini aliandika: “Wanadamu hawawezi kuvumbua kazi ambayo imefanywa chini ya jua; lakini hata wanadamu waendelee namna gani kufanya kazi kwa bidii kutafuta, bado hawagundui. Na hata wakisema kwamba wana hekima ya kutosha kuweza kujua, hawawezi kuvumbua.”—Mhubiri 8:17.

Ikiwa wanadamu hawawezi kuzuia misiba ya asili, ni nani anayeweza? Biblia inasema kwamba Muumba wetu ndiye anayeweza kuleta mabadiliko hayo. Yeye ndiye aliyeumba mifumo ya kimazingira duniani, kama vile mzunguko wa maji. (Mhubiri 1:7) Na kinyume na wanadamu, Mungu ana nguvu nyingi zisizo na mipaka. Akithibitisha jambo hilo, nabii Yeremia alisema: “Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova! Tazama, wewe mwenyewe umeziumba mbingu na dunia kwa nguvu zako kuu na kwa mkono wako ulionyooshwa. Jambo hilo lote si la ajabu mno kwako.” (Yeremia 32:17) Kwa kuwa Mungu aliumba dunia na vitu vyake vya asili, ni jambo linalopatana na akili kuamini kwamba anajua jinsi ya kuongoza mambo ili watu waishi duniani kwa amani na usalama.—Zaburi 37:11; 115:16.

Basi, Mungu ataletaje mabadiliko yanayohitajiwa? Kumbuka kuwa makala ya pili katika mfululizo huu ilitaja kwamba mambo mengi yenye kutisha ambayo yanatukia duniani leo yanafanyiza “ishara” inayoonyesha “umalizio wa mfumo wa mambo.” Yesu alisema: “Mnapoona mambo hayo yakitukia, jueni kwamba ufalme wa Mungu uko karibu.” (Mathayo 24:3; Luka 21:31) Ufalme wa Mungu, ambao ni serikali ya mbinguni iliyofanyizwa na Mungu, utaleta mabadiliko makubwa duniani, hata utadhibiti nguvu za asili. Ingawa Yehova Mungu ana uwezo wa kufanya jambo hilo, ameamua kumpa Mwana wake kazi hiyo. Nabii Danieli alisema hivi kumhusu: “Naye akapewa utawala na heshima na ufalme, ili vikundi vyote vya watu, vya mataifa na lugha vimtumikie yeye.”—Danieli 7:14.

Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, amepewa nguvu za kutosha kuleta mabadiliko yote yanayohitajiwa ili kufanya dunia iwe mahali penye kupendeza. Yesu alipokuwa duniani miaka elfu mbili hivi iliyopita, alionyesha kwa kiwango kidogo uwezo wake wa kudhibiti nguvu za asili. Pindi moja, yeye na wanafunzi wake walipokuwa ndani ya mashua kwenye Bahari ya Galilaya, ‘kulitokea dhoruba kubwa ya upepo wenye nguvu nyingi, na mawimbi yakawa yakiipiga mashua kwa nguvu, hivi kwamba karibu mashua ifunikwe na maji.’ Wanafunzi wake waliingiwa na hofu na wakaanza kumlilia Yesu kwa sababu waliogopa kufa. Yesu alifanya nini? ‘Aliukemea upepo na kuiambia bahari: “Nyamaza, utulie!” Na upepo ukapunguka, kukawa utulivu mkubwa.’ Wanafunzi wake walishangaa na kuuliza: “Kwa kweli huyu ni nani, kwa sababu hata upepo na bahari zinamtii?”—Marko 4:37-41.

Tangu wakati huo, Yesu ameinuliwa na kwenda mbinguni na amepewa mamlaka na nguvu nyingi zaidi. Akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu, ana jukumu na pia uwezo wa kuhakikisha kwamba watu wanaishi kwa amani na usalama duniani.

Hata hivyo, kama tulivyoona, matatizo na misiba mingi inatokana na wanadamu, yaani, inasababishwa au kufanywa iwe mibaya zaidi na shughuli za watu wenye ubinafsi na pupa. Ufalme huo utawachukulia hatua gani wale wanaoendelea na shughuli hizo na kukataa kubadilika? Biblia inasema kwamba Bwana Yesu atakuja “kutoka mbinguni pamoja na malaika zake wenye nguvu katika mwali wa moto, anapoleta kisasi juu ya wale wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema juu ya Bwana wetu Yesu.” Ndiyo, ‘atawaharibu wale wanaoiharibu dunia.’—2 Wathesalonike 1:7, 8; Ufunuo 11:18.

Baadaye, ‘Mfalme huyo wa wafalme,’ Yesu Kristo, atadhibiti kabisa nguvu za asili za dunia. (Ufunuo 19:16) Atahakikisha kwamba raia wa Ufalme hawatateseka tena kwa sababu ya msiba wowote. Atatumia uwezo wake kuongoza nguvu za asili ili hali ya hewa na majira mbalimbali yawafaidi wanadamu. Matokeo ni kwamba jambo ambalo Yehova Mungu aliwaahidi watu wake zamani za kale litatimia: “Hakika mimi pia nitawapa ninyi manyunyu yenu ya mvua wakati wake unaofaa, nayo nchi itatoa mazao yake, nao mti wa shambani utatoa matunda yake.” (Mambo ya Walawi 26:4) Watu watajenga nyumba bila kuogopa kwamba watazipoteza katika msiba fulani: “Na hakika wao watajenga nyumba na kukaa ndani yake; na hakika wao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake.”—Isaya 65:21.

Unapaswa Kufanya Nini?

Bila shaka, kama watu wengine wengi, wewe pia unavutiwa na ahadi ya kuishi katika ulimwengu usio na misiba inayosababisha uharibifu. Hata hivyo, unapaswa kufanya nini ili uishi katika ulimwengu huo? Kwa kuwa “wale wasiomjua Mungu” na “wale wasiotii habari njema” hawatastahili kuishi katika ulimwengu huo usio na misiba ambao utakuja, ni wazi kwamba ni lazima mtu ajifunze sasa kumhusu Mungu na kuunga mkono mpango wake wa kuitawala dunia. Mungu anataka tumjue na kutii habari njema za Ufalme ambao amesimamisha kupitia Mwana wake.

Kujifunza Biblia kwa makini ndiyo njia bora ya kufanya hivyo. Biblia ina miongozo inayoweza kumsaidia mtu astahili kuishi katika mazingira salama ambayo yatakuwapo chini ya utawala wa Ufalme. Tunakutia moyo uwaombe Mashahidi wa Yehova wakusaidie kujifunza mambo ambayo Biblia inafundisha. Wako tayari kufanya hivyo. Jambo moja ni hakika—ukijitahidi kumjua Mungu na kutii habari njema, basi maneno ya Methali 1:33 yatathibitika kuwa ya kweli kwako: “Kwa habari yake mtu anayenisikiliza, yeye atakaa salama wala hatasumbuliwa na hofu ya msiba.”