Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jina la Mungu na Jitihada za Alfonso de Zamora za Kutokeza Maandishi Sahihi

Jina la Mungu na Jitihada za Alfonso de Zamora za Kutokeza Maandishi Sahihi

Jina la Mungu na Jitihada za Alfonso de Zamora za Kutokeza Maandishi Sahihi

MNAMO mwaka wa 1492, Ferdinand na Isabella, mfalme na malkia wa Hispania, walitoa agizo hili: “Tunawaamuru Wayahudi wote, yaani, wanaume kwa wanawake . . . kwamba kufikia mwisho wa Julai mwaka huu, wawe wameondoka katika maeneo yaliyo chini ya ufalme na miliki yetu. Wanapaswa kuondoka pamoja na wana na binti zao na vijakazi wao wa kiume na wa kike na watu wote wa jamaa zao, wakubwa kwa wadogo, bila kujali umri wao, na wasijaribu kurudi tena.”

Chini ya agizo hilo, kila familia ya Kiyahudi ilipewa nafasi ya kuchagua kati ya kupelekwa uhamishoni au kukana dini yao. Huenda rabi mmoja aliyeitwa Juan de Zamora, alihisi kwamba lingekuwa jambo zuri kubadili dini yake na kuwa Mkatoliki na hivyo kubaki Hispania, nchi ambayo mababu zake walikuwa wameishi kwa miaka mingi. Kwa sababu ya asili yake ya Kiyahudi, inawezekana kwamba Juan alimpeleka mwana wake Alfonso katika shule maarufu ya masomo ya Kiebrania jijini Zamora. Baadaye, Alfonso alipata ujuzi mwingi wa lugha ya Kilatini, Kigiriki, na Kiaramu. Baada ya kumaliza masomo yake, alianza kufundisha Kiebrania katika Chuo Kikuu cha Salamanca. Muda mfupi baadaye, ujuzi wake ulianza kutumiwa na wasomi mbalimbali wa Biblia kotekote barani Ulaya.

Mwaka wa 1512, Chuo Kikuu cha Alcalá de Henares kilimchagua Alfonso de Zamora kusimamia kitengo cha masomo ya Kiebrania. Kwa kuwa Zamora alikuwa mmoja kati ya wasomi stadi wakati huo, kadinali Jiménez de Cisneros, ambaye alianzisha chuo hicho, alimwomba amsaidie kufanya kazi muhimu sana ya kutayarisha Biblia ya Complutensian Polyglot. Biblia hiyo yenye mabuku sita, ina maandishi matakatifu katika Kiebrania, Kigiriki, na Kilatini, na vilevile sehemu fulani katika Kiaramu. *

Kuhusu mradi huo, msomi wa Biblia Mariano Revilla Rico anasema hivi: “Kati ya Wayahudi watatu waliogeuzwa imani ambao walishiriki katika kazi ya Kadinali [Cisneros], Alfonso de Zamora ndiye anayejulikana zaidi. Alikuwa mwanafalsafa, mtaalamu wa sarufi, mtaalamu wa Talmud, na pia msomi wa lugha ya Kilatini, Kigiriki, Kiebrania, na Kiaramu.” Elimu ya Zamora ilifanya afikie mkataa kwamba ili mtu aweze kutafsiri Biblia kwa usahihi, alipaswa kuwa na ujuzi wenye kina wa lugha za awali. Hata alikuja kuwa mmoja kati ya wale waliokuwa mstari wa mbele katika kuwachochea watu wawe wasomi wa Biblia mwanzoni mwa karne ya 16.

Hata hivyo, Zamora aliishi wakati ambapo ilikuwa vigumu na hatari kuwachochea watu wawe wasomi wa Biblia nchini Hispania. Wakati huo Baraza la Kuhukumu Waasi wa Kidini la Hispania lilikuwa limechacha, nalo Kanisa Katoliki lilithamini sana Vulgate ya Kilatini na kuiona kuwa tafsiri pekee ya Biblia “iliyoidhinishwa.” Hata hivyo, tangu wakati wa Enzi za Kati, wasomi wa dini ya Katoliki walikuwa wametambua kwamba maandishi ya Kilatini katika Biblia ya Vulgate hayakuwa sahihi. Kufikia mwanzoni mwa karne ya 16, Alfonso de Zamora na watu wengine walianza kazi ya kutokeza maandishi sahihi.

‘Kazi ya Kutafsiri Ilihitajiwa ili Watu Waokolewe’

Bila shaka, kazi iliyo muhimu zaidi kati ya kazi ambazo Zamora alifanya, ni ile ya kunakili kwa usahihi sehemu ya Biblia ambayo wengi wanaiita Agano la Kale, kutia ndani tafsiri yake ya Kilatini. Huenda alitaka hati hizo zilizosahihishwa zitumiwe sana katika kutayarisha Biblia ya Complutensian Polyglot. Mojawapo ya hati zake inapatikana katika maktaba ya El Escorial iliyo karibu na jiji la Madrid, nchini Hispania. Hati hiyo inayoitwa G-I-4, ina kitabu kizima cha Mwanzo katika Kiebrania, pamoja na tafsiri yake ya neno kwa neno katika Kilatini.

Hati hiyo ina maneno haya kwenye utangulizi wake: “Maandiko Matakatifu yanahitaji kutafsiriwa katika lugha nyingine ili mataifa yaokolewe. . . . Tumeona . . . ni jambo muhimu sana kwamba waaminifu wawe na Biblia iliyotafsiriwa neno kwa neno, yaani, kwa kila neno la Kiebrania kuwe neno lenye maana sawa katika Kilatini.” Alfonso de Zamora alikuwa na ujuzi uliohitajika kutafsiri Biblia hiyo mpya katika Kilatini kwa sababu alikuwa msomi maarufu wa lugha ya Kiebrania.

‘Roho Yangu Haiwezi Kupata Mahali pa Kupumzikia’

Kwa njia moja, Hispania ilikuwa nchi iliyofaa zaidi kwa wasomi kama Zamora kufanyia kazi katika karne ya 16. Katika Enzi za Kati, Hispania ilikuwa kitovu cha utamaduni wa Kiyahudi. Kitabu The Encyclopædia Britannica kinaeleza: “Kwa sababu ya idadi kubwa ya Waislamu na Wayahudi, Hispania ndiyo nchi pekee katika Ulaya magharibi wakati wa Enzi za Kati ambayo ilikuwa na watu wa jamii na dini mbalimbali. Hali hiyo ilichangia kusitawi kwa ustaarabu wa dini, fasihi, sanaa, na majengo nchini humo mwishoni mwa Enzi za Kati.”

Kwa sababu kulikuwa na Wayahudi wengi nchini Hispania, hati za Biblia ya Kiebrania zilikuwa nyingi. Waandishi Wayahudi waliokuwa katika maeneo mengi ya Hispania walijitahidi sana kuandika nakala nyingi za hati hizo ili zitumiwe wakati wa kusoma Maandiko hadharani kwenye masinagogi. Katika kitabu chake The Earliest Editions of the Hebrew Bible, L. Goldschmidt anataja kwamba “si nakala za pentateuki za Kihispania na Kireno pekee zilizojulikana sana kuwa sahihi miongoni mwa wasomi wa Kiyahudi, bali pia hati zilizotumiwa kutokeza nakala hizo na vilevile tafsiri za wasomi zenye lugha nyingi.”

Ingawa Hispania iliwafaa wasomi, upinzani mkubwa ulikuwa umeanza kutokea dhidi ya wale waliotaka kutafsiri Biblia. Katika mwaka wa 1492, majeshi ya Kikatoliki ya Mfalme Ferdinand na Malkia Isabella yaliteka jamii ya mwisho ya Waarabu iliyokuwa Hispania. Kama ilivyotajwa mwanzoni, mwaka huohuo watawala hao waliagiza wafuasi wote wa dini ya Kiyahudi wafukuzwe kutoka Hispania. Miaka kumi baadaye, Waislamu pia waliagizwa waondoke Hispania. Kuanzia wakati huo, dini ya Katoliki ikawa dini ya Taifa ya Hispania, na dini nyingine zikapigwa marufuku.

Hali hiyo mpya ya kidini ingeathirije utafsiri wa Biblia? Yaliyompata Alfonso de Zamora yanaonyesha jinsi mambo yalivyokuwa. Ingawa msomi huyo Myahudi alikuwa amebadili dini yake na kuwa Mkatoliki, wakuu wa Hispania bado walizingatia jamii yake. Wapinzani fulani walimshutumu Kadinali Cisneros kwa kuwa alipotayarisha Biblia ya Polyglot alitumia wasomi Wayahudi waliokuwa wamebadili dini zao. Zamora aliteseka sana kwa sababu ya mashambulizi hayo. Zamora analalamika hivi katika maelezo yaliyo kwenye hati inayopatikana katika Chuo Kikuu cha Madrid: “Mimi, . . . nimeachwa na kuchukiwa na marafiki zangu wote—ambao sasa ni adui zangu—na sina mahali pa kupumzisha roho yangu wala nyayo zangu.”

Mmoja wa adui zake wakubwa alikuwa Juan Tavera, askofu mkuu wa Toledo, ambaye baadaye alikuja kuwa mkuu wa lile baraza la kuwahukumu waasi wa kidini. Zamora alivunjwa moyo sana na mashambulizi ya Tavera hata akakata rufaa kwa papa. Kwa sehemu, barua yake ilisema: “Mtakatifu, tungependa kukuomba utusaidie . . . na kutulinda kutokana na adui yetu askofu wa Toledo, Don Juan Tavera. Kila siku, bila kuacha, anatutesa kwa njia nyingi. . . . Tunahisi uchungu mwingi sana, kwa kuwa machoni pake sisi ni kama wanyama wanaopelekwa machinjoni. . . . Mtakatifu, ikiwa utasikiliza ombi letu, ‘Yahweh atakuwa mlinzi wako na ataulinda mguu wako usitekwe.’ (Met. 3:23)” *

Mambo Ambayo Alfonso de Zamora Alitimiza

Licha ya mashambulizi hayo, kazi ya Zamora iliendelea kufanikiwa na kuwasaidia wanafunzi wengi wa Biblia. Ingawa hakutafsiri Maandiko katika lugha za wakati wake, aliwasaidia sana watafsiri wengine. Ili kuelewa msaada aliotoa, ni lazima tukumbuke kwamba kwa kawaida kutafsiri Biblia kunategemea aina mbili za wasomi. Kwanza, lazima kuwe na wasomi wanaochunguza nakala za maandishi matakatifu katika lugha za awali—Kiebrania, Kiaramu, na Kigiriki—ili watokeze maandishi yaliyorekebishwa na yaliyo sahihi ya lugha hizo. Kisha, mtafsiri anaweza kutumia maandishi hayo kama msingi wa kutafsiri katika lugha yake.

Alfonso de Zamora alikuwa msomi mkuu aliyetayarisha na kurekebisha maandishi ya Kiebrania ambayo mwishowe yalichapishwa katika Biblia ya Complutensian Polyglot, mwaka wa 1522. (Katika Biblia hiyo, sarufi ya Kiebrania na maneno ya Kiebrania yaliyotafsiriwa kwa Kilatini yaliwasaidia sana watafsiri.) Erasmus, aliyeishi wakati mmoja na Zamora, alifanya kazi kama hiyo kuhusiana na Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, yanayojulikana sana kama Agano Jipya. Maandishi hayo yaliyorekebishwa ya Kiebrania na Kigiriki yalipokuwa tayari, watafsiri wengine walianza kazi muhimu ya kutafsiri Biblia katika lugha ambayo watu wangeelewa. Wakati William Tyndale alipotafsiri Biblia katika Kiingereza, alikuwa mmoja wa watafsiri wa kwanza kutumia maandishi ya Kiebrania ya Biblia ya Complutensian Polyglot.

Kusambazwa kwa Biblia kwa wingi leo kunaonyesha wazi kazi nzito iliyofanywa na wanaume kama Zamora ambao walitumia maisha yao ili kutusaidia kuelewa Maandiko vizuri zaidi. Kama Zamora alivyotambua, watu walipaswa kuelewa Neno la Mungu na kulifuata ili wapate wokovu. (Yohana 17:3) Hilo linawezekana tu ikiwa Biblia itatafsiriwa katika lugha ambazo watu wanaweza kuelewa ndiposa ujumbe wake uguse mioyo na akili za mamilioni ya watu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Kwa habari zaidi kuhusu umuhimu wa Biblia ya Complutensian Polyglot, ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Aprili 15, 2004, ukurasa wa 28-31.

^ fu. 15 Inapendeza kuona kwamba Zamora alitumia jina la Mungu, bali si jina la cheo, katika ombi lake kwa papa wa Roma. Katika tafsiri ya Kihispania ya ombi la Zamora, jina hilo ni “Yahweh.” Haijulikani kabisa jinsi jina hilo lilivyokuwa katika maandishi ya Kilatini. Kuhusu tafsiri ya Zamora na matumizi ya jina la Mungu, ona sanduku “Kutafsiri Jina la Mungu” katika ukurasa wa 19.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 19]

Kutafsiri Jina la Mungu

Ni muhimu kutambua jinsi Alfonso de Zamora, mwanamume msomi mwenye asili ya Kiebrania, alivyotafsiri jina la Mungu. Kama picha iliyo katika ukurasa huu inavyoonyesha, Zamora ameandika jina la Mungu kuwa “jehovah” katika maelezo yake ya pambizoni kwenye maandishi yake ya Kiebrania ya kitabu cha Mwanzo ambayo yametafsiriwa neno kwa neno katika Kilatini.

Ni wazi kuwa Zamora alikubali kutafsiriwa kwa jina hilo la Mungu kuwa “jehovah” katika Kilatini. Katika karne ya 16, wakati Biblia ilipotafsiriwa katika lugha kuu zilizotumika Ulaya, watafsiri wengi wa Biblia walitumia jina hilo jinsi lilivyokuwa katika Kilatini au likiwa limebadilishwa kidogo. Watafsiri hao wanatia ndani William Tyndale (Kiingereza, 1530), Sebastian Münster (Kilatini, 1534), Pierre-Robert Olivétan (Kifaransa, 1535) na Casiodoro de Reina (Kihispania, 1569).

Hivyo, Zamora akawa mmoja wa wasomi wa Biblia wa karne ya 16 ambao walisaidia watu kujua jina la Mungu. Jambo lililofanya watu wasilijue jina na Mungu mwanzoni ni kwamba Wayahudi waliacha kulitumia jina hilo kwa sababu za kishirikina. Kwa kufuata mapokeo hayo ya Wayahudi, watafsiri wa Biblia wa dini zinazodai kuwa za Kikristo—kwa mfano, Jerome, mtafsiri wa Vulgate ya Kilatini—waliondoa jina la Mungu na badala yake wakaweka maneno kama “Bwana”au “Mungu.”

[Picha]

Tetragramatoni ya Kiebrania iliyoongezwa ukubwa ambayo Zamora alitafsiri kuwa “yehova”

[Picha katika ukurasa wa 18]

Agizo la mfalme na malkia wa Hispania, 1492

[Hisani ya Picha]

Decree: Courtesy of the Archivo Histórico Provincial, Ávila, Spain

[Picha katika ukurasa wa 18]

Chuo Kikuu cha Alcalá de Henares

[Picha katika ukurasa wa 21]

Picha iliyo kwenye ukurasa wa kwanza wa tafsiri ya Zamora ya neno kwa neno