Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza kujitayarisha sasa kwa ajili ya ulimwengu mpya unaokuja

Paradiso Iko Karibu!

Paradiso Iko Karibu!

Mungu aliumba dunia ili wanadamu waadilifu waishi milele ndani yake. (Zaburi 37:29) Aliwaweka wanadamu wa kwanza, Adamu na Hawa, kwenye bustani maridadi ya Edeni, na aliwapa wao pamoja na wazao wao kazi ya kuilima na kuitunza dunia.​—Mwanzo 1:28; 2:15.

Leo, dunia si Paradiso. Hata hivyo, kusudi la Mungu halijabadilika. Mungu atatimizaje kusudi lake la kuifanya dunia iwe Paradiso? Kama tulivyoona kwenye makala zilizotangulia, Mungu hataiharibu sayari yetu dunia. Badala yake, atawaruhusu wanadamu waaminifu waishi ndani yake. Hali zitakuwaje duniani Mungu atakapotimiza ahadi zake?

Serikali ya ulimwenguni pote

Hivi karibuni, serikali ya Mungu itakapowatawala wanadamu wote, dunia itakuwa mahali pazuri ambapo watu wataishi pamoja kwa umoja, nao watafanya kazi nzuri na zenye kuridhisha. Mungu amemweka rasmi Yesu Kristo kuwa mtawala wa dunia. Tofauti na watawala wengi leo, Yesu atapendezwa kikweli na kutoka moyoni na raia wake. Atakuwa mtawala mwenye upendo, fadhili, huruma, na anayetenda haki.​—Isaya 11:4.

Watu watakuwa na umoja duniani pote

Wanadamu watakaoishi katika ulimwengu mpya hawatagawanyika kwa sababu ya utaifa au ukabila. Wanadamu wote wataungana. (Ufunuo 7:9, 10) Wanadamu wote watakaoishi duniani watampenda Mungu na jirani zao, nao watashirikiana kwa amani kukamilisha kusudi la Mungu la awali la kutunza makao yao, yaani, dunia.​—Zaburi 115:16.

Wanadamu watafurahia mazingira mazuri na yaliyo salama

Ufalme wa Mungu utakapotawala dunia, Muumba wetu atahakikisha hali ya hewa inakuwa nzuri na yenye usawaziko. (Zaburi 24:1, 2) Alipokuwa duniani, Yesu alionyesha kwa kiwango kidogo nguvu alizopewa na Mungu alipotuliza dhoruba yenye kutisha. (Marko 4:39, 41) Chini ya utawala wa Kristo, hakuna mtu yeyote atakayekuwa na sababu ya kuhofia majanga ya asili. Ufalme wa Mungu utahakikisha wanadamu wanafurahia mazingira mazuri na yaliyo salama.​—Hosea 2:18.

Afya kamilifu na chakula kingi

Kila mtu atafurahia afya bora na kamilifu. Hakuna mtu atakayekuwa mgonjwa, kuzeeka, wala kufa. (Isaya 35:5, 6) Watu watafurahia mazingira maridadi na yaliyo safi kama yale ambayo wanadamu wa kwanza waliyafurahia kwenye bustani ya Edeni. Kama ilivyokuwa kwenye bustani ya Edeni, ardhi katika dunia mpya itatokeza chakula kingi, na watu watakuwa na chakula cha kutosha. (Mwanzo 2:9) Kila mtu katika Paradiso ‘atakula mkate na kushiba,’ kama ilivyokuwa katika taifa la Mungu la Israeli la kale.​—Mambo ya Walawi 26:4, 5.

Amani ya kweli na usalama

Chini ya utawala wa Mungu, watu wote watafurahia amani na watatendeana kwa fadhili na haki. Hakutakuwa na vita, matumizi mabaya ya mamlaka, na watu hawatahangaika ili kupata mahitaji yao ya msingi. Biblia inaahidi hivi: “Wataketi, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, na hakuna yeyote atakayewaogopesha.”​—Mika 4:3, 4.

Kila mtu atakuwa na mahali pazuri pa kuishi na kazi yenye kuridhisha

Kila familia itakuwa na nyumba yake bila kuwa na hofu ya kufukuzwa, na kazi zote tutakazofanya zitakuwa zenye kuridhisha. Kama Biblia inavyosema, wale watakaoishi kwenye ulimwengu mpya wa Mungu, “hawatafanya kazi ya bure.”​—Isaya 65:21-23.

Elimu bora

Biblia inaahidi hivi: “Kwa hakika dunia itajaa ujuzi kumhusu Yehova.” (Isaya 11:9) Watu watakaoishi chini ya Ufalme wa Mungu, watajifunza hekima isiyo na mwisho ya Muumba wao, Yehova, na kuhusu vitu vizuri alivyoumba. Hawatatumia ujuzi wao kutengeneza silaha au kuwadhuru wengine. (Isaya 2:4) Badala yake, watajifunza jinsi ya kuishi pamoja kwa amani, na kuitunza dunia.​—Zaburi 37:11.

Uzima wa milele

Mungu aliitayarisha dunia vizuri sana ili tuweze kufurahia maisha kila siku. Anataka wanadamu waishi milele duniani. (Zaburi 37:29; Isaya 45:18) Ili atimize kusudi lake la awali, Mungu “atameza kifo milele.” (Isaya 25:8) Biblia inaahidi hivi: “Kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.” (Ufunuo 21:4) Mungu atawapa wanadamu wote nafasi ya kuishi milele, yaani, wale watakaookoka mfumo huu mwovu utakapoharibiwa na watu wengi watakaofufuliwa katika ulimwengu mpya unaokuja.​—Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15.

Leo, mamilioni ya watu wanajitayarisha ili waweze kuishi chini ya Ufalme wa Mungu ambao uko karibu sana. Ingawa wao si wakamilifu, wanajitahidi kuwa watu ambao Mungu anataka waishi kwenye ulimwengu mpya. Jinsi gani? Kwa kujifunza kumhusu Yehova Mungu na Yesu Kristo, yule aliyetumwa na Mungu.​—Yohana 17:3.

Jifunze mengi zaidi kuhusu jinsi unavyoweza kuokoka mwisho wa ulimwengu huu na kuishi katika ulimwengu bora unaokuja. Waombe Mashahidi wa Yehova wajifunze nawe Biblia bila malipo kwa kutumia kitabu Furahia Maisha Milele!