Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MAONI YA BIBLIA

Pesa

Pesa

Je, pesa ni chanzo cha uovu wote?

“Kupenda pesa ni chanzo cha mambo mabaya ya namna zote.”​—1 Timotheo 6:10.

WATU FULANI HUSEMA NINI?

Pesa ni chanzo cha uovu wote.

BIBLIA INASEMA NINI?

“Kupenda pesa”​—bali si pesa zenyewe​—ndicho chanzo cha “mambo mabaya.” Katika Biblia, Mfalme Sulemani ambaye alikuwa tajiri alitaja mambo matatu mabaya ambayo watu wanaopenda pesa huvuna. Wasiwasi: “Wingi alio nao tajiri haumruhusu kulala.” (Mhubiri 5:12) Kutoridhika: “Anayependa fedha hatatosheka na fedha, wala anayependa mali hatatosheka na mapato.” (Mhubiri 5:10) Kushawishika kuvunja sheria: “Yeye anayefanya haraka kupata utajiri hatabaki pasipo hatia.”​—Methali 28:20.

 Pesa hutimiza kusudi gani?

“Pesa ni ulinzi.”​—Mhubiri 7:12.

WATU FULANI HUSEMA NINI?

Pesa hukufanya uhisi ukiwa salama na mwenye furaha.

BIBLIA INASEMA NINI?

Wazo la kwamba pesa zinaweza kununua furaha na usalama ni sehemu ya “nguvu za udanganyifu za utajiri.” (Marko 4:19) Hata hivyo, “pesa ndizo hutokeza jibu katika mambo yote.” (Mhubiri 10:19) Kwa mfano, pesa zinaweza kununua vitu unavyohitaji ili uendelee kuishi, kama vile chakula na dawa.—2 Wathesalonike 3:12.

Pia, pesa hukusaidia uweze kuitunza familia yako. Kwa kweli, Biblia inasema hivi: “Ikiwa yeyote hawaandalii mahitaji wale walio wake mwenyewe, na hasa wale walio washiriki wa nyumba yake, ameikana imani.”​—1 Timotheo 5:8.

Unaweza kutumiaje pesa kwa hekima?

“Keti kwanza na kuhesabu gharama.”​—Luka 14:28.

BIBLIA INASEMA NINI?

Tumia pesa katika njia ambayo Mungu anakubali. (Luka 16:9) Ni jambo la hekima kutumia pesa vizuri na kwa unyoofu. (Waebrania 13:18) Ili uepuke mzigo wa kuishi maisha yanayozidi mapato yako, ‘namna yako ya maisha inapaswa kuwa bila upendo wa pesa.’​—Waebrania 13:5.

Ingawa Biblia haikatazi kukopa, inaonya hivi: “Mkopaji ni mtumishi wa mtu anayemkopesha.” (Methali 22:7) Epuka kununua vitu ambavyo hujapangia, kwa sababu “kila mtu anayetenda haraka-haraka bila shaka huuelekea uhitaji.” (Methali 21:5) Badala yake, ‘weka kando kitu fulani katika akiba,’ kwa ajili ya mambo yaliyo muhimu kwako.​—1 Wakorintho 16:2.

Biblia inatutia moyo tuwe na “mazoea ya kuwapa watu.” (Luka 6:38) Watu wanaotaka kumpendeza Mungu wana sababu nzuri za kuwa wakarimu kwa sababu “Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.” (2 Wakorintho 9:7) Kwa hiyo, usisahau “kutenda mema na kushiriki vitu pamoja na wengine, kwa maana Mungu hupendezwa vema na dhabihu za namna hiyo.”​—Waebrania 13:16.