Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mungu Anataka Uwe Tajiri?

Je, Mungu Anataka Uwe Tajiri?

Maoni ya Biblia

Je, Mungu Anataka Uwe Tajiri?

“Mungu amenipa siku nyingine mpya! Nitakuwa tajiri!”

“Ninataka kuwa tajiri sana kwa sababu Mungu na malaika wote wanataka niwe tajiri sana.”

“Mungu anatupa uwezo wa kupata mali.”

“Ninafanikiwa kwa sababu ya kile Kitabu [Biblia].”

MANENO hayo yanaonyesha maoni ya watu wengi wa kidini ambao husema kwamba mtu hupata mali kwa sababu ya kubarikiwa na Mungu. Wao huhubiri Injili ya kwamba ukifanya yale ambayo Mungu anataka, Mungu atakupa mali wakati huu na pia atakubariki baadaye. Injili hiyo imewavutia watu wengi na vitabu vinavyoiendeleza vinauzwa kwa wingi. Lakini je, “Injili ya ufanisi” inapatana na Biblia?

Kwa kweli, Muumba wetu, ambaye Biblia inamtaja kuwa “Mungu mwenye furaha” anataka tuwe wenye furaha na tufanikiwe maishani. (1 Timotheo 1:11; Zaburi 1:1-3) Isitoshe, yeye huwabariki wale wanaompendeza. (Methali 10:22) Lakini, je, leo baraka hizo zinakuja kupitia kupata mali? Jibu linakuwa wazi ikiwa tunaelewa umuhimu wa nyakati zetu kuhusiana na kusudi la Mungu.

Je, Huu Ni Wakati wa Kutafuta Utajiri?

Nyakati za kale, Yehova Mungu aliwabariki baadhi ya watumishi wake kwa kuwapa mali. Kwa mfano, Mungu aliwabariki Ayubu na Mfalme Sulemani kwa mali. (1 Wafalme 10:23; Ayubu 42:12) Hata hivyo, kuna watu wengi wenye kumwogopa Mungu kama vile Yohana Mbatizaji na Yesu Kristo, ambao hawakuwa na mali. (Marko 1:6; Luka 9:58) Tunajifunza nini kutokana na hilo? Biblia inaonyesha kwamba Mungu hushughulika na watumishi wake kupatana na kusudi lake wakati huo. (Mhubiri 3:1) Tunaweza kutumia kanuni hiyo leo namna gani?

Unabii wa Biblia unaonyesha kwamba tunaishi katika “umalizio wa mfumo wa mambo,” au “siku za mwisho” za ulimwengu huu. Kipindi hicho kingekuwa na vita, magonjwa, njaa, matetemeko ya nchi, na kuzorota kwa jamii. Mambo hayo yamekumba wanadamu kwa kiwango kikubwa tangu mwaka wa 1914. (Mathayo 24:3; 2 Timotheo 3:1-5; Luka 21:10, 11; Ufunuo 6:3-8) Kwa ufupi, ulimwengu huu ni kama meli iliyo karibu kuzama! Tunapofikiria mambo hayo, je, lingekuwa jambo la akili kwa Mungu kubariki kila mtumishi wake kwa mali, au Mungu angetaka tutangulize mambo mengine muhimu?

Yesu Kristo alilinganisha nyakati zetu na siku za Noa. Yesu alisema: “Kwa maana kama vile walivyokuwa katika siku hizo kabla ya gharika, wakila na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiolewa, mpaka siku ambayo Noa aliingia ndani ya safina; nao hawakujali mpaka gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.” (Mathayo 24:37-39) Yesu pia alilinganisha siku zetu na siku za Loti. Majirani wa Loti huko Sodoma na Gomora walikuwa ‘wakila, wakinywa, wakinunua, wakiuza, wakipanda, na kujenga.’ “Lakini siku ambayo Loti alitoka Sodoma kulinyesha moto na kiberiti kutoka mbinguni na kuwaangamiza wote,” Yesu aliongezea hivi: “Itakuwa vivyo hivyo siku ile ambayo Mwana wa binadamu atafunuliwa.”—Luka 17:28-30.

Kwa kweli, hakuna ubaya wowote kula, kunywa, kufunga ndoa, kununua, na kuuza. Jambo hatari ni kujihusisha sana na mambo hayo hata tusahau umuhimu wa nyakati tunazoishi. Kwa hiyo jiulize, ‘Je, Mungu angekuwa akitufaidi ikiwa angetubariki kwa kutupa vitu ambavyo vingetukengeusha maishani?’ * Badala ya kutufaidi, angekuwa akituhatarisha. Mungu mwenye upendo hatendi kwa njia hiyo! —1 Timotheo 6:17; 1 Yohana 4:8.

Wakati wa Kuokoa Uhai!

Wakati huu muhimu katika historia, watu wa Mungu wana kazi inayopaswa kufanywa haraka. Yesu alisema: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Mashahidi wa Yehova wanachukulia maneno hayo kwa uzito sana. Hivyo, wao huwatia moyo majirani wao wajifunze kuhusu Ufalme na matakwa ya Mungu ya kupata uzima wa milele.—Yohana 17:3.

Hata hivyo, Mungu hataki watumishi wake waaminifu wajinyime raha za maisha. Badala yake, anataka waridhike na mahitaji ya lazima maishani ili wakazie fikira kumtumikia. (Mathayo 6:33) Wanapofanya hivyo, Mungu atahakikisha kwamba wamepata vitu vya kimwili wanavyohitaji. Waebrania 13:5 inasema hivi: “Namna yenu ya maisha iwe bila upendo wa pesa, huku mkiridhika na vitu vya sasa. Kwa maana yeye [Mungu] amesema: ‘Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.’”

Mungu atatimiza ahadi hiyo kwa njia kubwa atakapohifadhi hai “umati mkubwa” wa waabudu wa kweli waokoke mwisho wa mfumo huu wa mambo na kuingia katika ulimwengu mpya wenye amani na ufanisi wa kweli. (Ufunuo 7:9, 14) Yesu alisema: “Mimi nimekuja ili [wafuasi wake waaminifu] wapate kuwa na uzima na wapate kuwa nao kwa wingi.” (Yohana 10:10) ‘Uzima huo mwingi’ si kupata mali nyingi maishani sasa, bali ni uzima usio na mwisho katika Paradiso chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu.—Luka 23:43.

Usikubali kudanganywa na Injili ya ufanisi ambayo kwa kweli ni Injili ya kukengeusha. Badala yake, tii himizo hili la dharura ambalo Yesu alitoa kwa upendo: “Jiangalieni ninyi wenyewe kwamba mioyo yenu isilemewe kamwe na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha, na kwa ghafula siku hiyo iwe juu yenu mara moja kama mtego.”—Luka 21:34, 35.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, leo Wakristo fulani waaminifu ni matajiri. Hata hivyo, Mungu anawaonya kwamba wasitegemee wala kukengeushwa na mali zao. (Methali 11:28; Marko 10:25; Ufunuo 3:17) Wakristo wote, wawe matajiri au maskini, wanapaswa kukazia fikira kufanya mapenzi ya Mungu.—Luka 12:31.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Huu ni wakati uliowekwa wa kufanya nini?—Mathayo 24:14.

▪ Yesu alilinganisha siku zetu na siku za watu gani wanaotajwa katika Biblia?—Mathayo 24:37-39; Luka 17:28-30.

▪ Ni lazima tuepuke nini ili tupate uzima wa milele?—Luka 21:34.

[Blabu katika ukurasa wa 13]

Injili ya ufanisi kwa kweli ni Injili ya kukengeusha