Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAONI YA BIBLIA

Malaika

Malaika

Malaika wamezungumziwa katika vitabu mbalimbali, michoro, na sinema. Hata hivyo, malaika ni nani, nao wana jukumu gani?

Malaika ni nani?

BIBLIA INASEMA NINI?

 

Kabla ya Mungu kuumba ulimwengu na wanadamu, tayari alikuwa ameumba viumbe wenye akili sana kuliko wanadamu. Wana nguvu nyingi kuliko wanadamu, nao wanaishi mbinguni pamoja na Mungu, mahali ambapo wanadamu hawawezi kuingia au kupaona. (Ayubu 38:4, 7) Katika Biblia, viumbe hao wenye uwezo mkubwa wanaitwa “roho” au “malaika.”—Zaburi 104:4. *

Kuna malaika wangapi? Wengi sana. Malaika wanaokizunguka kiti cha enzi cha Mungu ni “makumi ya maelfu ya makumi ya maelfu na maelfu ya maelfu.” (Ufunuo 5:11) Ikiwa usemi huo si wa mfano, basi kuna mamia ya mamilioni ya malaika!

“Nami nikaona . . . malaika wengi kuzunguka kile kiti cha ufalme . . . , na hesabu yao ilikuwa makumi ya maelfu ya makumi ya maelfu na maelfu ya maelfu.”—Ufunuo 5:11.

Malaika walitimiza majukumu gani nyakati za kale?

BIBLIA INASEMA NINI?

 

Malaika walitumiwa wakiwa wajumbe au wasemaji wa Mungu. * Pia, Biblia inasema kwamba Mungu aliwatumia kufanya miujiza. Mungu alimtuma malaika kumbariki na kumzuia Abrahamu asimtoe mwana wake Isaka kuwa dhabihu. (Mwanzo 22:11-18) Malaika alimtokea Musa katika mwali wa moto katikati ya mti wa miiba na kumletea ujumbe ambao ungebadili maisha yake. (Kutoka 3:1, 2) Nabii Danieli alipotupwa katika shimo la simba, “Mungu . . . alimtuma malaika wake na kufunga vinywa vya simba.”—Danieli 6:22.

“Ndipo malaika wa Yehova akamtokea [Musa] katika mwali wa moto katikati ya mti wa miiba.”—Kutoka 3:2.

Malaika wanafanya nini wakati wetu?

BIBLIA INASEMA NINI?

 

Hatuwezi kujua mambo yote ambayo malaika wanafanya leo. Hata hivyo, Biblia inasema kwamba wanashiriki kuwasaidia watu wenye mioyo minyofu wamjue Mungu.—Matendo 8:26-35; 10:1-22; Ufunuo 14:6, 7.

Katika ndoto, Yehova alimwonyesha mzee wa ukoo Yakobo malaika wakipanda na kushuka kwenye “ngazi” iliyotoka duniani hadi mbinguni. (Mwanzo 28:10-12) Baada ya kuota ndoto hiyo, huenda Yakobo alifikia mkataa ambao sisi pia tunaweza kukubaliana nao, kwamba Yehova Mungu huwatuma malaika wake duniani watimize majukumu mbalimbali ili kuwasaidia wanadamu washikamanifu wanaohitaji msaada.—Mwanzo 24:40; Kutoka 14:19; Zaburi 34:7.

“Kulikuwa na ngazi iliyosimamishwa juu ya dunia na kilele chake kilikuwa kimefika mbinguni; na, tazama! malaika za Mungu walikuwa wakipanda na kushuka juu yake.”—Mwanzo 28:12.

^ fu. 6 Biblia husema kwamba baadhi ya viumbe wa roho waliasi mamlaka ya Mungu, na malaika hao wabaya wanaitwa “roho waovu.”—Luka 10:17-20.

^ fu. 11 Maneno ya awali ya Kiebrania na Kigiriki yanayotumiwa katika Biblia kurejelea “malaika” yanamaanisha “mjumbe.”