Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | NDOA

Jinsi ya Kuzungumzia Matatizo

Jinsi ya Kuzungumzia Matatizo

KIKWAZO

Wewe na mwenzi wako mnapozungumzia matatizo, je, ninyi humaliza mazungumzo mkiwa mmekasirika? Ikiwa ndivyo, mnaweza kuboresha hali hiyo. Kwanza, mnahitaji kujua kwamba wanaume na wanawake huwasiliana kwa njia tofauti. *

MAMBO UNAYOHITAJI KUJUA

Kwa kawaida wanawake hupenda kusikilizwa kwanza wanapoeleza matatizo kabla ya kupata suluhisho. Kwa kweli, wakati fulani kuzungumza kuhusu tatizo ni suluhisho kwao.

“Ninajihisi vizuri ninapoeleza hisia zangu na kujua kwamba mume wangu amenielewa. Kwa kawaida mimi hujihisi vizuri sana muda mfupi tu baada ya kuzungumzia jambo hilo.”—Sirppa. *

“Siwezi kujihisi vizuri ikiwa sijamweleza mume wangu tatizo linalonisumbua. Baada ya kumweleza mimi hutulia.” —Ae-Jin.

“Kujieleza ni kama kujichunguza kibinafsi. Ninapoongea, mimi huchanganua tatizo na kuelewa chanzo chake.” —Lurdes.

Kwa kawaida wanaume hufikiria haraka jinsi ya kutatua matatizo. Hilo linaeleweka, kwa sababu mwanaume huhisi vizuri anapofaulu kutatua jambo fulani. Kusuluhisha tatizo ni njia ya mwanaume kumthibitishia mke kuwa anaweza kumtegemea anapohitaji msaada. Hivyo, waume hujihisi vibaya msaada wao unapokataliwa. Mume anayeitwa Kirk anasema hivi: “Sielewi kwa nini mtu aongee kuhusu matatizo ikiwa hataki suluhisho la matatizo hayo!”

Lakini kitabu The Seven Principles for Making Marriage Work kinaonya hivi, “Ni muhimu kuelewa jambo kabla ya kutoa ushauri. Ni muhimu mwenzi wako ajue kwamba unaelewa vizuri tatizo lake na unamhurumia kabla ya kutoa suluhisho. Si mara zote mwenzi wako wa ndoa anahitaji suluhisho la jambo fulani, bali anataka tu umsikilize kwa makini.”

MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Mume: Msikilize mke wako kwa makini na ujaribu kuelewa hisia zake. Mume anayeitwa Tomás anasema: “Baada ya kumsikiliza mke wangu nyakati fulani mimi hujiambia hivi, ‘Sijatimiza jambo lolote.’ Lakini mara nyingi kusikilizwa ndilo jambo ambalo mke wangu anahitaji.” Mume anayeitwa Stephen anakubaliana naye. Anaongezea hivi: “Nimeona kuwa ni vizuri kumwacha mke wangu ajieleze bila kumkatisha, na mara nyingi baada ya kunieleza yeye huniambia kuwa anahisi vizuri zaidi.”

Jaribu kufanya hivi: Unapozungumza na mke wako kuhusu matatizo, epuka kutoa suluhisho haraka. Mtazame usoni, na umsikilize kwa makini. Tikisa kichwa kuonyesha unakubaliana naye. Rudia aliyosema ili kuonyesha kwamba unamwelewa. Mume anayeitwa Charles anasema, “wakati mwingine mke wangu anahitaji tu kujua kwamba ninamwelewa na ninamuunga mkono.”—Kanuni ya Biblia: Yakobo 1:19.

Mke: Mwambie mume wako jambo ambalo ungependa afanye. Mke anayeitwa Eleni anasema; “Huenda ukadhani kwamba mume anajua kitu unachohitaji, lakini wakati fulani ni muhimu kumweleza mahitaji yako.” Mke anayeitwa Ynez, anapendekeza kusema hivi: “Kuna jambo linalonisumbua ambalo ningependa kukueleza. Si kwamba ninahitaji suluhisho, lakini ningependa ujue vile ninavyohisi.”

Jaribu kufanya hivi: Ikiwa mume wako hutoa suluhisho haraka, usikate kauli kwamba hakujali. Huenda anajaribu kupunguza uzito wa tatizo. Mke anayeitwa Ester anasema hivi: “Badala ya kukasirika, mimi hujaribu kuelewa kwamba mume wangu ananijali na anataka kunisikiliza, lakini pia anapenda kunisaidia.”—Kanuni ya Biblia: Waroma 12:10.

Mume na Mke: Kwa kawaida tunataka kuwatendea wengine kama vile tunavyotaka watutendee. Hata hivyo, ili uzungumzie matatizo kwa njia nzuri, unahitaji kujua jinsi mwenzi wako anavyotaka kutendewa. (1 Wakorintho 10:24) Mume anayeitwa Miguel anasema hivi: “Mume, anahitaji kuwa tayari kusikiliza. Mke, uwe tayari wakati fulani kukubali suluhisho. Mkiwa tayari kushirikiana, wote wawili mtafaidika sana.”—Kanuni ya Biblia: 1 Petro 3:8.

^ fu. 4 Huenda mambo tutakayozungumzia yasihusu wenzi wote wa ndoa. Hata hivyo, kanuni zinazotajwa katika makala hii zinaweza kumsaidia mtu yeyote aliyefunga ndoa kumwelewa mwenzi wake na kuwasiliana naye vizuri.

^ fu. 7 Majina katika makala hii yamebadilishwa.