Hamia kwenye habari

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | NDOA

Jinsi ya Kutumia Teknolojia kwa Usawaziko

Jinsi ya Kutumia Teknolojia kwa Usawaziko

 Matumizi ya teknolojia yanaweza kuboresha au kudhoofisha ndoa yako. Teknolojia inaathirije ndoa yako?

 Unachopaswa kujua

  •   Kutumia teknolojia kwa hekima kunaweza kuwa na faida kubwa katika ndoa. Kwa mfano, wenzi fulani hutumia teknolojia kuwasiliana wakati ambapo hawapo pamoja.

     “Ujumbe mfupi tu unaosema ‘Nakupenda’ au ‘Ninakufikiria’ unaweza kugusa moyo sana.”—Jonathan.

  •   Kutumia teknolojia bila hekima kunaweza kudhoofisha ndoa. Kwa mfano, baadhi ya watu hutumia vifaa vyao kila wakati, na hivyo wanakosa kumpa mwenzi wao wakati na uangalifu anaohitaji.

     “Nina hakika kuna pindi ambazo mume wangu alitaka kuzungumza nami lakini nilikuwa nikitumia simu yangu.”—Julissa.

  •   Baadhi ya watu husema kwamba wanaweza kuwa na mazungumzo ya kina na wenzi wao huku wakitumia vifaa vyao. Mwanasosholojia Sherry Turkle anasema kwamba “watu fulani hufikiri wanaweza kufanya zaidi ya jambo moja kwa wakati mmoja, lakini hilo haliwezekani.” Na kwa kweli, hilo si jambo zuri. Anaongezea kusema, “ubora wa utendaji wetu hupungua tunapofanya zaidi ya jambo moja kwa wakati mmoja.” a

     “Kuzungumza na mume wangu ni jambo lenye kufurahisha sana, lakini sihisi hivyo anapofanya jambo lingine huku akizungumza nami. Akifanya hivyo ni kana kwamba ananiambia anaweza kuwa na furaha akiwa na vifaa vyake tu.”—Sarah.

 Jambo kuu: Matumizi yako ya teknolojia yanaweza kusaidia au kuathiri ndoa yako.

 Unachoweza kufanya

 Fahamu mambo ya kutanguliza. Biblia inasema: “Mhakikishe mambo muhimu zaidi.” (Wafilipi 1:10) Jiulize, ‘Je, mimi na mwenzi wangu hutumia vifaa vyetu kwa muda mwingi kuliko tunaotumia pamoja?’

 “Inasikitisha kuona mwanamume na mwanamke wakiwa mkahawani wakitumia simu zao badala ya kuzungumza pamoja—ni kana kwamba wametekwa na vifaa vyao. Hatungependa kuwa watumwa wa teknolojia na kusahau jambo muhimu zaidi—uhusiano wetu.”—Matthew.

 Weka mipaka. Biblia inasema: “Endeleeni kuangalia sana jinsi mnavyotembea, si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, mkiutumia vizuri kabisa wakati wenu.” (Waefeso 5:15, 16) Jiulize, ‘Je, ninaweza kutenga muda hususa wa kusoma na kujibu jumbe ambazo hazina uharaka badala ya kuzijibu mara moja?’

 “Nimeona kwamba inasaidia sana kuzima mlio wa simu yangu halafu kujibu jumbe zinazoingia kwa wakati mwafaka zaidi. Ni mara chache sana kwamba utakuta kuna simu, ujumbe, au barua-pepe ya dharura sana ambayo inahitaji kujibiwa mara moja.”—Jonathan.

 Ikiwezekana, acha kazi ibaki kazini. Biblia inasema hivi: “Kuna wakati uliowekwa wa kila jambo.” (Mhubiri 3:1) Jiulize maswali haya: ‘Je, ninaruhusu shughuli za kazi ziathiri maisha ya nyumbani kwa kutumia simu kufanyia kazi nyumbani? Kama ndivyo, jambo hilo linaathirije ndoa yangu? Mwenzi wangu angejibuje swali hilo?’

 “Kwa sababu ya teknolojia, tuna uwezo wa kufanya kazi wakati wowote. Nilihitaji kujitahidi sana ili niepuke kutazama simu yangu kila wakati au kushughulikia mambo yanayohusu kazi ninapokuwa na mke wangu.”—Matthew.

 Zungumzia matumizi ya teknolojia pamoja na mwenzi wako. Biblia inasema: “Kila mmoja na aendelee kutafuta, si faida yake mwenyewe, bali faida ya yule mtu mwingine.” (1 Wakorintho 10:24) Zungumza na mwenzi wako kuhusu jinsi kila mmoja wenu anavyotumia teknolojia na ikiwa kuna mabadiliko yoyote mnayohitaji kufanya. Mnaweza kuanza kwa kutumia mwongozo wa mazungumzo ulio katika makala hii.

 “Mimi na mume wangu huambiana ukweli sikuzote, na tunajulishana ikiwa tunahisi kwamba mmoja wetu anatumia simu au tablet yake kupita kiasi. Sisi sote tunatambua kwamba hili linaweza kuwa tatizo, hivyo tunazingatia sana maoni ya kila mmoja.”—Danielle.

 Jambo kuu: Hakikisha wewe si mtumwa wa teknolojia.

a Kutoka kwenye kitabu Reclaiming Conversation—The Power of Talk in a Digital Age.