Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Yohana 1:1​—“Hapo Mwanzo Neno Alikuwako”

Yohana 1:1​—“Hapo Mwanzo Neno Alikuwako”

 “Hapo mwanzo Neno alikuwako, naye Neno alikuwa pamoja na Mungu, na Neno alikuwa mungu.”—Yohana 1:1, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Hapo mwanzo kulikuwako Neno, naye Neno alikuwako kwa Mungu, naye Neno alikuwa Mungu.”—Yohana 1:1, Union Version.

Maana ya Yohana 1:1

 Andiko hili linazungumzia maisha ya Yesu Kristo kabla ya kuja duniani akiwa mwanadamu. (Yohana 1:14-17) Katika mstari wa 14 “Neno” (au “Logos,” Kigiriki, ho loʹgos) hutumika kama jina la cheo. Inaonekana jina la cheo “Neno” linafafanua jukumu la Yesu la kuwajulisha wengine sheria na maagizo ya Mungu. Yesu aliendelea kutangaza neno la Mungu wakati wa huduma yake hapa duniani na baada ya kurudi mbinguni.—Yohana 7:16; Ufunuo 1:1.

 “Mwanzo” unaotajwa unarejelea wakati ambapo Mungu alianza kazi ya uumbaji kutia ndani kumuumba Neno. Kisha, Neno alitumiwa na Mungu katika kuumba vitu vingine vyote. (Yohana 1:2, 3) Biblia inasema kwamba Yesu ni “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote” na kwamba “kupitia kwake vitu vingine vyote viliumbwa.”—Wakolosai 1:15, 16.

 Maneno “Neno alikuwa mungu” yanaonyesha kwamba Yesu alikuwa na uwezo wa kimungu kabla ya kuja duniani. Inaweza kusemwa hivyo kumhusu kwa sababu ya jukumu lake akiwa Msemaji wa Mungu na nafasi yake ya pekee akiwa Mwana mzaliwa wa kwanza wa Mungu ambaye kupitia kwake Mungu aliumba vitu vingine vyote.

Muktadha wa Yohana 1:1

 Kitabu cha Biblia cha Yohana kinasimulia maisha na huduma ya Yesu alipokuwa duniani. Mistari ya mwanzo ya sura ya kwanza inasimulia maisha ya Yesu kabla ya kuja duniani, uhusiano wake wa pekee na Mungu, na nafasi yake muhimu inayowezesha Mungu kushughulika na wanadamu. (Yohana 1:1-18) Mambo hayo yanatusaidia kuelewa yale ambayo Yesu alisema na kutenda wakati wa huduma yake duniani.—Yohana 3:16; 6:38; 12:49, 50; 14:28; 17:5.

Maoni Yasiyo Sahihi Kuhusu Yohana 1:1

 Maoni yasiyo sahihi: Maneno ya mwisho katika Yohana 1:1 yanapaswa kutafsiriwa “Neno alikuwa Mungu.”

 Ukweli: Ingawa watafsiri wengi wa Biblia wametafsiri mstari huo hivyo, wengine wameona umuhimu wa kuutafsiri kwa njia tofauti. Katika lugha ya awali, maneno “Mungu” (Kigiriki, the·osʹ) yanayopatikana mara mbili katika Yohana 1:1, yanatofautiana kisarufi. Linapotokea mara ya kwanza, neno “Mungu” linatanguliwa na kibainishi wazi cha Kigiriki, na linapotokea mara ya pili katika neno hilo, kibainishi wazi hakitumiwi. Wasomi wengi wanasema kwamba kukosekana kwa kibainishi wazi kabla ya the·osʹ ya pili ni jambo la msingi. Kwa mfano, kitabu The Translator’s New Testament kinasema hivi kuhusu kukosekana kwa kibainishi wazi: “Kwa njia fulani, hali hiyo huipa sifa ya kuwa kivumishi matumizi ya pili ya neno Theos (Mungu) ili maneno hayo yamaanishe “Neno alikuwa wa kimungu.’” a Wasomi wengine b na tafsiri za Biblia zinataja tofauti hiyo pia.—Ona “ Yohana 1:1 Kulingana na Tafsiri Nyingine.”

 Maoni yasiyo sahihi: Mstari huo unafundisha kwamba Neno ni sawa na Mungu Mweza-Yote.

 Ukweli: Maneno “Neno alikuwa pamoja na Mungu” yanaonyesha kwamba watu wawili tofauti wanazungumziwa katika mstari huo. Ni jambo lisilowezekana kwa Neno kuwa “pamoja na Mungu” na wakati huohuo awe Mungu Mweza-Yote. Muktadha unathibitisha pia kwamba Neno si Mungu Mweza-Yote. Yohana 1:18 inasema kwamba “hakuna mwanadamu ambaye amemwona Mungu wakati wowote.” Hata hivyo, watu walimwona Neno, Yesu, kwa kuwa Yohana 1:14 inasema “Neno akawa mwili, akakaa kati yetu, nasi tukauona utukufu wake.”

 Maoni yasiyo sahihi: Neno amekuwapo siku zote.

 Ukweli: “Mwanzo” unaorejelewa katika mstari huu hauwezi kumaanisha “mwanzo” wa Mungu, kwa sababu Mungu hana mwanzo. Yehova c Mungu ni wa “tangu milele hadi milele.” (Zaburi 90:1, 2) Hata hivyo, Neno, Yesu Kristo, alikuwa na mwanzo. Yeye ni “mwanzo wa uumbaji wa Mungu.”—Ufunuo 3:14.

 Maoni yasiyo sahihi: Kumwita Neno “mungu” ni kufundisha ibada ya miungu wengi.

 Ukweli: Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “Mungu” au “mungu” (the·osʹ) mara nyingi hufanana na maneno ya Kiebrania ʼel na ʼelo·himʹ, yanayotumiwa katika ile inayoitwa Agano la Kale. Kimsingi, maneno hayo ya Kiebrania humaanisha “Mwenye Uwezo; Mwenye Nguvu” na hutumiwa kumaanisha Mungu mweza yote, miungu wengine, na hata wanadamu. (Zaburi 82:6; Yohana 10:34) Mungu aliumba kila kitu kupitia Neno, hivyo anaweza kutajwa kwa kufaa kuwa mwenye nguvu. (Yohana 1:3) Kumfafanua Neno kuwa “mungu” kunalingana na unabii katika Isaya 9:6, uliotabiri kwamba yule atakayechaguliwa na Mungu, Masihi au Kristo, angeitwa “Mungu Mwenye Nguvu” (Kiebrania, ʼEl Gib·bohrʹ), wala si “Mungu Mweza-Yote” (ʼEl Shad·daiʹ, kulingana na Mwanzo 17:1; 35:11; Kutoka 6:3; Ezekieli 10:5).

 Biblia haifundishi kuabudu miungu mingi. Yesu Kristo alisema: “Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.” (Mathayo 4:10) Biblia inasema hivi: “Kwa maana hata ingawa kuna wale wanaoitwa miungu, iwe ni mbinguni au duniani, kama vile kulivyo na ‘miungu’ mingi na ‘mabwana’ wengi, kwa kweli kwetu kuna Mungu mmoja aliye Baba, ambaye vitu vyote vimetoka kwake na sisi kwa ajili yake; na kuna Bwana mmoja, Yesu Kristo, ambaye vitu vyote vimepitia kwake na sisi kupitia kwake.”—1 Wakorintho 8:5, 6.

 Yohana 1:1 Kulingana na Tafsiri Nyingine

 “Katika mwanzo alikuwa Neno, na Neno alikuwa pamoja na Mungu, Neno alikuwa Mungu.”—Yoane 1:1, Zaire Swahili Bible

 “Hapo mwanzo, Neno alikuwako; naye alikuwa na Mungu, naye alikuwa Mungu.”—Yohane 1:1, Biblia Habari Njema

 “Mwanzoni Neno alikuwako, naye Neno alikuwa kwa Mungu, naye Neno alikuwa Mungu.”—Yoane 1:1, Verbum Bible

 “Mwanzoni, kabla ya kuumbwa ulimwengu, Neno alikuwako; naye alikuwa na Mungu, naye alikuwa Mungu.”—Yohane 1:1, Biblia Takatifu Agano Jipya

a Kitabu The Translator’s New Testament, ukurasa wa 451.

b Msomi Jason David BeDuhn anasema kwamba kukosekana kwa kibainishi wazi hufanya mitajo miwili ya neno “Mungu” “kuwa sawa na tofauti iliyopo katika neno ‘mungu’ na ‘Mungu’ katika lugha ya Kiingereza.” Anaongezea hivi: “Katika Yohana 1:1, Neno si Mungu yule wa pekee, bali ni mungu, au mwenye uwezo wa kimungu.”—Kitabu Truth in Translation: Accuracy and Bias in English Translations of the New Testament, ukurasa wa 115, 122, na 123.

c Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu.—Zaburi 83:18.