Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Yohana 14:6​—“Mimi ndiye Njia na Kweli na Uzima”

Yohana 14:6​—“Mimi ndiye Njia na Kweli na Uzima”

 “Yesu akamwambia: ‘Mimi ndiye njia na kweli na uzima. Hakuna mtu anayekuja kwa Baba bila kupitia kwangu.’”—Yohana 14:6, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Yesu akamwambia, ‘Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.’”—Yohana 14:6, Union Version.

Maana ya Yohana 14:6

 Ikiwa mtu anataka kumwabudu Baba, Yehova a Mungu, anapaswa kutambua jukumu muhimu la Yesu.

 “Mimi ndiye njia.” Yesu ndiye “njia” inayokubalika ya kumfikia Mungu. Kwa mfano, watu wanaosali kwa Mungu, wanapaswa kufanya hivyo katika jina la Yesu. (Yohana 16:23, 24) Kifo cha Yesu kimewawezesha wanadamu kupatanishwa na Mungu, au kupata kibali chake. (Waroma 5:8-11) Yesu pia aliweka mfano wa mwenendo ambao wale wanaotaka kumpendeza Mungu wanapaswa kuufuata.—Yohana 13:15.

 “Mimi ni . . . kweli.” Yesu alisema na kuishi kupatana na kweli sikuzote. (1 Petro 2:22) Kwa kumsikiliza yeye, mtu angeweza kujifunza kweli kumhusu Mungu. (Yohana 8:31, 32) Yesu pia ni “kweli” kwa sababu alitimiza unabii wa Biblia. Hivyo, alifanya ahadi za Mungu kuwa kweli.—Yohana 1:17; 2 Wakorintho 1:19, 20; Wakolosai 2:16, 17.

 “Mimi ni . . . uzima.” Yesu alitoa uhai wake ili wale wanaomwamini waweze kupata uzima wa milele. (Yohana 3:16, 36) Yeye pia ni “uzima” kwa wale waliokufa kwa sababu atawafufua.—Yohana 5:28, 29; 11:25.

 “Hakuna mtu anayekuja kwa Baba bila kupitia kwangu.” Wale wanaotaka kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu wanapaswa kukubali jukumu la pekee la Yesu. Wanafanya hivyo kwa kusali kwa Mungu kupitia jina la Yesu, na hivyo kuonyesha kwamba wanatambua mamlaka ya Yesu Kristo. (Yohana 15:16) Pia wanatambua kwamba wokovu unawezekana kwa sababu tu ya Yesu.—Matendo 4:12; Wafilipi 2:8-11.

Muktadha wa Yohana 14:6

 Yohana sura ya 13 hadi ya 17, zina mashauri ya mwisho ambayo Yesu aliwapa mitume wake 11 waaminifu usiku kabla ya kifo chake. Katika sura ya 14, Yesu aliwatia moyo wanafunzi wake wawe na imani katika yeye na Baba yake, na wampende na kumtii yeye na Baba yake. (Yohana 14:1, 12, 15-17, 21, 23, 24) Alionyesha kwamba sikuzote yeye na Baba yake wana uhusiano wa karibu. (Yohana 14:10, 20, 28, 31) Ijapokuwa muda mfupi baada ya hapo angerudi mbinguni, aliwahakikishia wanafunzi wake kwamba hangewaacha. (Yohana 14:18) Pia aliwaahidi kwamba watapata “msaidizi” na akafafanua msaidizi huyo kuwa “roho takatifu, ambayo Baba ataituma katika jina langu.” (Yohana 14:25-27) Kwa njia hiyo na nyingine nyingi, Yesu aliwatayarisha wafuasi kwa ajili ya hali nyingi ngumu ambazo wangekabili wakati ujao.