Hamia kwenye habari

Yesu Alikuwa na Sura ya Aina Gani?

Yesu Alikuwa na Sura ya Aina Gani?

Jibu la Biblia

 Hakuna mtu anayejua kabisa Yesu alikuwa na sura ya aina gani, kwa kuwa Biblia haifafanui umbo lake. Hilo linaonyesha kwamba mwonekano wa nje wa Yesu si jambo muhimu. Hata hivyo, Biblia inatusaidia kupata wazo fulani kuhusu umbo lake.

  •   Sura: Yesu alikuwa Myahudi na inaelekea alirithi sifa za Kiyahudi kutoka kwa mama yake. (Waebrania 7:​14) Haielekei kwamba alikuwa na sura ya pekee sana. Pindi moja alisafiri kwa siri kutoka Galilaya hadi Yerusalemu bila kutambuliwa. (Yohana 7:​10, 11) Na inaonekana kwamba sura yake haikuwa tofauti sana na ile ya wanafunzi wake wa karibu. Kumbuka kwamba Yuda Iskariote alihitaji kumtambulisha Yesu kwa ule umati wenye silaha uliokuja kumkamata.​—Mathayo 26:47-​49.

  •   Urefu wa nywele: Haielekei kwamba Yesu alikuwa na nywele ndefu kwa kuwa Biblia inasema kwamba “mwanamume akiwa na nywele ndefu, ni aibu kwake.”​—1 Wakorintho 11:14.

  •   Ndevu: Yesu alikuwa na ndevu. Alifuata sheria ya Kiyahudi, ambayo iliwakataza wanaume ‘wasiharibu ncha ya ndevu zao.’ (Mambo ya Walawi 19:27; Wagalatia 4:4) Pia, Biblia inataja ndevu za Yesu katika unabii uliohusu kuteseka kwake.​—Isaya 50:6.

  •   Mwili: Mambo yote yanaonyesha kwamba Yesu alikuwa na mwili wenye nguvu sana. Wakati wa huduma yake, alisafiri kilomita nyingi. (Mathayo 9:​35) Alisafisha hekalu la Wayahudi mara mbili, akipindua meza za waliokuwa wakibadili pesa, na kufukuza mifugo wote kwa kutumia mjeledi. (Luka 19:45, 46; Yohana 2:​14, 15) Kitabu McClintock and Strong’s Cyclopedia kinasema hivi: “Simulizi lote la injili linaonyesha kwamba [Yesu] alikuwa na mwili wenye afya na nguvu.”​—Buku la 4, ukurasa wa 884.

  •   Ishara za uso: Yesu alikuwa mchangamfu na mwenye huruma, na bila shaka uso wake ulionyesha hilo. (Mathayo 11:28, 29) Watu wa aina zote walimtafuta ili awafariji na kuwasaidia. (Luka 5:​12, 13; 7:​37, 38) Hata watoto walijihisi wakiwa wametulia walipokuwa naye.​—Mathayo 19:13-​15; Marko 9:​35-​37.

Maoni yasiyo sahihi kuhusu sura ya Yesu

 Maoni yasiyo sahihi: Watu fulani wanadai kwamba Yesu alikuwa na asili ya Kiafrika kwa sababu kitabu cha Ufunuo kinalinganisha nywele zake na sufu na miguu yake na “shaba safi.”​—Ufunuo 1:​14, 15.

 Ukweli: Kitabu cha Ufunuo kimetolewa kwa njia ya “ishara.” (Ufunuo 1:1) Ufafanuzi wa nywele na miguu ya Yesu unatumia lugha ya mfano kuonyesha sifa za Yesu baada ya kufufuliwa, si kufafanua sura yake alipokuwa duniani. Ufunuo 1:14 inaposema kwamba “kichwa chake na nywele zake zilikuwa nyeupe kama sufu nyeupe” inatumia rangi wala haijaribu kuonyesha jinsi zilivyokuwa zinapoguswa. Rangi hiyo inawakilisha hekima yake kwa sababu ya umri. (Ufunuo 3:14) Mstari huu haujaribu kuonyesha jinsi nywele za Yesu zilivyo zinapoguswa kwa kulinganishwa na sufu ilivyo inapoguswa kama tu ambavyo haizilinganishi na theluji inapoguswa.

 Miguu ya Yesu ilionekana kama “shaba safi inapowaka katika tanuru.” (Ufunuo 1:​15) Pia, sura yake “ilikuwa kama jua linapoangaza katika nguvu zake.” (Ufunuo 1:​16) Kwa kuwa hakuna watu duniani walio na ngozi yenye rangi kama hiyo, lazima maono hayo yawe yalikuwa ya mfano, yakionyesha kwamba Yesu aliyefufuliwa alikuwa yule “anayekaa katika nuru isiyoweza kufikiwa.”​—1 Timotheo 6:16.

 Maoni yasiyo sahihi: Yesu alikuwa dhaifu na mnyonge.

 Ukweli: Yesu hakuwa dhaifu. Kwa mfano, alijitambulisha kwa ujasiri umati wenye silaha ulipokuja kumkamata. (Yohana 18:​4-8) Pia, lazima Yesu awe alikuwa na mwili wenye nguvu ili aweze kufanya kazi akiwa seremala kwa kutumia vifaa vilivyohitaji atumie nguvu nyingi.​—Marko 6:3.

 Basi, kwa nini Yesu alihitaji msaada kubeba mti wake wa mateso? Na kwa nini alikufa kabla ya wale wengine waliouawa pamoja naye? (Luka 23:26; Yohana 19:31-​33) Kabla tu ya Yesu kuuawa, mwili wake ulidhoofishwa sana. Hakuwa amelala usiku mzima, sababu moja ikiwa ni kwa sababu ya kuteseka kihisia. (Luka 22:42-​44) Usiku wote Wayahudi walikuwa wamemtendea kwa ukatili, na asubuhi iliyofuata Waroma walimtesa. (Mathayo 26:67, 68; Yohana 19:​1-3) Inaelekea mambo hayo yalifanya afe haraka zaidi.

 Maoni yasiyo sahihi: Pindi zote Yesu alikuwa na huzuni.

 Ukweli: Yesu alionyesha kikamilifu sifa za Baba yake wa mbinguni, Yehova ambaye Biblia inamfafanua kuwa “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:11; Yohana 14:9) Kwa kweli, Yesu aliwafundisha wengine jinsi ya kuwa na furaha. (Mathayo 5:​3-9; Luka 11:28) Mambo hayo yanaonyesha kwamba mara nyingi uso wa Yesu ulionyesha kwamba alikuwa mwenye furaha.