Hamia kwenye habari

Je, Biblia Inafundisha ‘Ukiokolewa, Umeokolewa Milele’?

Je, Biblia Inafundisha ‘Ukiokolewa, Umeokolewa Milele’?

Jibu la Biblia

 Hapana, haifundishi wazo la kwamba ‘ukiokolewa, umeokolewa milele.’ Mtu akipata wokovu kwa kuwa na imani katika Yesu Kristo anaweza kupoteza imani na wokovu unaotokana na imani hiyo. Biblia inasema kwamba ili mtu adumishe imani anapaswa kutia jitihada nyingi, afanye “pigano kali.” (Yuda 3, 5) Wakristo wa mapema ambao tayari walikuwa wamemkubali Kristo waliambiwa hivi: “Endeleeni kuufanyia kazi wokovu wenu wenyewe kwa kuogopa na kutetemeka.”​—Wafilipi 2:​12.

Mistari ya Biblia inayopinga fundisho la kwamba ‘ukiokolewa, umeokolewa milele’

  •   Biblia inaonya dhidi ya kufanya dhambi nzito ambazo zitamzuia mtu kuingia katika Ufalme wa Mungu. (1 Wakorintho 6:9-11; Wagalatia 5:19-21) Ikiwa mtu hawezi kupoteza wokovu, maonyo kama hayo hayangekuwa na maana. Badala yake, Biblia inaonyesha kwamba mtu ambaye ameokolewa anaweza kuanguka kwa kufanya dhambi nzito. Kwa mfano, Waebrania 10:26 inasema: “Tukizoea kutenda dhambi kimakusudi baada ya kupokea ujuzi sahihi juu ya kweli, hakuna tena dhabihu yoyote iliyobaki kwa ajili ya dhambi.”​—Waebrania 6:​4-6; 2 Petro 2:20-22.

  •   Yesu alikazia umuhimu wa kudumisha imani alipotoa mfano ambao alijilinganisha na mzabibu na akawalinganisha wafuasi wake na matawi ya mzabibu huo. Baadhi yao wangeonyesha imani kwa muda kwa kutokeza matunda, yaani, matendo yao, lakini baadaye wangeacha na hivyo ‘watupwe nje kama tawi’ lisilozaa matunda. Kwa sababu hiyo wangepoteza wokovu wao. (Yohana 15:1-6) Mtume Paulo alitumia mfano kama huo, akisema kwamba Wakristo ambao hawaendelei kuwa na imani ‘wangekatwa.’​—Waroma 11:17-​22.

  •   Wakristo wanaamriwa ‘waendelee kukesha.’ (Mathayo 24:42; 25:13) Watu wanaolala kiroho, iwe ni kwa kutenda “matendo ya giza” au kwa kutotenda matendo ambayo Yesu aliamuru, wanapoteza wokovu wao.​—Waroma 13:11-13; Ufunuo 3:​1-3.

  •   Maandiko mengi yanaonyesha kwamba wale ambao wameokolewa wanapaswa kuvumilia kwa uaminifu hadi mwisho. (Mathayo 24:13; Waebrania 10:36; 12:2, 3; Ufunuo 2:10) Wakristo wa karne ya kwanza walishangilia walipofahamu kwamba waamini wenzao walikuwa wakidumisha imani yao. (1 Wathesalonike 1:​2, 3; 3 Yohana 3, 4) Je, inapatana na akili kwamba Biblia ikazie umuhimu wa mtu kuvumilia kwa uaminifu ikiwa wale ambao hawajavumilia wataokolewa pia?

  •   Ni wakati tu ambapo alikuwa karibu kufa ndipo mtume Paulo alihisi kwamba wokovu wake ni hakika. (2 Timotheo 4:​6-8) Mapema maishani mwake alitambua kwamba anaweza kukosa kuokolewa ikiwa angefuatilia tamaa za kimwili. Aliandika hivi: “Naupigapiga mwili wangu na kuuongoza kama mtumwa, ili, baada ya mimi kuwahubiria wengine, mimi mwenyewe nisikataliwe kwa njia fulani.”​—1 Wakorintho 9:27; Wafilipi 3:12-​14.