Hamia kwenye habari

Roho Takatifu Ni Nini?

Roho Takatifu Ni Nini?

Jibu la Biblia

 Roho takatifu ni nguvu za utendaji za Mungu. (Mika 3:8; Luka 1:​35) Mungu huituma roho yake kwa kuelekeza nguvu zake mahali popote anapotaka ili kutimiza mapenzi yake.​—Zaburi 104:30; 139:7.

 Katika Biblia, neno “roho” limetafsiriwa kutokana na neno la Kiebrania ruʹach na neno la Kigiriki pneuʹma. Mara nyingi, maneno hayo hurejelea nguvu za utendaji za Mungu, au roho takatifu. (Mwanzo 1:2) Hata hivyo, Biblia pia hutumia maneno hayo kwa njia nyingine:

 Maana hizo zote zinatoa wazo la kitu kisichoonekana na wanadamu ambacho hufanya mambo yanayoweza kuonekana. Vivyo hivyo, roho ya Mungu, “kama tu upepo, haionekani, si kitu halisi, na ina nguvu.”​—An Expository Dictionary of New Testament Words, by W. E. Vine.

 Biblia pia hurejelea roho takatifu ya Mungu kuwa “mikono” au “vidole” vyake. (Zaburi 8:3; 19:1; Luka 11:20; linganisha Mathayo 12:28.) Kama tu msanii anavyotumia mikono na vidole vyake kufanya kazi zake, Mungu ametumia roho yake kutokeza vitu kama hivi:

Roho takatifu si mtu

 Inaporejelea roho ya Mungu kama “mikono,” “vidole,” au “pumzi” yake, Biblia inaonyesha kwamba roho takatifu si mtu. (Kutoka 15:​8, 10) Mikono ya msanii haiwezi kufanya kazi bila akili au mwili wake; vivyo hivyo, roho takatifu ya Mungu hutenda tu anapoielekeza. (Luka 11:13) Pia Biblia hulinganisha roho ya Mungu na maji na kuihusianisha na vitu kama vile imani na ujuzi. Ulinganifu huo huonyesha kwamba roho takatifu si mtu.​—Isaya 44:3; Matendo 6:5; 2 Wakorintho 6:6.

 Biblia hutueleza majina ya Yehova Mungu na ya Mwana wake, Yesu Kristo; hata hivyo, hakuna mahali inapotaja jina la roho takatifu. (Isaya 42:8; Luka 1:​31) Yule mfia-imani Mkristo Stefano alipoona maono ya kimuujiza mbinguni, aliona watu wawili, si watatu. Biblia inasema: “Yeye, akiwa amejaa roho takatifu, akakaza macho mbinguni, akaona utukufu wa Mungu na wa Yesu akiwa amesimama kwenye mkono wa kuume wa Mungu.” (Matendo 7:​55) Roho takatifu ilikuwa nguvu za utendaji za Mungu zilizomwezesha Stefano kuona maono hayo.

Maoni yasiyo sahihi kuhusu roho takatifu

 Maoni yasiyo sahihi: Roho takatifu ni mtu na ni sehemu ya Utatu, kama inavyotajwa katika 1 Yohana 5:​7-9 katika Biblia ya Union Version.

 Ukweli: Katika 1 Yohana 5:​7-9, Biblia ya Union Version imeongeza maneno “mbinguni, Baba, na Neno, na Roho Mtakatifu, na watatu hawa ni umoja. Kisha wako watatu washuhudiao duniani.” Hata hivyo, watafiti wamegundua kwamba maneno hayo hayakuandikwa na mtume Yohana kwa hiyo hayapaswi kuwa katika Biblia. Profesa Bruce M. Metzger aliandika hivi: “Ni jambo la hakika kwamba maneno hayo ni bandia na hayapaswi kuwa katika Agano Jipya.”​—A Textual Commentary on the Greek New Testament.

 Maoni yasiyo sahihi: Biblia huzungumza kuhusu roho takatifu kana kwamba ina uhai, na hilo linathibitisha kwamba roho hiyo ni mtu.

 Ukweli: Nyakati nyingine Maandiko huzungumza kuhusu roho takatifu kana kwamba ina uhai. Kwa mfano, Yesu aliitaja roho takatifu kana kwamba ni mtu alipoirejelea kuwa “msaidizi” (paraclete) ambaye angetoa ushahidi, angeongoza, angesema, angesikia, angetangaza, angetukuza, na kupokea. (Yohana 16:​7-​15) Lakini hilo halimaanishi kwamba roho takatifu ni mtu. Biblia huzungumza pia kuhusu hekima, kifo, na dhambi kana kwamba zina uhai. (Methali 1:​20; Waroma 5:​17, 21) Kwa mfano, hekima inasemekana kuwa ina “matendo” na “watoto,” nayo dhambi inatajwa kuwa ina uwezo wa kushawishi, kuua, na kufanyiza tamaa.​—Mathayo 11:19; Luka 7:​35; Waroma 7:​8, 11.

 Maoni yasiyo sahihi: Ubatizo katika jina la roho takatifu unathibitisha kwamba ni mtu.

 Ukweli: Nyakati nyingine Biblia hutumia neno “jina” kuwakilisha nguvu au mamlaka. (Kumbukumbu la Torati 18:​5, 19-​22; Esta 8:​10) Mtu anayebatizwa “katika jina la” roho takatifu anatambua nguvu na fungu la roho takatifu katika kutimiza mapenzi ya Mungu.​—Mathayo 28:19.

 Maoni yasiyo sahihi: Mitume wa Yesu na wanafunzi wengine wa mapema waliamini kwamba roho takatifu ilikuwa mtu.

 Ukweli: Biblia haisemi hivyo, na historia pia haionyeshi hivyo. Kitabu Encyclopædia Britannica kinasema: “Ufafanuzi wa kwamba Roho Takatifu ni Mtu wa kimungu . . . ulianza kwenye Baraza la Constantinople katika mwaka wa 381 baada ya Kristo.” Hiyo ilikuwa zaidi ya miaka 250 baada ya mtume wa mwisho kufa.