Hamia kwenye habari

Babiloni Mkubwa Ni Nani?

Babiloni Mkubwa Ni Nani?

Jibu la Biblia

 Babiloni Mkubwa, anayefafanuliwa katika kitabu cha Ufunuo, anawakilisha dini zote za uwongo ambazo Mungu hakubali. a (Ufunuo 14:8; 17:5; 18:21) Ingawa dini hizo hutofautiana katika mambo kadhaa, zote huongoza watu mbali na ibada ya Mungu wa kweli, Yehova.​—Kumbukumbu la Torati 4:35.

Mambo Yanayomtambulisha Babiloni Mkubwa

  1.   Babiloni Mkubwa ni jina la mfano. Biblia inamrejelea kama “mwanamke” na “kahaba mkubwa,” anayeitwa jina la ‘fumbo: “Babiloni Mkubwa.”’ (Ufunuo 17:​1, 3, 5) Kitabu cha Ufunuo kimeandikwa “kwa njia ya ishara” kwa hiyo inafaa kusema kwamba Babiloni Mkubwa ni jina la mfano, si mwanamke halisi. (Ufunuo 1:1) Kwa kuongezea, ‘anakaa juu ya maji mengi’ ambayo yanawakilisha “watu na umati na mataifa na lugha.” (Ufunuo 17:​1, 15) Haiwezekani kwa mwanamke halisi kufanya jambo hilo.

  2.   Babiloni Mkubwa ni milki ya ulimwenguni pote. Anatajwa kuwa “jiji kubwa lililo na ufalme juu ya wafalme wa dunia.” (Ufunuo 17:18) Kwa hiyo, ana uvutano katika mataifa yote.

  3.   Babiloni Mkubwa ni shirika la kidini, si la kisiasa wala la kijamii. Babiloni la kale lilikuwa jiji lililojaa mambo ya kidini, ambalo lilijulikana kwa “maapizo” yake ya kuwasiliana na pepo na “ulozi.” (Isaya 47:​1, 12, 13; Yeremia 50:​1, 2, 38) Jiji hilo liliendeleza dini ya uwongo iliyompinga Mungu wa kweli, Yehova. (Mwanzo 10:​8, 9; 11:​2-4, 8) Watawala wa Babiloni walijiinua juu ya Yehova na ibada yake. (Isaya 14:​4, 13, 14; Danieli 5:​2-4, 23) Vivyo hivyo, Babiloni Mkubwa anajulikana kwa mazoea yake ya “kuwasiliana na pepo.” Hilo linamtambulisha kuwa shirika la kidini.​—Ufunuo 18:23.

     Babiloni Mkubwa hawezi kuwa shirika la kisiasa, kwa sababu “wafalme wa dunia” wanaomboleza uharibifu wake. (Ufunuo 17:​1, 2; 18:9) Pia yeye si muungano maarufu wa kibiashara, kwa sababu Biblia inamtofautisha na “wanabiashara wa dunia.”​—Ufunuo 18:11, 15.

  4. Jiwe la maandishi la Mfalme Nabonido wa Babiloni likiwa na ishara za miungu wa utatu Sini, Ishtari, na Shamashi

      Dini ya uwongo inapatana kabisa na ufafanuzi wa Babiloni Mkubwa. Badala ya kufundisha watu jinsi ya kumkaribia Mungu wa kweli, Yehova, dini ya uwongo huwaongoza kuabudu miungu mingine. Biblia hutaja jambo hilo kuwa “uasherati” wa kiroho. (Mambo ya Walawi 20:6; Kutoka 34:15, 16) Imani kama vile Utatu na kutokufa kwa nafsi, na mazoea kama kutumia sanamu katika ibada, yalitoka katika Babiloni la kale na yanapatikana katika dini ya uwongo hadi leo. Dini hizi huchanganya ibada yao na mambo ya ulimwengu. Biblia hurejelea ukosefu huo wa uaminifu kuwa uzinzi wa kiroho.​—Yakobo 4:4.

     Utajiri na kujionyesha kwa dini ya uwongo kunapatana kabisa na jinsi Biblia inavyomfafanua Babiloni Mkubwa kuwa “amevikwa nguo za rangi ya zambarau na nyekundu,” na “alikuwa amepambwa dhahabu na jiwe la thamani na lulu.” (Ufunuo 17:4) Babiloni Mkubwa ndiye chanzo cha mafundisho na matendo yasiyomheshimu Mungu yanayotajwa kuwa “machukizo ya dunia.” (Ufunuo 17:5) Washiriki wa dini ya uwongo wanafafanuliwa kuwa “watu na umati na mataifa na lugha” wanaomuunga mkono Babiloni Mkubwa.​—Ufunuo 17:15.

 Babiloni Mkubwa ndiye kisababishi cha vifo vya “wale wote ambao wameuawa juu ya dunia.” (Ufunuo 18:24) Historia inaonyesha kwamba dini ya uwongo haijachochea tu vita na matendo ya kigaidi bali pia imeshindwa kuwafundisha watu ukweli kumhusu Mungu mwenye upendo, Yehova. (1 Yohana 4:8) Jambo hili limesababisha umwagaji mkubwa wa damu. Kwa sababu hiyo, wale wanaotaka kumpendeza Mungu lazima ‘watoke kwake,’ na hivyo kujiepusha na dini ya uwongo.​—Ufunuo 18:4; 2 Wakorintho 6:​14-​17.