Hamia kwenye habari

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | KULEA WATOTO

Watoto na Mitandao ya Kijamii​—Sehemu ya 2: Mfundishe Kijana Wako Kutumia Mitandao ya Kijamii kwa Njia Salama

Watoto na Mitandao ya Kijamii​—Sehemu ya 2: Mfundishe Kijana Wako Kutumia Mitandao ya Kijamii kwa Njia Salama

 Baada ya kufikiria hatari zilizopo, wazazi wengi wameamua kwamba watoto wao hawatatumia mitandao ya kijamii. Ikiwa utamruhusu kijana wako kutumia mitandao ya kijamii, unaweza kufanya nini ili umsaidie kuepuka madhara ya mitandao hiyo na kutenda kwa njia inayofaa mtandaoni?

Katika makala hii

 Kijana wako anatanguliza mambo gani?

 Unachopaswa kujua: Ni rahisi sana kuwa mraibu wa mitandao ya kijamii, basi msaidie kijana wako kudhibiti kiasi cha muda anaotumia kwenye mitandao hiyo.

 Kanuni ya Biblia: “Mhakikishe mambo muhimu zaidi.”​—Wafilipi 1:10.

 Jambo la kufikiria: Je, kijana wako hutumia mitandao ya kijamii muda ambao anapaswa kulala, kufanya kazi za shule au kuwa pamoja na wengine katika familia? Wataalamu wanasema kwamba vijana wanahitaji kulala kwa saa tisa hivi kila siku, lakini inaelekea kwamba wale wanaotumia mitandao ya kijamii kwa saa kadhaa kila siku, wanalala chini ya saa saba.

 Unachoweza kufanya: Zungumza pamoja na kijana wako kuhusu mambo anayopaswa kutanguliza na umwonyeshe kwa nini ni jambo la hekima kudhibiti muda anaotumia katika mitandao ya kijamii. Weka sheria zenye usawaziko, kwa mfano usiruhusu matumizi ya vifaa vya kielektroni kwenye chumba cha kulala wakati wa usiku. Lengo lako ni kumsaidia kijana wako akuze sifa ya kujizuia na sifa hiyo itamsaidia hata atakapokuwa mtu mzima.​—1 Wakorintho 9:25.

 Kijana wako ataathiriwaje kihisia?

 Unachopaswa kujua: Kijana anapotazama picha za wengine ambazo zimeboreshwa kwa njia za kielektroni ili zipendeze zaidi, au mambo ya kujifurahisha wanayofanya, huenda akahisi upweke au kushuka moyo.

 Kanuni ya Biblia: “Acheni . . . wivu.”​—1 Petro 2:1.

 Jambo la kufikiria: Je, mitandao ya kijamii inamfanya kijana wako ahisi vibaya kuhusu mwonekano wake anapojilinganisha na wengine? Je, kijana wako anahisi kwamba watu wengine wote, wanafurahia maisha isipokuwa yeye?

 Unachoweza kufanya: Zungumza pamoja na kijana wako kuhusu hatari za kujilinganisha na wengine. Ni vizuri kujua kwamba huenda wasichana wakaathiriwa zaidi kuliko wavulana kwa sababu wasichana hufikiria zaidi kuhusu masuala ya urafiki na pia kuhusu mwonekano wao. Huenda hata ukapendekeza kijana wako aache kutumia mitandao ya kijamii kwa muda fulani. Kijana anayeitwa Jacob anasema hivi: “Niliacha kutumia mitandao ya kijamii kwa muda fulani. Kufanya hivyo kulinisaidia kutanguliza mambo yanayofaa na kuwa na maoni mazuri kujihusu na kuwahusu wengine.”

 Kijana wako atajiendeshaje kwenye mtandao?

 Unachopaswa kujua: Kutumia mitandao ya kijamii ni kama kuishi mbele ya umati. Kwa sababu hiyo kutoelewana na kukosana kutatokea mara kwa mara.

 Kanuni ya Biblia: “Acheni kabisa kila aina ya chuki yenye uhasama, hasira, ghadhabu, kufoka, matusi . . . Bali mtendeane kwa fadhili.”​—Waefeso 4:31, 32.

 Jambo la kufikiria: Je, mitandao ya kijamii imemfanya kijana wako aanze kupiga porojo, kukosana na wengine, au hata kuzungumza bila fadhili?

 Unachoweza kufanya: Msaidie kijana wako kuelewa jinsi ya kujiendesha vizuri kwenye mtandao. Kitabu Digital Kids kinasema hivi: “Ni jukumu letu tukiwa wazazi kuwafundisha watoto wetu kwamba hawapaswi kuwa wajeuri iwe wanazungumza na mtu moja kwa moja au kwenye mtandao.”

 Kumbuka kwamba si lazima kijana atumie mitandao ya kijamii na pia si wazazi wote ambao wanaruhusu vijana wao kuitumia. Ukimruhusu kijana wako kutumia mitandao ya kijamii, hakikisha kwamba ana ukomavu wa kutosha kudhibiti muda anaotumia kwenye mitandao hiyo, anaweza kudumisha marafiki wazuri, na kuepuka mambo yasiyofaa.