Hamia kwenye habari

APRILI 23, 2020
EKUADO

Mashahidi Nchini Ekuado Wahubiri Kutoka Nyumbani

Mashahidi Nchini Ekuado Wahubiri Kutoka Nyumbani

Ndugu na dada zetu ulimwenguni pote wanaendelea kubadilisha mbinu za kuhubiri kadiri ugonjwa wa virusi vya corona unavyoendelea kuenea. Wahubiri nchini Ekuado wamefanikiwa kutumia mbinu mbalimbali za kuhubiri ili kuwafikia watu wakiwa na habari njema.

Katika jiji la Ambato, mhubiri mwenye umri wa miaka saba, pamoja na mama yake, waliwatumia walimu wa shule yake ujumbe mfupi wa simu. Baadhi ya jumbe hizo zilisema hivi: “Habari mwalimu. Ninakuandikia ili kukutumia ujumbe wa faraja kwa sababu sasa kuna hali ngumu. Kwenye Ufunuo 21:4, Biblia inatuambia kutakuwa na wakati ujao mzuri. Ninakutumia kiunganishi hiki kilicho na habari nyingi zaidi.”

Mwalimu mmoja alijibu hivi: “Asante sana, binti yangu mpendwa. Ingawa wewe ni mdogo, maneno yako yana hekima sana.” Mwalimu mwingine alimshukuru sana na kumuuliza ikiwa Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia kinapatikana kielektroni. Mwalimu huyo alieleza kwamba hapo awali alikuwa nacho lakini alimwazima mwanafunzi mwingine. Msichana huyo alimweleza mwalimu kwamba anaweza kukipakua kutoka kwenye jw.org.

Wenzi wa ndoa katika jiji la Quevedo waliangalia orodha ya watu katika simu yao kuona ni nani ambao si Mashahidi na kuwatumia ujumbe huu: “Mimi ni Shahidi wa Yehova. Kwa sababu ya janga hili linaloathiri nchi yetu na ulimwengu mzima, hatuwezi kuwahubiri watu nyumba kwa nyumba, lakini tungependa sana kuzungumza nawe kupitia video kwenye Intaneti.”

Watu wengi walikubali mwaliko huo. Mwanamke mmoja ambaye hakupenda kuwasikiliza Mashahidi walipomtembelea, aliwashukuru wenzi hao wa ndoa na kuwapongeza kwa kazi yao. Mwanamke huyo alieleza kwamba anajihisi akiwa na mkazo kwa sababu ya hali zilizopo. Wenzi hao wa ndoa walimtumia mwanamke huyo gazeti Amkeni!, Na. 1 2020, lenye kichwa “Unaweza Kukabiliana na Mkazo—Jinsi Gani?,” kwenye PDF. Walipozungumza wakati mwingine, mwanamke huyo aliwashukuru kwa gazeti hilo na kuwaambia kwamba alilisoma mara kadhaa.

Dada mmoja kiziwi anayeitwa Johana, anaishi katika jimbo la Santo Domingo de los Tsáchilas, alichora picha. * Kisha alichukua picha hiyo aliyochora na kuipiga picha kwa kutumia simu na kuwatumia viziwi wote waliokuwa kwenye orodha yake ya simu. Hata hivyo, kati ya wale walioipokea, mmoja alikuwa mwanamke aliye na uwezo wa kusikia. Mwanamke huyo alimwandikia ujumbe mara moja akiuliza maswali. Kwa kuwa Johana hakuelewa maswali hayo, dada mmoja painia aliye na uwezo wa kusikia anayeitwa Rhonda alifuatilia upendezi huo.

Mwanamke huyo alimweleza Rhonda kwamba picha ambayo Johana alituma ilimshangaza. Aliuliza ikiwa kuna mistari mingine katika Biblia inayoelezea mambo yanayotendeka sasa duniani. Rhonda alimsomea Luka 21:10, 11 na kumtumia mwanamke huyo kiunganishi cha video yenye kichwa Kwa Nini Mungu Anaruhusu Kuteseka? na Kwa Nini Mungu Aliumba Dunia? Mwanamke huyo alikubali kuendeleza mazungumzo.

Kama mtume Paulo alivyoendelea “kutoa ushahidi kamili kuhusu Ufalme wa Mungu” alipokuwa kifungoni, ndugu zetu wanatumia kila nafasi wanayopata kuhubiri, hata ingawa hawawezi kutoka nyumbani.—Matendo 28:23.

^ Kwa kuwa ni vigumu kwa viziwi wengi kuelewa mambo yaliyoandikwa, wahubiri wengi wanaohubiri katika lugha ya ishara huchora picha ili kuelezea mawazo badala ya kuandika maneno. Mbinu moja wanayotumia ni kubuni aina fulani ya ramani inayotegemea picha zilizopangwa ili kutokeza mawazo.