Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI KUBWA | SAYANSI IMEKAMATA NAFASI YA BIBLIA?

Sayansi na Maisha Yako

Sayansi na Maisha Yako

Kamusi moja inasema kama sayansi ni “kujifunza hali na tabia ya vitu vyenye kuwa katika ulimwengu kwa kuvichunguza, kuvijaribu na kuvipima.” Kazi yote hiyo ni ngumu sana na mara nyingi ni yenye kusumbua. Wanasayansi wanatumia majuma, miezi ao hata miaka mingi ili kujaribu na kuchunguza vitu fulani. Wakati fulani kazi yao hailete matokeo yoyote, lakini mara nyingi inaletea watu faida. Ona mifano fulani.

Shirika moja la Ulaya limetumia plastiki ngumu na vyombo vya hali ya juu vya kusafisha maji, ili kutengeneza chombo fulani cha kusaidia mutu asipate magonjwa yenye kuletwa na maji machafu. Vyombo kama hivyo vimetumiwa wakati wa misiba ya asili kama vile tetemeko la inchi lenye lilitokea Haiti mwaka wa 2010.

Mbali sana katika anga kuna satelite zenye zinasaidia kujua nafasi mutu ao kitu fulani kinapatikana. Mwanzoni, satelite hizo zilitumiwa katika kazi za kijeshi, lakini leo zinasaidia watu kujua njia, kama vile watu wenye kutembeza motokari, avion, mashua, ao hata wawindaji na watu wenye kufanya matembezi. Wanasayansi wenye walitengeneza satelite hizo wamesaidia watu kujua mahali wanataka kuenda.

Unatumikisha telefone, ordinatere ao Internete? Umeona namna maendeleo yenye yamefanyika katika mambo ya matunzo yamekusaidia kuwa na afya ya muzuri ao kupona ugonjwa fulani? Unasafiri katika avion? Ikiwa ni hivyo, unapata faida katika mambo yenye sayansi imefanya ili kusaidia wanadamu. Sayansi imekusaidia katika njia nyingi.

MAMBO YENYE SAYANSI HAIWEZI KUFANYA

Ili wajue mambo mengi zaidi, wanasayansi wa leo wanachunguza sana vitu vyenye kuwa katika ulimwengu. Wanasayansi fulani wanajifunza namna sehemu za ndani ya atome zinafanya kazi, na wengine wanajifunza mambo ya zamani sana, ili kujua namna ulimwengu ulianza. Kadiri wanaendelea kufanya uchunguzi hata katika mambo yenye hatuwezi kuona ao kugusa, wanasayansi fulani wanasema kama, ikiwa Mungu mwenye kutajwa katika Biblia iko kabisa, wangeweza kumupata.

Wanasayansi fulani na watu wenye kujifunza filozofia wanaenda mbali zaidi. Wanaendelesha mawazo yenye Amir Aczel, muandikaji wa mambo ya sayansi alizungumuzia wakati alisema kama watu fulani “wanatumia sayansi ili kuonyesha kama hakuna Mungu.” Kwa mufano, mwanasayansi mumoja mwenye kujulikana sana alisema hivi: “Hakuna jambo lolote lenye kuhakikisha kama kuna Mungu anayetimiza kazi fulani ya maana katika ulimwengu, na hilo linaonyesha wazi kama mungu huyo haiko.” Wengine wanasema kama mambo yenye Mungu mwenye kutajwa katika Biblia anafanya ni “ya uchawi” na hayawezi kueleweka. *

Lakini ni jambo la maana kujiuliza hivi: Wanasayansi wamekwisha kujifunza mambo mengi juu ya ulimwengu na wanaweza kueleza habari za kweli kabisa? Kwa kifupi, jibu ni hapana. Sayansi imeendelea sana, lakini wanasayansi wengi wanatambua kama kuna mambo mengi sana yenye hawajajua na pengine yenye hawataweza kujua. Steven Weinberg, mwanasayansi aliyepata zawadi ya Nobel alisema kama “hakuna siku tutaelewa mambo yote” juu ya vitu vyenye kutuzunguka. Profesa Martin Rees, wa Uingereza aliandika hivi: “Inawezekana kuna mambo wanadamu hawataelewa hata siku moja.” Jambo la kweli ni hili: kuna mambo mengi sana yenye wanasayansi hawajaweza kuelewa, kuanzia chembe ndogo sana mupaka ulimwengu mukubwa sana. Fikiria mifano hii:

  • Wanasayansi wa biolojia hawaelewe kabisa mambo yenye kufanyika katika chembe za viumbe wenye uzima. Hawajue kabisa namna chembe zinatumia nguvu, namna zinatoa proteini, na namna zinajigawanya.

  • Kila wakati, nguvu za uvutano ziko na matokeo fulani juu yetu. Lakini wanasayansi wanashindwa kuelewa nguvu hizo. Hawajue kabisa namna nguvu hizo zinakokota mutu kwenye udongo wakati anaruka juu, ao namna zinawezesha mwezi kuzunguka dunia.

  • Wanasayansi wenye kujifunza juu ya ulimwengu na namna ulitokea, wanakadiria kuwa sehemu kubwa ya ulimwengu (95%) haionekane, na vyombo vyao haviwezi kutoa habari yoyote juu ya sehemu hiyo. Wanagawanya sehemu hiyo mara mbili, ni kusema, vitu visivyoonekana, na nguvu isiyoonekana. Hawajue sehemu hiyo iko namna gani.

Kuna mambo mengine yasiyojulikana yenye wanasayansi wanashindwa kuelewa. Sababu gani ni lazima kujua hivyo? Muandikaji mumoja wa mambo ya sayansi mwenye kujulikana sana anasema hivi: “Mambo yenye hatujue ni mengi sana kuliko yenye tunajua. Ninaona kama, sayansi inapaswa kushangaza mutu lakini haipaswe kumufanya akatae mawazo ya wengine.”

Kwa hiyo, ikiwa unajiuliza kama sayansi itakamata nafasi ya Biblia na kufanya watu wasiamini tena Mungu, ufikirie jambo hili: Wanasayansi wakubwa wenye kuwa na vyombo vya hali ya juu wamefikia kuelewa mambo kidogo tu juu ya ulimwengu. Unaona kama tunapaswa kukataa mara moja kuamini mambo yenye sayansi haiwezi kutuambia? Kitabu Encyclopedia Britannica kinatoa habari ndefu yenye kuzungumuzia historia na maendeleo ya elimu ya vitu vyenye kuwa katika anga. Kinasema hivi kwenye mwisho wa habari hiyo: “Kisha miaka karibu 4000 ya kujifunza vitu vyenye kuwa katika anga, tunaendelea kuona kama ulimwengu haueleweke; ni kama vile tu Wababiloni walikuwa wanauona zamani.”

Mashahidi wa Yehova wanaheshimia haki ya kila mutu ya kuamua juu ya jambo hilo. Tunajikaza kufuata kanuni hii ya Biblia: “Usawaziko wenu na ujulikane kwa watu wote.” (Wafilipi 4:5) Tunakualika uchunguze namna Biblia na sayansi vinapatana na kusaidiana, lakini tunaheshimia haki yako ya kuamua.

^ fu. 9 Watu fulani wanakataa Biblia kwa sababu ya mafundisho ya leo na ya zamani ya dini. Kwa mufano, dini zinafundisha kama dunia iko katikati ya ulimwengu ao kama Mungu aliumba ulimwengu kwa siku sita za saa 24.— Soma kisanduku chenye kichwa “Sayansi Inaunga Mukono Habari za Biblia.”