Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

‘Kutoka Katika Milima Utachimba Shaba’

‘Kutoka Katika Milima Utachimba Shaba’

Kikundi cha wachimbuaji wa vitu vya zamani kilichimba ndani ya mabonde na mapango katika jangwa la Yudea. Washiriki wa kikundi hicho walivumbua pango ndefu sana lenye miteremuko ya gafula. Je, wangepata vitu vya maana sana, labda vyombo vya zamani ao vitabu vya kukunjwa kama vile vya Bahari ya Chumvi? Jambo ambalo liliwashangaza ni kwamba walivumbua hazina ya maana sana, ambayo iliitwa baadaye Nahal Mishmar.

UKIWA wenye kufichwa katika mupasuko wa mwamba na kukunjwa katika mukeka wa matete, mukusanyo huo wa vitu, uliopatikana katika Mwezi wa 3, 1961, ulikuwa na vitu zaidi ya 400, vingi kati ya vitu hivyo vilikuwa vimetengenezwa na shaba. Kati ya vitu hivyo kulikuwa taji mbalimbali, fimbo za kifalme, vyombo mbalimbali, magongo ao fimbo nene za chuma, na silaha zingine. Vitu hivyo vilivyovumbuliwa vinapendeza wasomaji wa Biblia kwa kufikiria mambo yanayosemwa katika andiko la Mwanzo 4:22 juu ya Tubal-kaini aliyekuwa ‘mufuaji wa kila namna ya vifaa vya shaba na chuma.’

Kuna maulizo mengi juu ya mahali ambapo hazina hiyo ya maana sana ilitoka na juu ya historia yake. Hata hivyo, uvumbuzi wa hazina hiyo unaonyesha kwamba kuchimba shaba, kuiyeyusha, na kuipatia umbo ni mambo ambayo yalijulikana tangu zamani sana katika inchi zinazozungumuziwa katika Biblia.

MAENEO YALIYOKUWA NA SHABA KATIKA INCHI YA AHADI

Waisraeli walipokaribia kuingia katika Inchi ya Ahadi, Musa aliwaambia hivi: “Kutoka katika milima [ya inchi hiyo] utachimba shaba.” (Kumbukumbu la Torati 8:7-9) Wachimbuaji wa vitu vya zamani wamevumbua katika Israeli na Yordani maeneo mengi ya zamani ambamo shaba ilichimbwa na kuyeyushwa, maeneo kama vile Feinan, Timna, na Khirbat en-Nahas. Maeneo hayo yanaonyesha nini?

Eneo la Feinan na la Timna lina mashimo mafupi ambamo wachimbuaji walichimba shaba kwa muda wa miaka 2000 hivi. Hata leo, mutu mwenye kutembelea huko anaweza kuona vipande vya shaba vyenye kuchanganyika na mawe, vilivyo na madoa-madoa, na ambavyo vina rangi ya kijani kibichi vikiwa vyenye kusambaa huku na huku. Wachimbuaji wa zamani wa shaba walichimba mwamba kwa bidii kwa kutumia vyombo vya kuvunja mawe ili wafikie kupata shaba iliyokuwa chini ya mwamba huo. Walipomaliza kuzoa shaba hiyo, walichimba tena zaidi kwa kutumia vyombo vya chuma, walipanua mapango na kuchimba zaidi mashimo marefu na kufanya mifereji chini ya udongo. Katika kitabu cha Biblia cha Ayubu, tunapata maelezo juu ya kazi hiyo ya kutafuta mawe ya bei chini ya udongo. (Ayubu 28:2-11) Hiyo ilikuwa kazi ngumu ambayo iliomba kutumia nguvu nyingi za mwili; kwa kweli, kuanzia mwaka wa 201 mupaka mwaka wa 500, wakubwa wa serikali ya Roma walihukumu wakosaji wabaya zaidi na wafungwa wengine kwa kuwatuma watumike katika mashimo ya shaba katika eneo la Feinan.

Marundo makubwa ya takataka za mawe ya bei yanapatikana katika eneo la Khirbat en-Nahas (jina linalomaanisha “Takataka za Shaba”), hilo linaonyesha kwamba kazi ya kuyeyusha shaba ilifanywa sana katika eneo hilo. Watu wenye elimu wanaamini kwamba udongo uliokuwa na mawe ya bei uliletwa hapo kutoka mashimo yaliyokuwa katika maeneo ya karibu, kama vile Feinan na Timna. Ili kutenganisha shaba na udongo, vyombo vya kupulizia vilitumiwa kwa muda wa saa nane mupaka saa kumi ili kuongeza joto la makaa ya moto kwa kiwango cha digrii 1200 za selsiasi. Kwa kawaida, iliomba kilo 5 ya udongo wenye kuchanganyika na shaba ili kupata kilo 1 ya shaba nyekundu, ambayo ingeweza kutengeneza vyombo mbalimbali.

NAMNA SHABA ILIVYOTUMIWA KATIKA ISRAELI LA ZAMANI

Kwenye Mulima Sinai, Yehova Mungu aliagiza hasa kwamba chuma hicho chenye kungaa kilichochimbwa katika eneo hilo kitumiwe katika ujenzi wa hema la kukutania, na baadaye hekalu la Yerusalemu lilijengwa kwa kufuata mufano wa hema la kukutania. (Kutoka sura ya 27) Inawezekana Waisraeli walijua kufanya kazi ya vyuma mbele waende Misri, ao labda walijifunza kazi hiyo huko Misri. Walipokuwa katika safari yao ya kutoka Misri, waliweza kutengeneza ndama ya kuyeyushwa. Waliweza pia kutengeneza vyombo vingi vya shaba ambavyo vilipaswa kutumiwa katika hema la kukutania, vyombo kama vile beseni kubwa, vyungu, pano zilizotumiwa ili kukaanga, vipao, na kanya.​—Kutoka 32:4.

Baadaye, walipokuwa katika safari yao jangwani, labda karibu na Punon (inawezekana kwa sasa inaitwa Feinan), eneo lililo na shaba nyingi, watu walilalamika juu ya mana na maji. Ili kuwaazibu, Yehova alituma nyoka wenye sumu na watu wengi walikufa. Kisha Waisraeli kutubu, Musa alimuomba Yehova kwa ajili yao, na Yehova akamuagiza afanye nyoka wa shaba na kumusimamisha juu ya muti murefu. Habari hiyo inasema hivi: ‘Ikawa kwamba nyoka alipomuuma mutu naye akamutazama yule nyoka wa shaba, ndipo alipoendelea kuwa hai.’​—Hesabu 21:4-10; 33:43.

SHABA YA MUFALME SULEMANI

Sehemu nyingi za hekalu la Yerusalemu zilijengwa kwa kutumia shaba

Mufalme Sulemani alitumia kiasi kikubwa cha shaba ili kupamba hekalu la Yerusalemu. Shaba nyingi kati ya hiyo ilikusanywa na baba yake, Daudi, kutoka maeneo ya Siria ambayo alikuwa ameshinda. (1 Mambo ya Nyakati 18:6-8) “Bahari ya kuyeyushwa” yenye shaba, ni kusema, beseni kubwa iliyotumiwa na makuhani ili kunawa, ilikuwa na uwezo wa lita 66 000 za maji na uzito wa toni 30. (1 Wafalme 7:23-26, 44-46) Kisha kulikuwa na nguzo mbili kubwa za shaba ambazo zilishimikwa kwenye mwingilio wa hekalu. Nguzo hizo zilikuwa na urefu wa meta 8 na zilifunikwa na makombe yenye urefu wa meta 2.2. Zilikuwa na shimo ndani, unene wa pande za nguzo hizo ulikuwa wa sentimeta 7 na nusu, na zilikuwa na diametri ya meta 1.7. (1 Wafalme 7:15, 16; 2 Mambo ya Nyakati 4:17) Inashangaza kufikiri juu ya kiasi cha shaba kilichotumiwa ili kutengeneza vitu hivyo.

Shaba ilitumiwa sana na watu wa nyakati za Biblia katika maisha yao ya kila siku. Kwa mufano, tunasoma juu ya silaha, pingu, vyombo vya muziki, na milango iliyotengenezwa na shaba. (1 Samweli 17:5, 6; 2 Wafalme 25:7; 1 Mambo ya Nyakati 15:19; Zaburi 107:16) Yesu alisema juu ya feza ya “shaba” kwa ajili ya mikoba, na mutume Paulo alitaja “Aleksanda yule fundi wa shaba.”​—Mathayo 10:9; 2 Timotheo 4:14.

Wachimbuaji wa vitu vya zamani na wanahistoria bado wanatafuta majibu ya maulizo mengi juu ya utajiri wa shaba wa nyakati za Biblia, na pia juu ya hazina ya maana sana inayoitwa Nahal Mishmar. Hata hivyo, kama inavyoonyeshwa na masimulizi ya Biblia, jambo la hakika ni kwamba inchi ambayo Waisraeli waliriti ilikuwa kwa kweli ‘inchi nzuri, . . . ambayo kutoka katika milima yake wangechimba shaba.’​—Kumbukumbu la Torati 8:7-9.