Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

BIBLIA INABADILISHA MAISHA YA WATU

Biblia Inabadilisha Maisha ya Watu

Biblia Inabadilisha Maisha ya Watu
  • ALIZALIWA MWAKA WA 1960

  • ALIZALIWA KATIKA INCHI YA FINLANDE

  • ALIKUWA MUCHEZAJI WA MUZIKI WENYE MUDUNDO MUKALI

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Nilikomalia huko Turku, muji ambamo mashua zinaegesha, watu hawakuwa matajiri katika muji huo. Baba yangu alikuwa muchezaji mukubwa wa ngumi, na mimi na ndugu yangu mudogo sana tulikuwa wenye bidii katika muchezo huo. Kwenye masomo, nilipigana mara nyingi; sikujizuia kutumia ngumi zangu. Nilipokuwa kijana, nilijiunga na kikundi kimoja cha watu kilichojulikana kuwa na sifa mbaya, ambacho kiliniongoza mara nyingi katika mapigano. Pia nilivumbua muziki wenye mudundo mukali na nikaanza kutamani kuwa mwanamuziki anayejulikana sana wa muziki wenye mudundo mukali.

Nilinunua ngoma fulani, nikaanzisha kikundi cha wanamuziki, na bila kukawia nikakuwa kiongozi wa kikundi hicho. Nilipokuwa kwenye jukwaa, nilijiendesha kama mwendawazimu. Kwa sababu kikundi chetu kilikuwa chenye ugomvi na tulijiendesha kama wendawazimu katika namna yetu ya kuvaa na katika mwenendo wetu, kikundi chetu kiliendelea kujulikana. Tulianza kucheza mbele ya watu wengi na tukafanya rekodi chache za muziki, na rekodi ya mwisho ilisifiwa sana na watu. Mwishoni mwa miaka ya 1980, tulisafiri mupaka États-Unis ili kufanya kikundi chetu kijulikane sana. Mara chache, tulicheza muziki huko New York na katika Los Angeles, na tukaonana na kikundi cha watu wenye elimu ya juu katika mambo ya muziki mbele ya kurudia Finlande.

Ijapokuwa nilifurahia kuwa katika kikundi hicho, nilitamani sana kuwa na maisha yenye maana zaidi. Sikupendezwa na roho ya ushindani na ugomvi iliyokuwa katika mambo ya muziki na nilivunjika moyo kwa sababu ya namna yangu ya kuishi iliyokuwa ya kipumbavu. Nilijisikia kuwa mutu mubaya, na niliogopa kuunguzwa katika moto wa mateso. Nilijaribu kutafuta majibu fulani katika vitabu vya kidini vya namna zote na nilisali pia kwa bidii ili Mungu anisaidie, hata ikiwa nilijisikia kuwa siwezi kumupendeza hata kidogo.

BIBLIA ILIBADILISHA MAISHA YANGU:

Ili kutosheleza mahitaji yangu, nilitumika kwenye biro ya posta ya eneo letu. Siku moja, nilivumbua kwamba mufanyakazi mwenzangu mumoja alikuwa Shahidi wa Yehova. Nilimuuliza maulizo mengi sana. Nilipendezwa sana na majibu yake yenye kueleweka na yenye kutegemea Maandiko, na kwa hiyo, nikakubali kujifunza Biblia pamoja naye. Kisha kujifunza kwa majuma fulani, kikundi chetu cha muziki kilipata ombi lenye kuvutia la kufanya rekodi ya muziki ili kutoa albumu huko États-Unis. Niliona hiyo kuwa bahati ya kupata maisha mazuri.

Nilimuambia Shahidi aliyekuwa akinifundisha Biblia kwamba nilipenda kutoa albumu ingine moja tu na kisha kufanya hivyo, ningeanza kutumikisha kwa moyo wote kanuni za Biblia katika maisha yangu. Shahidi huyo hakuonyesha maoni yake; aliniomba tu nisome maneno ya Yesu katika andiko la Mathayo 6:24. Andiko hilo linasema hivi: “Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili.” Nilishituka nilipoelewa maana ya maneno hayo ya Yesu. Lakini kisha siku chache, mwalimu wangu wa Biblia ndiye alishituka sasa! Nilimuambia kwamba niliachana na kikundi hicho kwa sababu nilipenda kumufuata Yesu!

Niliiona Biblia kama kioo kilichofunua makosa yangu. (Yakobo 1:22-25) Nilitambua kwamba nilikuwa na tabia mbaya sana: Nilikuwa mwenye majivuno, nilitamani sana mambo makubwa. Nilizoea kutumia maneno machafu, kugombana, kuvuta tumbaku, na kunywa pombe sana. Nilipoona kwamba namna yangu ya kuishi haikupatana na kanuni za Biblia, nilivunjika moyo sana. Hata hivyo, nilikuwa tayari kufanya mabadiliko yaliyohitajiwa.​—Waefeso 4:22-24.

“Baba yetu wa mbinguni ni mwenye rehema, na anataka kuponyesha vidonda vya wale wanaotubu makosa yao”

Nilisikitika sana kwa sababu ya mwenendo wangu wa zamani, zaidi sana wakati nilianza kujifunza Biblia. Lakini, Shahidi aliyenifundisha Biblia alinisaidia sana. Alinionyesha mambo ambayo Biblia inasema katika andiko la Isaya 1:18. Andiko hilo linasema hivi: ‘Hata zambi zenu zikiwa nyekundu, zitafanywa kuwa nyeupe kama seluji.’ Andiko hilo na maandiko mengine yalinisadikisha kwamba Baba yetu wa mbinguni ni mwenye rehema na anataka kuponyesha vidonda vya wale wanaotubu makosa yao.

Nilipoanza kumuona Yehova kuwa mutu anayeishi kwelikweli na kumupenda, nilitaka kujitoa kwake. (Zaburi 40:8) Nilibatizwa katika mwaka wa 1992 kwenye mukusanyiko wa kimataifa wa Mashahidi wa Yehova uliofanywa huko Saint-Petersburg, Russie.

FAIDA AMBAYO NIMEPATA:

Nimejifanyia marafiki wengi wazuri kati ya waabudu wa Yehova. Mara kwa mara, tunakutana pamoja ili kucheza muziki unaofaa na tunafurahia zawadi hiyo iliyotoka kwa Mungu. (Yakobo 1:17) Baraka ya pekee ambayo nimepata ni kumuoa Kristina, bibi yangu mupendwa. Ninachangia mambo mengi pamoja naye, kama vile furaha na matatizo ya maisha, na pia namna ninavyojisikia moyoni.

Kama singekuwa Shahidi wa Yehova, labda singekuwa muzima leo. Zamani, nilikuwa nikijikuta katika matatizo na shida mara kwa mara. Sasa maisha yangu ni yenye maana kwelikweli, na ninajisikia kuwa mambo yote yanaendeka vizuri.