Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Jinsi Unavyoweza Kuishi Kulingana na Mapato Yako

Jinsi Unavyoweza Kuishi Kulingana na Mapato Yako

Jinsi Unavyoweza Kuishi Kulingana na Mapato Yako

HEBU wazia una ndoo iliyotoboka, na unapaswa kuijaza maji. Ungefanya hivyo jinsi gani? Ungefaulu tu ikiwa ungehakikisha kwamba kiwango cha maji yanayomwagika kutoka kwenye ndoo ni sawa na kile unachoweka katika ndoo hiyo.

Kimsingi, hiyo ndiyo maana ya kuishi kulingana na mapato yako. Mapato yako yanaweza kulinganishwa na maji unayoweka kwenye ndoo. Nayo matumizi yako ni kama maji yanayomwagika kupitia lile tundu. Tatizo ni kuhakikisha kwamba matumizi yako yanalingana na mapato yako.

Ingawa huenda maelezo hayo yakasikika kuwa rahisi, ni vigumu watu kuishi kulingana na mapato yao na kunufaika kutokana na jambo hilo. Watu wangeepuka matatizo mengi ya kifedha kama wangefuata kanuni hiyo ya msingi. Tunaweza kufaulu jinsi gani? Tunaweza kupata wapi miongozo itakayotusaidia kufaulu? Biblia ina habari nyingi zinazoweza kutusaidia. Acheni tuchunguze mambo machache ambayo inasema.

Kanuni za Biblia Zinazoweza Kukusaidia

Biblia ina kanuni nyingi zinazoweza kukusaidia utumie pesa zako kwa njia inayofaa. Tutachunguza kanuni chache tu. Tafadhali soma habari inayofuata kuhusu kanuni hizo na utaona kwamba zinaweza kukusaidia kuishi kulingana na mapatano yako.

Uwe na mpango, au bajeti. Ili uweze kutumia pesa zako vizuri unahitaji kujua ni pesa ngapi unazopata na jinsi unavyozitumia. Biblia inasema: “Mipango ya mwenye bidii bila shaka huleta faida, lakini kila mtu anayetenda haraka-haraka bila shaka huuelekea uhitaji.” (Methali 21:5) Watu wengine wanatumia bahasha kadhaa wanapopanga jinsi watakavyotumia pesa zao. Katika kila bahasha wanaweka pesa kwa ajili ya matumizi mbalimbali, kama vile pesa za “Chakula,” “Kodi ya Nyumba,” au “Mavazi.” Iwe unatumia mbinu hii rahisi au nyingineyo, jambo muhimu ni kwamba utajua jinsi pesa zako zinavyotumika, na wakati wote utatanguliza mahitaji ya lazima badala ya anasa.

Epuka wivu. Watu wengi wanaoishi katika mataifa maskini wanatamani vitu ambavyo watu wa mataifa yaliyoendelea kiviwanda wanavyo. Wengine wengi wanashawishiwa kupata vitu ambavyo jirani zao wanajivunia kuwa navyo. Huo unaweza kuwa mtego. Huenda hata jirani hao hawana uwezo wa kununua vitu hivyo kwa pesa zao wenyewe. Kwa nini ufuate mfano wa mtu asiye na busara na mwishowe uingie katika matatizo ya kifedha? Biblia inaonya: “Mtu mwenye jicho la wivu hukimbilia vitu vyenye thamani, lakini hajui kwamba atakuwa na uhitaji.”—Methali 28:22.

Ishi maisha rahisi. Yesu aliwashauri wafuasi wake wawe na jicho “rahisi.” (Mathayo 6:22) Kwa nini uchague chakula cha bei ya juu sana huku ukijua kwamba chakula unachoweza kupata kulingana na mapato yako ni ugali na mboga za majani? Kulingana na ripoti moja ya Benki ya Maendeleo ya Asia, karibu asilimia 33 ya watu wanaoishi Ufilipino na zaidi ya nusu ya watu wanaoishi India ni maskini sana hivi kwamba wanatumia dola 1.35 za Marekani kwa siku. Mapato yanapokuwa kidogo hivyo, ni jambo la busara kukazia fikira mahitaji ya lazima tu. Lakini hata katika nchi tajiri, kanuni hiyo inaweza kuwalinda watu wasipatwe na matatizo mengi ya kifedha.

Tosheka na vitu unavyohitaji. Himizo hili linapatana na ile kanuni ya kuishi maisha rahisi. Biblia inatoa shauri hili kwenye 1 Timotheo 6:8: “Tukiwa na chakula na kitu cha kujifunika, tutaridhika na vitu hivyo.” Baadhi ya watu wenye furaha zaidi duniani hawana pesa nyingi; hata hivyo, wao wanatosheka na vitu walivyo navyo vinavyotia ndani si vitu vya kimwili tu bali pia upendo kutoka kwa familia zao na marafiki.—Methali 15:17.

Epuka madeni yasiyo ya lazima. Maneno haya ya Biblia ni ya kweli kabisa: “Mtu tajiri ndiye huwatawala maskini, na mkopaji ni mtumishi wa mtu anayemkopesha”! (Methali 22:7) Ingawa kuna wakati ambapo huenda ikawa vigumu kuepuka kukopa pesa, wale wanaokopa isivyo lazima ili tu wanunue kitu fulani wanachotaka, mara nyingi wanajikuta wamelewa na madeni makubwa sana. Jambo hilo linatukia hasa wakati wanapotumia kadi za mkopo. Gazeti Time linasema, “Mtu anapokuwa na kadi ya mkopo, anaweza kuanza kununua vitu kwa msisimko tu bila kufikiri.” Eric anayeishi nchini Ufilipino, anasema: “Ninapotumia kadi ya mkopo, ninanunua vitu vingi zaidi kuliko wakati ninapotumia pesa. Jambo hilo linavuruga bajeti yangu kwa kuwa lazima nilipie bidhaa nilizonunua kwa kutumia kadi ya mkopo.” Bila shaka, tunahitaji kuwa waangalifu sana tunapotumia kadi za mkopo!—2 Wafalme 4:1; Mathayo 18:25.

Weka akiba kabla ya kununua vitu. Ingawa huenda likaonekana kuwa jambo lililopitwa na wakati, kuweka pesa akiba ili kununua kitu fulani ndiyo njia ya busara zaidi inayoweza kutusaidia kuepuka matatizo ya kifedha. Kufanya hivyo kunawaepusha watu wengi na madeni na matatizo yanayotokana na madeni hayo, kama vile kiwango kikubwa cha faida ambacho mkopaji analipa anaponunua bidhaa kwa mkopo, jambo ambalo hatimaye hufanya alipe pesa nyingi zaidi kwa bidhaa alizonunua. Katika Biblia, chungu anatajwa kuwa mwenye “hekima” kwa sababu anaweka akiba ya “chakula chake wakati wa mavuno” ili aweze kukitumia baadaye.—Methali 6:6-8; 30:24, 25.

Kujifunza Kutoka kwa Wengine

Huenda mashauri yote ya Biblia ambayo tumezungumzia yakasikika kuwa mazuri, lakini je, yamewasaidia watu kuishi kulingana na mapato yao? Acheni tuchunguze visa kadhaa kuhusu watu ambao wamefuata mashauri hayo na wakafaulu kutatua matatizo ya kifedha.

Diosdado, baba ya watoto wanne, anasema kwamba kuzorota kwa hali ya uchumi hivi karibuni, kumefanya iwe vigumu zaidi kwake kutosheleza mahitaji ya familia yake. Hata hivyo, anatambua umuhimu wa kuwa na bajeti. Anasema: “Mimi ninapangia pesa zote ninazopata. Nina orodha ya jinsi ninavyotumia pesa zangu.” Danilo anafuata kanuni hiyohiyo. Biashara aliyokuwa akifanya pamoja na mke wake haikufaulu. Hata hivyo, wanaweza kulipia mahitaji yao kwa kupangia pesa zao vizuri. Anasema: “Tunajua ni pesa ngapi tunazopata na tunazotumia kila mwezi. Tukiwa na hayo akilini, tunazungumzia kiasi cha pesa tunachoweza kutumia.”

Ili kufaulu kutumia bajeti waliopanga, wengine wameamua kupunguza kiwango cha matumizi yao. Myrna, mjane aliye na watoto watatu, anasema: “Badala ya kutumia magari ya umma kwenda kwenye mikutano ya Kikristo, sasa mimi na watoto wangu tunatembea tu.” Myrna amejitahidi kuwasaidia watoto wake waone umuhimu wa kuishi maisha rahisi. Anasema: “Nimejaribu kuwawekea mfano mzuri katika kutumia kanuni ya 1 Timotheo 6:8-10, inayoonyesha umuhimu wa mtu kutosheka na vitu alivyo navyo.”

Gerald, aliye na watoto wawili amefanya vivyo hivyo. Anasema: “Wakati wa funzo la Biblia la familia, tunazungumzia mifano ya Wakristo wanaokazia fikira mambo yaliyo muhimu zaidi, yaani, mambo ya kiroho. Matokeo ya kufanya hivyo yanatia moyo kwa sababu watoto wetu hawadai vitu ambavyo si muhimu.”

Janet ni mseja na amejitolea kufundisha Biblia wakati wote nchini Ufilipino. Alipoteza kazi yake hivi karibuni, lakini anaishi kulingana na mapato yake. Anasema: “Ninafanya hivyo kwa kujitia nidhamu na kupanga vizuri matumizi ya pesa na vitu nilivyo navyo. Badala ya kwenda kwenye maduka makubwa-makubwa ambayo huenda yakawa na bidhaa za bei ya juu, mimi ninatafuta maduka yanayouza bidhaa kwa bei nafuu. Kwa nini ninunue vitu kwa bei ya juu na ninaweza kuvipata kwa bei ya chini? Pia ninaepuka kununua vitu bila kufikiri.” Janet anaona hekima inayotokana na kuweka akiba ya pesa. “Ninapopata pesa za ziada, hata kama ni kidogo,” anasema Janet, “ninaziweka akiba ili nizitumie wakati kunapotokea hali isiyotazamiwa.”

Kuhusu kadi za mkopo, Eric, aliyetajwa mwanzoni, anasema: “Nimejitahidi kujizuia nisitumie kadi ya mkopo, isipokuwa kutokee jambo lisilotazamiwa.” Diosdado anakubaliana naye: “Ili kujizuia, kwa kawaida mimi huacha kadi yangu ofisini.”

Unaweza Kuishi Kulingana na Mapato Yako

Ndiyo, wengi wanatambua kwamba ingawa Biblia ni kitabu kinachoweza kutusaidia katika mambo ya kiroho, pia kinatoa miongozo inayoweza kutunufaisha katika mambo ya kimwili pia. (Methali 2:6; Mathayo 6:25-34) Kwa kufuata kanuni za Biblia zilizozungumziwa katika makala hii na kwa kujifunza kutokana na jinsi ambavyo wengine wamefaidika kwa kufuata kanuni hizo, wewe pia unaweza kuishi kulingana na mapato yako. Kwa kufanya hivyo, unaweza kuepuka matatizo na mahangaiko yanayowapata mamilioni ya watu leo.

[Blabu katika ukurasa wa 10]

‘Tunazungumzia kinaganaga kiasi cha pesa tunachoweza kutumia’

[Blabu katika ukurasa wa 11]

‘Badala ya kutumia gari kwenda kwenye mikutano ya Kikristo, sisi tunatembea tu’

[Blabu katika ukurasa wa 11]

“Ninaepuka kununua vitu bila kufikiri”