Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

MAMBO YENYE HISTORIA INATUFUNDISHA

Desiderius Erasmus

Desiderius Erasmus

MWANZONI, watu wa wakati wa Desiderius Erasmus (mwenye aliishi kati ya mwaka wa 1469 na 1536 hivi) walimusifu na kumuona kuwa musomi mukubwa zaidi katika Ulaya, kisha walimuona kuwa mutu mwenye woga ao muasi-imani. Alikuwa amejiingiza katika mazungumuzo mengi ya dini, na bila woga alionyesha wazi makosa ya Kanisa Katoliki na ya watu wenye walitaka kufanya mabadiliko katika kanisa hilo. Leo, inajulikana kama yeye ndiye alisaidia sana kuleta mabadiliko katika mambo ya dini katika Ulaya. Alifanya hivyo namna gani?

UCHUNGUZI WAKE NA MAMBO YENYE ALIAMINI

Kwa sababu Erasmus alijua sana Kigiriki na Kilatini, hilo lilimuwezesha kulinganisha tafsiri za Kilatini za Biblia, kama vile Vulgate ya Kilatini, na maandishi ya zamani ya Kigiriki ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, yenye kuitwa pia Agano Jipya. Alifikia kuwa hakika kama mafundisho ya Biblia yalikuwa ya lazima. Ndiyo sababu alisema kama Maandiko Matakatifu yalipaswa kutafsiriwa katika luga zingine za watu wa kawaida wa wakati wake.

Erasmus alikazia mabadiliko yafanywe katika Kanisa Katoliki, kwa sababu aliamini kama Ukristo ni namna ya kuishi, haiko tu kufuata desturi zenye hazina maana. Kwa hiyo, wakati warekebishaji walianza kupinga Kanisa la Roma na kuomba mabadiliko yafanywe katika kanisa hilo, Wakatoliki walikuwa na mashaka juu yake.

Bila woga Erasmus alionyesha wazi makosa ya Kanisa Katoliki na ya watu wenye walitaka kufanya mabadiliko katika kanisa hilo

Katika maandishi yake, alionyesha kwa zihaka mambo mabaya yenye viongozi wa dini walikuwa wanafanya, namna yao ya kuishi yenye majivuno, na mapapa wenye tamaa ambao waliunga mukono vita. Alikuwa tofauti na viongozi wa dini wakorofi wenye walitumia desturi za kanisa kama vile kutubu zambi, kuabudu watakatifu, kufunga, na safari mbalimbali kwa ajili ya ibada ili kupata faida kutoka kwa waamini. Alipinga pia desturi za kanisa kama vile, mutu kulipa feza ili asamehewe na kulazimisha watu fulani katika kanisa wabakie bila kufunga ndoa.

MAANDISHI YA KIGIRIKI YA AGANO JIPYA

Katika mwaka wa 1516, Erasmus alichapisha tafsiri yake ya kwanza ya Agano Jipya ya Kigiriki; hiyo ilikuwa tafsiri ya kwanza ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo kuchapishwa. Tafsiri hiyo ya Erasmus ilikuwa na maelezo. Ilikuwa pia na tafsiri ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Kilatini, yenye ilikuwa tofauti na Vulgate. Kwa wakati fulani, aliendelea kufanya mabadiliko katika tafsiri yake, mupaka alifikia kutoa tafsiri yenye ilikuwa tofauti zaidi na maandishi ya Kilatini ya Vulgate.

Agano Jipya ya Kigiriki ya Erasmus

Kati ya maandishi yenye yalikuwa tofauti kulikuwa andiko la 1 Yohana 5:7. Ili kuunga mukono fundisho la Utatu lenye haliko la Biblia, maneno fulani yenye kuitwa comma Johanneum yaliongezwa katika Vulgate. Maneno hayo yanasema hivi: “Huko mbinguni, Baba, Neno, na Roho Mtakatifu: nao watatu hao ni mmoja.” Lakini, Erasmus hakutia maneno hayo katika tafsiri zake mbili za kwanza za Agano Jipya kwa sababu maandishi yote ya Kigiriki yenye alichunguza hayakuwa na maneno hayo. Hata hivyo, kanisa lilimukaza aongeze maneno hayo katika tafsiri yake ya tatu.

Tafsiri za Agano Jipya za Kigiriki zenye Erasmus alitafsiri muzuri zaidi zilitoa musingi wa kutafsiri kwa njia yenye kufaa katika luga za Ulaya. Watafsiri wenye kufuata walizitumia ili kutafsiri Maandiko ya Kigiriki katika luga mbalimbali: Martin Luther katika Kijerumani, William Tyndale katika Kiingereza, Antonio Brucioli katika Kiitaliano, na Francisco de Enzinas katika Kihispania.

Erasmus aliishi katika kipindi chenye muvurugo mwingi wa dini, na Warekebishaji Waprotestanti waliona tafsiri yake ya Agano Jipya ya Kigiriki kuwa musaada mukubwa. Mbele Marekebisho ya Dini yaanze kabisa, watu fulani waliwaza kama Erasmus alikuwa murekebishaji. Lakini, alikataa kuunga mukono sehemu yoyote katika mazungumuzo mengi ya teolojia yenye yalifuata. Jambo la kufurahisha ni kwamba, zaidi ya miaka 100 yenye imepita, muandikaji David Schaff aliandika kama Erasmus “alikufa akiwa mwenye kujitenga, bila kuwa na dini yoyote. Wakatoliki hawangeweza kusema kama alikuwa wao; Waprotestanti hawangeweza kusema hivyo pia.”