Hamia kwenye habari

Kuhubiri Kwenye Kingo za Mto Xingu

Kuhubiri Kwenye Kingo za Mto Xingu

Mapema Julai 2013, kikundi cha Mashahidi wa Yehova 28 nchini Brazili, kilisafiri kutoka São Félix do Xingu kuelekea eneo la watu wa makabila ya wa Cayapo na Yuruna. Walisafiri kwa mashua yenye urefu wa mita 15 kuelekea chanzo cha Mto Xingu, unaotiririka kilomita 2,092 upande wa kaskazini kuelekea Mto Amazon.

Mashahidi hao walifunga safari hiyo ili wawahubirie watu wanaoishi kwenye vijiji vilivyo kwenye kingo za Mto Xingu kuhusu Ufalme wa Mungu. Siku ya tatu, walifika kwenye kijiji cha Kokraimoro. Watu wa kijiji hicho waliwakaribisha kwa uchangamfu na walikuwa wakarimu. Mwanamke mmoja aliwapungia mkono kwa bidii. Mtu aliyekuwa akiwatembeza Mashahidi hao aliwaeleza hivi: “Ishara zake zinamaanisha: ‘Njooni nyinyi nyote. Tunataka kumjua kila mmoja wenu!’”

Mashahidi waliongea na watu wote​—wengine waliwahubiria kwa Kireno na wengine kwa njia ya ishara. Michoro yenye rangi maridadi iliyo kwenye machapisho ya Biblia ambayo walibeba iliwasaidia sana, na wanakijiji wengi walikubali kuchukua machapisho, hasa broshua yenye kichwa Msikilize Mungu.

Gerson, painia wa pekee anayetumikia São Félix do Xingu, anakumbuka jinsi mwanakijiji fulani alivyopokea kitabu kinachoitwa Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia: “Alikitazama kisha akakikumbatia kwa nguvu mkononi mwake; hakutaka kukiweka chini hata kidogo.”

Mashahidi wa Yehova waliwaachia wanakijiji wanaoishi kwenye kingo za mto huo vitabu 500 hivi, magazeti, na broshua. Katika kijiji cha Kawatire, wanakijiji walisikiliza kwa makini sana Mashahidi hao walipokuwa wakizungumzia ahadi ya Biblia kwamba kutakuwa na paradiso duniani. “Katika paradiso watu wataishi kama sisi tunavyoishi,” akasema Tonjaikwa, mwenyeji mwenye ukarimu wa kabila la Cayapo.

Watu wengi katika mji wa São Félix do Xingu walijua kuhusu safari hiyo. Simone, mmoja wa wale waliokuwa kwenye msafara huo, alisema kwamba baadhi ya watu wa mji wa kwao walitia shaka ikiwa yeye na waandamani wake wangeruhusiwa kuhubiri kwenye vijiji hivyo. Hata hivyo, hakukuwa na tatizo. “Tulikaribishwa,” Simone anasema, “na tuliwahubiria wote.”