Hamia kwenye habari

Je, Mashahidi wa Yehova Wameibadili Biblia Ili Ifaane na Mambo Wanayoamini?

Je, Mashahidi wa Yehova Wameibadili Biblia Ili Ifaane na Mambo Wanayoamini?

 La, hatujafanya hivyo. Kinyume na hilo, mara tu tunapogundua kwamba jambo fulani tunaloamini halipatani na yale ambayo Biblia inasema, tunaacha kuamini jambo hilo.

 Tulichunguza Neno la Mungu kwa makini miaka mingi hata kabla ya kuchapisha Biblia TakatifuTafsiri ya Ulimwengu Mpya katika mwaka wa 1950. Tulitumia tafsiri za Biblia zilizokuwepo ili kutegemeza mafundisho yetu. Hebu tufikirie baadhi ya mambo ambayo Mashahidi wa Yehova wameamini kwa miaka mingi, na ujaribu kuona ikiwa mambo hayo yanapatana kabisa na mambo ambayo Biblia inafundisha hasa.

  1.   Jambo tunaloamini: Mungu si utatu. Gazeti la Zion’s Watch Tower la Julai 1882 lilisema hivi: “Wasomaji wetu wanajua kwamba, ingawa tunamwamini Yehova na Yesu, na pia Roho takatifu, tunakataa kabisa fundisho la kuwa kuna Miungu watatu ndani ya mtu mmoja, au kama wanavyosema wengine, Mungu mmoja ndani ya watu watatu kwa sababu hilo si fundisho la Biblia.

      Biblia inasema nini? “Jehova Mwenyiezi Mngu wetu, Jehova ni mmoja.” (Kumbukumbu la Torati 6:4, The Old Testament in Swahili, [Mombasa]) “Kwetu sisi Mungu ni mmoja tu, aliye Baba, ambaye vitu vyote vimetoka kwake, nasi tunaishi kwake; yuko na Bwana mmoja Yesu Kristo, ambaye kwake vitu vyote vimekuwapo, na sisi kwa yeye huyo.” (1 Wakorintho 8:6, Union Version) Yesu mwenyewe alisema: “Baba ni mkuu kuliko mimi.”​—Yohana 14:28, Douay-Rheims Version.

  2.   Jambo tunaloamini: Wanadamu hawateseki milele katika moto wa mateso. Likinukuu andiko la Waroma 6:​23 kutoka kwenye tafsiri ya King James Version, gazeti la Zion’s Watch Tower la Juni 1882 lilikuwa na kichwa “Mshahara wa Dhambi Ni Kifo,” na lilisema: “Maneno hayo ni mepesi kuelewa na yako wazi kabisa. Inashangaza kwamba wengi wanaokiri kuipokea Biblia kama Neno la Mungu huendelea kupingana na maneno hayo ya kweli huku wakisisitiza kwamba Biblia inafundisha kuwa mshahara wa dhambi ni uzima wa milele katika mateso.”

      Biblia inasema nini? “Nafsi itendayo dhambi, itakufa.” (Ezekieli 18:​4, 20, King James Version) Adhabu ya mwisho ambayo wale wanaompinga Mungu watapata si kuteswa milele, bali “maangamizi ya milele.”​—2 Wathesalonike 1:9, Bible in Swahili.

  3.   Jambo tunaloamini: Ufalme wa Mungu ni serikali halisi, si hali fulani iliyo moyoni mwa mtu. Gazeti la Zion’s Watch Tower la Desemba 1881 lilisema: “Bila shaka kusimamishwa kwa ufalme huu, kutahusisha kupinduliwa kwa falme zote za dunia.”

      Biblia inasema nini? “Katika siku za wafalme hao Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele: bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”​—Danieli 2:​44, Union Version.

Je, Mashahidi wa Yehova wanategemea Biblia ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ili kutetea mambo wanayoamini?

 Hapana, kwa sababu tunapowahubiria watu sisi hutumia tafsiri nyinginezo za Biblia. Isitoshe, ingawa sisi huwapa watu Biblia ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya bila malipo ikiwa sehemu ya kazi yetu ya elimu ya bure ya Biblia, tunafurahia kujifunza na wale ambao wangependa kutumia tafsiri nyinginezo za Biblia pia.