Hamia kwenye habari

Mmoja Aanza Kujifunza Biblia Hatimaye Wengi Wanajiunga Naye

Mmoja Aanza Kujifunza Biblia Hatimaye Wengi Wanajiunga Naye

Marta, ambaye ni Shahidi wa Yehova nchini Guatemala, anajifunza lugha ya Kekchi ili ashiriki ujumbe wa Biblia na watu wanaozungumza lugha hiyo. Siku moja alimwona mwanamume fulani akitoka hospitalini. Mwonekano wake ulimfanya Marta alifikiri kwamba huenda anatoka kwenye kijiji cha Kekchi kilicho katika milima ambayo Mashahidi wa Yehova hawajaweza kuhubiri kwa ukawaida. Alimkaribia na kuanza kuzungumza naye maneno machache ya Kikekchi aliyofahamu.

Marta alimkaribisha mwanamume huyo ajifunze Biblia. Alikubali lakini akamwambia kwamba hakuwa na pesa za kulipia funzo hilo. Marta alimweleza kwamba Mashahidi wa Yehova hujifunza Biblia na watu bila malipo. Pia, alimwambia angeweza kujifunza kupitia simu, na familia yote iliruhusiwa kujiunga naye. Mwanamume huyo alikubali. Kwa sababu alijua kuzungumza na kusoma Kihispania, Marta alimpa Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Kihispania. Pia alimpa nakala ya Kikekchi ya kitabu cha kujifunzia Biblia kinachoitwa Biblia Inafundisha Nini Hasa? Juma lililofuata, mwanamume huyo, mke wake, na watoto wao wawili walianza kujifunza Biblia na Marta kupitia simu. Walijifunza mara mbili kwa juma. Marta anasema: “Kwa sababu sikujua Kikekchi vizuri, tulizungumza katika Kihispania, kisha mwanamume huyo akamtafsiria mke wake mambo tuliyosema. Lakini watoto walielewa Kihispania.”

Mwanamume huyo alikuwa kasisi katika kanisa lake. Alianza kuwafundisha waumini wake mambo aliyokuwa akijifunza katika funzo lake la Biblia. Waumini walifurahia mambo hayo na wakamuuliza alikuwa akipata wapi mafundisho hayo mapya. Alipowaambia kuhusu funzo lake la Biblia, walianza kujiunga mmoja baada ya mwingine. Baada ya muda mfupi, watu 15 hivi walikuwa wakijiungaa kila juma kujifunza na Marta kupitia simu. Baada ya muda, waliweka mikrofoni karibu na simu ili wote waweze kusikia.

Marta alipowaambia wazee wa kutaniko lake kuhusu funzo hilo la Biblia, mmoja wao alitembelea kijiji hicho ambapo wanafunzi hao walikuwepo. Aliwakaribisha kuhudhuria hotuba ya watu wote ambayo mwangalizi wa mzunguko a angetoa kutoka katika kijiji kilichokuwa mbali. Wangehitaji kusafiri saa moja kwa gari kisha kutembea kwa saa nyingine mbili kwa miguu. Wanafunzi hao walikubali na 17 kati yao walihudhuria.

Majuma kadhaa baadaye, mwangalizi wa mzunguko na Mashahidi wengine walitumia siku nne pamoja na wanafunzi hao. Asubuhi walitazama video zinazotegemea Biblia za lugha ya Kikekchi kwenye jw.org, na wakajifunza broshua Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo? Alasiri, walitazama sehemu mbalimbali za JW Broadcasting. Pia, mwangalizi wa mzunguko alipanga kila mmoja wa wanafunzi hao apate mtu wa kujifunza naye Biblia.

Wakati wa siku hizo nne, Mashahidi walihubiri pia katika vijiji jirani vya Kikekchi na kuwakaribisha watu kwenye mkutano wa pekee. Kwenye mkutano huo uliohudhuriwa na watu 47, akina ndugu waliwakaribisha wote ambao wangependa kujifunza Biblia. Familia 11 ziliomba kufundishwa.

Miezi michache baadaye, wazee walifanya mipango kuwa na mikutano katika kijiji cha kwanza kila mwisho juma. Leo, watu 40 hivi wanahudhuria mikutano hiyo kwa ukawaida. Na akina ndugu walipofanya Ukumbusho wa kifo cha Yesu, walifurahi watu 91 walipohudhuria.

Marta anapokumbuka jinsi simulizi hili lote lilivyoanza, anasema hivi: “Ninamshukuru Yehova sana. Nyakati nyingine ninahisi kwamba siwezi kutimiza mengi. Lakini sisi ni vifaa mikononi mwa Mungu. Alijua kilichokuwa moyoni mwa wanakijiji hao, naye akawavuta kwa watu wake. Yehova anawapenda.”

a Mwangalizi wa mzunguko ni mhudumu wa Mashahidi wa Yehova ambaye huyatembelea makutaniko 20 hivi yanayofanyiza mzunguko.