Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

CAMILLA ROSAM | SIMULIZI LA MAISHA

Kumtii Yehova Ndilo Jambo Muhimu Zaidi Maishani Mwangu

Kumtii Yehova Ndilo Jambo Muhimu Zaidi Maishani Mwangu

 Babu na nyanya yangu walijifunza kuhusu ahadi za Ufalme wa Yehova mwaka wa 1906, mwana wao alipokufa kutokana na ugonjwa wa koo. Daktari aliyekuwa akimtibu alikuwa Mwanafunzi wa Biblia, jina ambalo Mashahidi wa Yehova walitumia wakati huo. Daktari huyo aliwafariji kwa kuwaeleza kuhusu tumaini linalopatikana katika Biblia, kutia ndani tumaini la ufufuo. Kwa sababu hiyo, babu na nyanya yangu, mama yangu, na pia dada ya mama waliamua kuwa Wanafunzi wa Biblia.

 Kwa miaka mingi, wote walimtumikia Yehova kwa bidii. Nyanya, mama, na dada ya mama hata walifanya kazi ya kuwasaidia watu kupata viti katika ukumbi, sinema ya “Photo-Drama of Creation” ilipokuwa ikionyeshwa kwenye jiji la Chicago lililo katika jimbo la Illinois, Marekani. Hata hivyo, inasikitisha kwamba, ni Mama pekee aliyeendelea kumtumikia Yehova. Hali hiyo ilikuwa ngumu kwake kwa sababu siku zote familia yao ilikuwa na uhusiano wa karibu, nao walimtumikia Yehova kwa pamoja hadi miaka ya 1930. Mama alikuwa mshikamanifu na mtiifu kwa Yehova na hilo lilinivutia sana. Baba yangu pia aliniwekea mfano mzuri kwa sababu alikuwa Mwanafunzi mwaminifu wa Biblia.

Picha ya familia, 1948

 Nilizaliwa mwaka wa 1927 na nilikuwa mtoto wa kwanza kati ya watoto sita. Familia yetu yote ilishikamana na kweli. Baba yetu alifanya kazi ya useremala na tuliishi kwenye nyumba nzuri nje ya jiji la Chicago. Tulikuwa na bustani kubwa ya mboga na pia tulifuga kuku na bata.

 Nilipenda kufanya kazi. Moja kati ya majukumu yangu katika familia yetu ilikuwa ni kushona soksi zilipotoboka. Siku hizi watu hutupa tu soksi zinapotoboka; lakini zamani tulizishona. Soksi hizo zilishonwa kwa sindano na uzi. Ustadi huo ulinisaidia sana baadaye maishani kwa sababu nilishona sana.

Wazazi Wetu Walituwekea Mfano Mzuri

 Baba alihakikisha kwamba familia yetu haikupuuza mambo ya kiroho. Kwa hiyo, tulihudhuria mikutano yote ya Kikristo, tulishiriki huduma ya shambani kwa ukawaida, na tulisoma andiko la Biblia kila siku. Jumamosi jioni, tulijifunza Biblia tukiwa familia kwa kutumia Mnara wa Mlinzi.

 Baba aliweka bango la kielektroni upande wa ndani wa dirisha la sebule yetu ili kuwapa ushahidi mzuri majirani wetu. Bango hilo lilikuwa limetengenezwa na akina ndugu na lilitangaza hotuba ya watu wote au mojawapo ya machapisho yetu. Ndani ya bango hilo kulikuwa na taa iliyowaka na kuzima na hivyo ilivuta uangalifu wa watu waliokuwa wakipita. Baba pia alibandika mabango mengine mawili kwenye gari letu.

Tulihubiri kwa kutumia gramafoni pamoja na mama

 Kwa neno na tendo, baba alitufundisha umuhimu wa kumtii Yehova. Mama alimuunga mkono kabisa. Mdogo wetu wa mwisho alipokuwa na umri wa miaka mitano, Mama alianza kumtumikia Yehova akiwa painia. Mama aliishi kwa muda mrefu na aliendelea kupainia kwa maisha yake yote. Nilikuwa na wazazi wazuri sana.

 Maisha ya wakati huo yalikuwa tofauti sana na jinsi maisha yalivyo leo. Hatukuwa na televisheni kwa hiyo, mimi na wadogo zangu tuliketi sakafuni na kusikiliza hadithi zenye kusisimua kwenye redio. Zaidi ya hilo, familia yetu ilifurahia programu za kiroho ambazo tengenezo la Yehova lilipeperusha kupitia redio.

Makusanyiko, Gramafoni, na Mabango

 Tulipenda kuhudhuria makusanyiko ya Mashahidi wa Yehova. Katika kusanyiko lililofanywa mwaka wa 1935, tulijifunza kwamba “umati mkubwa” utakaookoka “dhiki kuu,” unaotajwa kwenye Ufunuo 7:9, 14, una tumaini la kuishi milele katika Paradiso duniani. Kabla ya mwaka huo, wazazi wangu wote wawili walishiriki mifano katika siku ya Ukumbusho. Hata hivyo, baada ya kusanyiko hilo, baba tu ndiye aliyeendelea kushiriki mifano hiyo. Sasa, mama alijua kwamba hakuwa na tumaini la kutawala pamoja na Kristo mbinguni bali alikuwa na tumaini la kuishi milele duniani.

 Mwaka wa 1941, tulipokuwa kwenye kusanyiko lililofanyika St. Louis, Missouri, Joseph Rutherford aliyekuwa akiongoza kazi wakati huo alitoa kitabu Children. Kwa furaha, wahudhuriaji walipiga makofi kwa muda mrefu! Wakati huo nilikuwa na umri wa miaka 14 na nilikuwa nimebatizwa mwaka uliotangulia. Ninakumbuka vizuri nikiwa kwenye mstari pamoja na watoto wengine tukielekea kwenye jukwaa ili kupokea nakala ya kitabu hicho.

Mimi na Lorraine, 1944

 Katika miaka hiyo ya mapema, utumishi ulikuwa tofauti na jinsi ulivyo leo. Katika miaka ya 1930 tulitumia gramafoni ambayo tulibeba ili kucheza rekodi za hotuba za Biblia kwa ajili ya wenye nyumba. Kabla ya kubisha mlango, tuliweka vizuri diski ya gramafoni na kuhakikisha kwamba ipo tayari kucheza. Mwenye nyumba alipokuja mlangoni tungemweleza kifupi kusudi la kumtembelea kisha tungecheza hotuba ya dakika nne na nusu iliyotegemea Biblia na kumpa chapisho. Watu walioishi katika eneo letu walisikiliza kwa heshima. Sikumbuki nikikutana na mtu yeyote ambaye alikuwa mkali au asiye na adabu. Nilipoanza kupainia nikiwa na umri wa miaka 16, baba yangu alinipa zawadi, yaani, gramafoni yangu mwenyewe nami nilifurahia kuitumia katika huduma. Nilifanya upainia pamoja na dada mzuri sana aliyeitwa Lorraine.

 Njia nyingine ya kuhubiri tuliyotumia ni maandamano ya kutangaza habari. Kwa muda fulani, tuliyaita maandamano hayo sandwich-sign parades, kwa sababu tulivaa mabango mawili, moja kwa mbele na lingine mgongoni. Mabango haya yalikuwa na ujumbe kama vile “Dini Ni Mtego na Hila” na “Mtumikie Mungu na Kristo Mfalme.”

Tulisimama ili kupigwa picha tukiwa tumebeba mabango

 Mikutano yetu ilitutayarisha kukabiliana na upinzani na ilitufundisha jinsi ya kuitetea kweli. Na tulipata upinzani. Kwa mfano, mara tu tulipoanza kugawa magazeti yetu katika eneo moja lenye maduka na watu wengi, tulichukuliwa na gari la polisi na kupelekwa hadi kwenye kituo cha polisi. Tuliachiliwa huru baada ya saa kadhaa, nasi tulikuwa na shangwe kwa sababu tulikuwa tumeteswa kwa kumtii Yehova.

Ndoa, Gileadi, na Mwito wa Kwenda Jeshini

Mimi na Eugene katika siku yetu ya harusi

 Siku moja, Lorraine alinitambulisha kwa ndugu aliyeitwa Eugene Rosam. Lorraine alikuwa amekutana na ndugu huyo kwenye kusanyiko huko Minneapolis, Minnesota. Eugene alilelewa katika eneo la Key West, Florida. Alipokuwa kidato cha pili alifukuzwa shuleni kwa kukataa kushiriki katika sherehe fulani ya kizalendo. Baada ya hapo, alianza upainia moja kwa moja. Siku moja Eugene alikutana na msichana ambaye hapo awali walikuwa darasa moja. Msichana huyo alishindwa kuelewa kwa nini mwanafunzi mzuri kama Eugene alikuwa amefukuzwa shuleni. Eugene alimpa majibu akitumia Maandiko na hilo lilimchochea msichana huyo kukubali kujifunza Biblia. Aliikubali kweli, akabatizwa na kuwa dada mwaminifu.

Tulipokuwa Key West, 1951

 Mimi na Eugene tulifunga ndoa mwaka wa 1948. Mara tu baada ya kufunga ndoa tulianza kufanya upainia jijini Key West. Mwaka wa 1951, tulialikwa kuhudhuria darasa la 18 la Shule ya Gileadi na tulihitimu mwanzoni mwa mwaka wa 1952. Tulipokuwa katika shule hiyo tulifundishwa Kihispania pia, hivyo tulitarajia kwamba tungepewa mgawo wa kuwa wamishonari katika nchi inayozungumza Kihispania. Hata hivyo, mambo hayakwenda hivyo. Tulipokuwa Gileadi, vita vya Korea vilizidi kupamba moto na Eugene akaitwa jeshini. Tulishangazwa na jambo hilo kwa kuwa katika Vita vya Pili vya Ulimwengu, Eugene alipewa ruhusa ya kutotumika jeshini kwa sababu alikuwa mtumishi wa kidini. Tuliambiwa tubaki Marekani kwa sababu ya mwito huo. Nililia kwa uchungu. Miaka miwili baadaye, Eugene alipewa tena ruhusa ya kutotumika jeshini. Changamoto hiyo ilitufundisha somo zuri—mlango mmoja unapofungwa, Yehova ana uwezo wa kufungua mlango mwingine, naye alifanya hivyo. Tulipaswa tu kuonyesha subira.

Darasa letu la Gileadi

Tulizungukia Makutaniko Kisha Tukaenda Kanada!

 Mwaka wa 1953, tulifanya upainia katika kutaniko la Kihispania huko Tucson, Arizona, kisha tukapewa kazi ya kuzungukia makutaniko. Tulitumikia katika mizunguko huko Ohio, California, na New York City. Mwaka wa 1958, mume wangu alipewa mgawo wa kuwa mwangalizi wa wilaya a na tulizungukia California na Oregon. Kwa kawaida, tulikaa katika nyumba za ndugu na dada. Kisha mwaka wa 1960, tulienda Kanada na Eugene alipewa mgawo wa kufundisha Shule ya Huduma ya Ufalme kwa ajili ya wazee wa makutaniko. Tuliendelea kuishi Kanada hadi mwaka wa 1988.

 Ninakumbuka mambo mazuri tuliyojionea katika utumishi wetu nchini Kanada, jambo moja ni kisa kuhusu familia fulani ambayo mimi na dada mmoja tulipata tulipokuwa tukihubiri nyumba kwa nyumba. Kwanza kabisa, tulimkuta Gail ambaye alituambia kwamba watoto wake walikuwa wamehuzunishwa sana na kifo cha babu yao. Wavulana hao walimuuliza, “Kwa nini amekufa? Ameenda wapi?” Gail hakuwa na majibu. Basi tulimwonyesha majibu yenye kufariji kutoka kwenye Biblia.

 Kipindi hicho Eugene alikuwa akitumikia akiwa mwangalizi wa mzunguko kwa hiyo tungekuwa pamoja na kutaniko hilo kwa juma moja tu. Hata hivyo, yule dada niliyekuwa nimeambatana naye alimrudia Gail. Matokeo yakawaje? Gail, na mume wake, Bill, pamoja na wana wao watatu—Christopher, Steve, na Patrick, wote walikubali kweli. Sasa Chris anatumikia akiwa mzee nchini Kanada. Steve anatumikia akiwa mwalimu katika shule ya Biblia iliyo Palm Coast, Florida. Naye Patrick ni mshiriki wa Halmashauri ya Tawi nchini Thailand. Kwa miaka mingi, mimi na Eugene tumekuwa na urafiki wa karibu na familia hiyo. Ninafurahi sana kwamba nilichangia kidogo kazi ya kuisaidia familia hiyo kumjua Yehova!

Ziara za Kuwatembelea Madaktari na Hatimaye Halmashauri za Uhusiano na Hospitali

 Tulipokuwa Kanada, Yehova alimfungulia Eugene mlango mwingine wenye kusisimua na wenye matokeo mazuri. Acha niwaelezee.

 Miaka mingi iliyopita, watu hawakuelewa kwa nini tulikataa kutiwa damu mishipani na hivyo walikuwa na maoni mabaya kutuhusu. Magazeti mbalimbali nchini Kanada yalikuwa yakichapisha hadithi zenye madai kwamba watoto wa Mashahidi wa Yehova walikuwa wakifa kwa sababu wazazi wao walikataa watiwe damu mishipani. Mume wangu alikuwa na pendeleo la kushiriki katika jitihada za kuthibitisha kwamba hadithi hizo zilikuwa za uwongo.

 Muda mfupi kabla ya kusanyiko la kimataifa la 1969 lililofanywa huko Buffalo, New York, Eugene alienda pamoja na ndugu wengine kutembelea hospitali kubwa zilizokuwa katika eneo hilo ili kuwajulisha kwamba Mashahidi 50,000 hivi kutoka Kanada na Marekani watahudhuria kusanyiko hilo. Ikiwa dharura ya kitiba ingetokea kusanyikoni, ingekuwa rahisi kwa madaktari kutusaidia kwa sababu wangekuwa tayari wameelewa msimamo wetu kuhusu damu na kujua manufaa zake. Ndugu hao waliwapa madaktari makala zilizotolewa kwenye majarida yenye kuheshimika na zilieleza kuhusu matibabu yasiyohusisha damu. Madaktari hao waliitikia vizuri na hilo lilimchochea Eugene na ndugu wengine kufanya mipango ya kutembelea hospitali kotekote nchini Kanada. Vilevile, waliwasaidia wazee wa makutaniko kushughulikia dharura za kitiba kwa njia nzuri zaidi.

 Kadiri muda ulivyosonga, jitihada hizo zilikuwa na matokeo mazuri. Kwa kweli, jitihada hizo zilikuwa mwanzo tu wa kazi kubwa hata zaidi! Jinsi gani?

Nilipenda kufanya kazi katika idara ya ushonaji

 Katika miaka ya 1980, Eugene alipigiwa simu na Milton Henschel kutoka makao makuu yaliyokuwa Brooklyn, New York. Baraza Linaloongoza lilitaka kupanua programu iliyokuwa ikiendelea nchini Marekani ya kuwapa madaktari habari. Lengo lao lilikuwa kuwafikia madaktari wengi zaidi. Kwa hiyo, mimi na Eugene tulihamia Brooklyn, na Januari 1988, Baraza Linaloongoza lilianzisha idara nyingine katika makao makuu iliyoitwa Huduma za Habari za Hospitali. Baadaye, mume wangu pamoja na ndugu wengine wawili walipewa mgawo wa kufanya semina, kwanza nchini Marekani na kisha katika nchi nyingine. Punde si punde, Idara za Habari za Hospitali zilianzishwa katika matawi mengine na Halmashauri za Uhusiano na Hospitali (HLC) zilianzishwa katika majiji mbalimbali. Mashahidi wengi pamoja na watoto wao wamenufaika kutokana na maandalizi hayo yenye upendo kutoka kwa Yehova. Eugene alipokuwa akifanya semina na kutembelea hospitali, mimi nilifanya kazi katika Betheli tuliyofikia, mara nyingi nilikuwa jikoni au nilipewa kazi katika idara ya kushona.

Darasa la Halmashauri ya Uhusiano na Hospitali lililofanyika Japani

Jaribu Kubwa Zaidi Maishani Mwangu

 Mwaka wa 2006, nilikabili jaribu kubwa zaidi maishani mwangu, mume wangu mpendwa, Eugene, alikufa. Ninamkosa sana, alinionyesha upendo na tulifanya mambo pamoja! Ni nini ambacho kimenisaidia kuvumilia jaribu hili? Mambo kadhaa. Kwa mfano, ninaendelea kukaa karibu na Yehova kwa kusali na kusoma Biblia kwa ukawaida. Ninasikiliza mazungumzo ya andiko la siku yanayofanywa na familia ya Betheli. Ninasoma sura nzima ya Biblia ambapo andiko la siku limetolewa. Nami ninajitahidi kufanya kazi kwa bidii katika Idara ya Ushonaji kwa sababu ninauthamini sana mgawo wangu. Zamani, hata nilipata pendeleo la kushona mapazia kwa ajili ya Majumba ya Kusanyiko yaliyo New Jersey na New York. Kwa sasa, ninatumikia kwenye Betheli ya Fishkill ambako ninarekebisha nguo na kazi nyingine ndogondogo. b

 Ninaona kwamba jambo muhimu zaidi maishani ni kumpenda Yehova na kumtii Yeye na pia tengenezo lake. (Waebrania 13:17; 1 Yohana 5:3) Ninafurahi kwamba mimi na Eugene tulitanguliza mambo hayo maishani mwetu. Kwa sababu hiyo, nina uhakika kabisa kwamba Yehova atatubariki kwa kutupa uzima wa milele kwenye dunia paradiso, kutia ndani shangwe ya kuonana tena.​—Yohana 5:28, 29.

a Waangalizi wa mzunguko hutembelea kutaniko mojamoja, lakini waangalizi wa wilaya walikuwa na jukumu la kutembelea mizunguko na kutoa hotuba kwenye makusanyiko ya mizunguko.

b Dada Camilla Rosam alikufa Machi 2022 makala hii ilipokuwa ikitayarishwa. Alikuwa na umri wa miaka 94.