Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Inawezekana Kuwa na Mfumo wa Kiuchumi Wenye Usawa?

Je, Inawezekana Kuwa na Mfumo wa Kiuchumi Wenye Usawa?

 Katika nchi moja baada ya nyingine, watu wamekuwa wakiandamana wakipinga kile wanachoona kuwa hali za kiuchumi zisizo na usawa. Ugonjwa wa COVID-19 umefanya hali hiyo kuwa mbaya na hata kutokeza fujo katika maeneo mbalimbali, kwa sababu vizuizi vya kutotoka nyumbani, upungufu wa vitu vya msingi, na ugumu wa kupata huduma za afya, vimefanya tofauti kubwa iliyopo kati ya matajiri na maskini ionekane wazi.

 Je, matatizo ya kiuchumi yanayowasababishia watu matatizo yatakwisha? Ndiyo. Biblia inafafanua kile ambacho Mungu atafanya ili kutatua matatizo tunayokabili.

Matatizo ya kiuchumi ambayo Mungu atatua

 Tatizo: Wanadamu hawajatokeza mfumo wa kiuchumi unaokidhi mahitaji ya watu wote.

 Suluhisho: Mungu ataleta serikali ambayo itachukua mahali pa serikali za wanadamu. Serikali hiyo inaitwa Ufalme wa Mungu. Itatawala dunia yote kutoka mbinguni.—Danieli 2:44; Mathayo 6:10.

 Matokeo: Kwa kuwa Ufalme wa Mungu utatawala juu ya dunia yote, itasimamia shughuli za dunia kwa kikamilifu. Watu hawatakuwa maskini tena wala hawatakuwa na wasiwasi kuhusu kuwa na mahitaji ya kutosha. (Zaburi 9:7-9, 18) Badala yake, watafurahia matokeo ya kazi yao na kuishi maisha yenye kuridhisha wakiwa na familia zao. Biblia inaahidi hivi: “Watajenga nyumba na kuishi ndani yake, nao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake. Hawatajenga na mtu mwingine akae ndani yake, wala hawatapanda na watu wengine wale.”—Isaya 65:21, 22.

 Tatizo: Watu hawawezi kuepuka hali zinazowafanya wateseke na kukosa mahitaji muhimu maishani.

 Suluhisho: Kupitia Ufalme wake, Mungu ataondoa mambo yote yanayowafanya watu wawe na hofu na wasijihisi salama.

 Matokeo: Chini ya uongozi wa Mungu, watu hawatapatwa tena na mambo yanayowafanya wapoteze vitu muhimu maishani. Kwa mfano, vita, ukosefu wa chakula, magonjwa ya mlipuko hayatatukia tena. (Zaburi 46:9; 72:16; Isaya 33:24) Mungu anasema hivi: “Watu wangu watakaa katika makao ya kudumu yenye amani, katika makao salama na mahali pa kupumzika penye utulivu.”—Isaya 32:18.

 Tatizo: Mara nyingi watu wenye ubinafsi na wenye pupa huwadhulumu wengine.

 Suluhisho: Raia wa Ufalme wa Mungu wataonyesha wazi kwamba wanawapenda wengine zaidi ya wanavyojipenda.—Mathayo 22:37-39.

 Matokeo: Chini ya Ufalme wa Mungu, kila mtu atamwiga Mungu kuonyesha upendo, ambao “hautafuti faida zake wenyewe.” (1 Wakorintho 13:4, 5) Biblia inasema hivi: “Hawatasababisha madhara yoyote wala uharibifu wowote katika mlima wangu wote mtakatifu, kwa maana kwa hakika dunia itajaa ujuzi kumhusu Yehova a kama maji yanavyoifunika bahari.”—Isaya 11:9.

 Biblia inaonyesha kwamba tunaishi katika siku za mwisho za mfumo wa huu mambo na kwamba hivi karibuni Mungu atatimiza ahadi yake ya kuleta mwisho wa matatizo ya kiuchumi. b (Zaburi 12:5) Kwa sasa, kanuni za Biblia zinaweza kukusaidia kukabiliana na matatizo ya kiuchumi unayopata. Kwa mfano, ona makala yenye kichwa “Jinsi ya Kuishi Ukiwa na Pesa Kidogo” na “Maoni Yenye Usawaziko Kuhusu Pesa.”

a Yehova ni jina la Mungu kama linavyoonyeshwa katika Biblia.—Zaburi 83:18.

b Ili kuona kwa nini unaweza kuiamini Biblia, ona makala yenye kichwa “Biblia—Chanzo Kinachotegemeka cha Kweli.”