Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Biblia Inaweza Kukusaidia Kukabiliana na Mabadiliko Makubwa ya Hali ya Hewa?

Je, Biblia Inaweza Kukusaidia Kukabiliana na Mabadiliko Makubwa ya Hali ya Hewa?

 Je, wewe ni miongoni mwa mamilioni ambao wameathiriwa na hali mbaya ya hewa? Hali mbaya ya hewa na madhara yake huja katika njia nyingi tofauti kama vile vimbunga, tufani, dhoruba, mafuriko, au madhara yanayotokana na upepo mkali. Mvua kubwa zinaweza kusababisha mmomonyoko wa udongo, dhoruba zinaweza kuja na radi ambazo zinaweza kuanzisha moto mkubwa wa msituni. Ukame, joto kali kupita kiasi, na dhoruba za barafu wakati wa baridi kali navyo pia vinaweza kuleta uharibifu mkubwa.

 Katika maeneo mengi duniani, misiba ya asili inayosababishwa na mabadiliko ya hali ya hewa inazidi kuongezeka kwa kasi zaidi na ni yenye nguvu zaidi. Kulingana na Shirika la Kimataifa la Msalaba Mwekundu na Shirika la Mwezi Mwekundu: “Watu wengi zaidi wanaathiriwa na majanga kuliko wakati mwingine kwa kuwa mafuriko, dhoruba, na ukame zimeongezeka. Kwa sababu hiyo, watu wengi wanakufa, wengi wanashindwa kupata riziki, na mamilioni ya watu wamepoteza makao yao.”

 Mambo haya yanapotokea watu huathiriwa kimwili na kihisia. Wanateseka kwa sababu wamepoteza nyumba, mali, au hata wapendwa wao.

 Ikiwa umeathiriwa na majanga yanayotokana na mabadiliko ya hali ya hewa, Biblia inaweza kukusaidia. Inaandaa faraja, tumaini, na mashauri yanayofaa ambayo yamewasaidia watu wengi walioathiriwa na majanga yaliyosababishwa na hali mbaya ya hewa. (Waroma 15:4) Biblia pia inajibu swali muhimu ambalo linawasumbua watu wengi: Kwa nini Mungu aliruhusu hili litendeke? Je, ananiadhibu?

Hali mbaya ya hewa tunayokabiliana nayo si adhabu kutoka kwa Mungu

 Biblia inafundisha kwamba Mungu hasababishi mateso ambayo yanawapata watu. Inatuhakikishia kwamba “Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu, wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote.” (Yakobo 1:13) Hii inamaanisha kwamba si yeye anayesababisha hali mbaya ya hewa inayowaathiri watu leo.

 Biblia inarekodi za wakati ambapo Mungu alitumia nguvu za asili ili kuwaadhibu waovu. Lakini matukio hayo ni tofauti sana na majanga ya siku zetu, ambayo hutokea ghafla na kuwaathiri watu wazuri na wabaya. Tofauti na hilo, masimulizi ya Biblia yanaonyesha kwamba katika pindi hizo Mungu aliwalinda wale wasio na hatia, alitoa maonyo mapema, na alieleza sababu za kuchukua hatua hizo. Kwa mfano, Mungu alieleza sababu za kuleta gharika katika siku za Noa, alitoa onyo mapema, na akamlinda Noa na familia yake.—Mwanzo 6:13; 2 Petro 2:5.

 Ili upate habari zaidi inayoonyesha kwa nini misiba ya asili inayotokea leo si adhabu kutoka kwa Mungu, ona makala yenye kichwa “Biblia Inasema Nini Kuhusu Misiba ya Asili?

Mungu anawajali watu walioathiriwa na hali mbaya ya hewa

 Biblia inafunua kwamba Yehova a Mungu anatujali na ni mwenye huruma. Fikiria mistari ifuatayo inayofariji.

  •   Isaya 63:9: “Katika taabu zao zote, yeye [Mungu] alitaabika.”

     Maana: Yehova anaumia sana kuwaona watu wakiteseka.

  •   1 Petro 5:7: “Yeye anawajali ninyi.”

     Maana: Yehova anahangaikia hali yako.

 Kwa kuwa Yehova anawahurumia watu na kuwajali, hilo humchochea kutenda. Anawafariji watu kupitia ushauri wenye kutegemeka unaopatikana katika Biblia na pia tumaini zuri la wakati ujao ambapo hakutakuwa na majanga yanayosababishwa na hali mbaya ya hewa.—2 Wakorintho 1:3, 4.

Wakati ambapo hakutakuwa na majanga yanayosababishwa na hali mbaya ya hewa

 Biblia inataja ahadi ya Yehova ya ‘kutupatia sisi wakati ujao na tumaini.’ (Yeremia 29:11) Anataka watu wafurahie maisha katika dunia paradiso, na si kuogopa madhara ya hali ya hewa.—Mwanzo 1:28; 2:15; Isaya 32:18.

 Mungu atatumia Ufalme wake kutimiza hilo. Ufalme huo ni serikali ya mbinguni inayoongozwa na Yesu. (Mathayo 6:10) Yesu ana hekima na nguvu zinazohitajika ili kuzuia majanga ya hali ya hewa. Yesu alipokuwa duniani, alionyesha uwezo wake wa kudhibiti hali ya hewa. (Marko 4:37-41) Atatawala kwa hekima na uelewaji, naye atawafundisha wanadamu jinsi ya kutunza mazingira na kuishi kwa njia ambayo hawataharibu mazingira. (Isaya 11:2) Chini ya utawala wa Yesu, watu hawataathiriwa kamwe na hali mbaya ya hewa.

 Huenda ukajiuliza, ‘Ni wakati gani ambapo Yesu atatumia nguvu zake kudhibiti hali ya hewa?’ Ili kujibu swali hilo, ona makala yenye kichwa “Ufalme wa Mungu Utaanza Kutawala Dunia Lini?

Kukabiliana na mabadiliko makubwa ya hali ya hewa

 Ushauri wa Biblia unaweza kukusaidia kabla ya mabadiliko makubwa ya hali ya hewa kutokea, yanapotokea, na baada ya kutokea.

  •   Kabla: Jitayarishe kiakili ili kuchukua hatua haraka.

     Biblia inasema nini: “Mtu mwerevu huona hatari na kujificha, lakini wajinga husonga mbele na kupata madhara.”—Methali 22:3.

     Maana: Chunguza aina za majanga yanayoweza kuathiri eneo lenu ili uweze kuchukua hatua haraka na kuilinda familia yako.

     Simulizi: “Siku tulipookoka moto wa msituni, tulikuwa tumejitayarisha mapema. Tulikuwa na mifuko yetu ya dharura. Tulitia ndani dawa zetu na pia nguo zetu. Watu waliotuzunguka walikuwa wamechanganyikiwa na hawakujua wafanye nini. Lakini sisi tulikuwa na kila kitu tulichohitaji, ninashukuru sana kwa sababu ya hilo!”—Tamara, California, Marekani.

  •   Yanapotokea: Kazia fikira mambo muhimu zaidi.

     Biblia inasema nini: “Hata mtu anapokuwa na vitu vingi, uhai wake hautokani na vitu alivyo navyo.”—Luka 12:15.

     Maana: Uhai ni wenye thamani kuliko mali.

     Simulizi: “Kimbunga Lawin b kilipoharibu nyumba yetu, sikujua nifanye nini. Lakini jambo moja nililofanya ni kusali kwa Yehova Mungu kutoka moyoni. Nilitambua kwamba tumepoteza vitu vya kimwili tu na si maisha yetu.”—Leslie, Ufilipino.

  •   Baada: Usihangaishwe na ya kesho.

     Biblia inasema nini: “Msihangaike kamwe kuhusu kesho, kwa maana kesho itakuwa na mahangaiko yake yenyewe. Kila siku ina matatizo yake ya kutosha.”—Mathayo 6:34.

     Maana: Usihangaikie kupita kiasi kuhusu matatizo yatakayotokea wakati ujao.

     Simulizi: “Baada ya Kimbunga Irma kufanya nyumba yangu ifurike, kulikuwa na maamuzi mengi ya kufanya kuliko wakati mwingine wowote, nami nilikuwa na mkazo mwingi. Nilijaribu kufuata ushauri wa Biblia wa kuepuka kuhangaika kupita kiasi kuhusu mambo ya kesho. Niligundua kwamba kwa msaada wa Yehova, niliweza kukabiliana na mambo mengi kuliko nilivyofikiri.”—Sally, Florida, Marekani.

 Ili kupata mapendekezo mengine yatakayokusaidia, ona makala yenye kichwa “Majanga Yanapotokea—Unachoweza Kufanya Ili Uokoke.”

a Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu—Zaburi 83:18.

b Jina lingine ni Kimbunga Haima.