Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

Yehova Amenipa Zaidi ya Ninavyostahili

Yehova Amenipa Zaidi ya Ninavyostahili

Nilipokuwa na umri wa miaka 17 nilikuwa na malengo na mahangaiko kama vijana wengine. Nilipenda kushirikiana na rafiki zangu kuogelea na kucheza mpira wa miguu. Hata hivyo jioni moja maisha yangu yalibadilika kabisa. Nilipata aksidenti mbaya ya pikipiki iliyofanya nipooze kuanzia shingoni kushuka chini. Hilo lilitukia miaka 30 hivi iliyopita, na nimekuwa mgonjwa wa kitandani kwa muda mrefu sana.

Nililelewa katika jiji la Alicante, pwani ya mashariki mwa Hispania. Familia yetu haikuwa na ushirikiano, hivyo nikiwa kijana nilitumia muda mwingi mitaani. Jirani na nyumba yetu kulikuwa na karakana ya kutengeneza tairi. Hapo nikawa rafiki ya José María, mmoja kati ya wafanyakazi wa karakana hiyo. Alikuwa mchangamfu na alinijali sana, mambo ambayo niliyakosa nyumbani. Katika nyakati za shida, yeye alikuwa kama ndugu yangu halisi, rafiki wa kweli, ingawa alinizidi umri kwa miaka 20.

José María alikuwa akijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Ninaweza kusema kwamba alipenda Maandiko, na mara nyingi alinieleza kweli za Biblia. Nilimsikiliza kwa heshima ingawa sikupendezwa na mambo aliyoniambia. Nikiwa kijana nilitamani mambo tofauti kabisa. Hata hivyo, mambo yangebadilika.

AKSIDENTI ILIYOBADILI MAISHA YANGU

Nisingependa kusimulia mengi kuhusu aksidenti hiyo ya barabarani. Ninachoweza kusema ni kwamba nilikuwa mpumbavu na sikuwa makini. Kwa siku moja tu, maisha yangu yalibadilika kabisa. Kutoka kuwa kijana mwenye nguvu, mpaka kupooza na kukaa hospitalini kwa muda mrefu. Haikuwa rahisi kuikubali hali yangu mpya. Nilijiuliza: ‘Je, kuna sababu yoyote ya kuendelea kuishi?’

José María alikuja kuniona, na mara moja akafanya mpango ili washiriki wa kutaniko la Mashahidi wa Yehova katika eneo hilo wanitembelee hospitalini. Ziara hizo za ukawaida zilinigusa moyo sana. Baada ya kutoka katika wodi ya wagonjwa mahututi, nilianza kujifunza Biblia. Nilielewa sababu kwa nini wanadamu wanateseka na kufa, na kwa nini Mungu ameruhusu mambo mabaya yatokee. Pia, nilijifunza kuhusu ahadi za Mungu za wakati ujao, yaani, dunia nzima itajaa wanadamu wakamilifu na hakuna mwanadamu atakayesema: “Mimi ni mgonjwa.” (Isaya 33:24) Kwa mara ya kwanza maishani nilipata kujua tumaini hilo zuri.

Nilipotoka hospitali, nilifanya maendeleo zaidi katika funzo langu la Biblia. Kwa kutumia kiti cha pekee chenye magurudumu, nilihudhuria baadhi ya mikutano ya Mashahidi wa Yehova na kushiriki katika kazi yao ya kuhubiri. Mnamo Novemba 5, 1988, nikiwa na umri wa miaka 20, nilibatizwa kwa kuzamishwa katika maji kwenye kidimbwi maalumu cha bafu. Yehova Mungu amenisaidia kuwa na mtazamo mpya kuhusu uhai. Hata hivyo, nilipaswa kufanya nini ili kumshukuru?

KUFANYA MAENDELEO LICHA YA ULEMAVU

Nilijua kwamba sipaswi kuruhusu hali yangu inizuie kufanya yote ninayoweza katika utumishi wa Yehova. Nilitaka kufanya maendeleo. (1 Timotheo 4:5) Mwanzoni, haikuwa rahisi, kwa kuwa familia yangu ilipinga imani yangu mpya. Hata hivyo, waamini wenzangu ambao ni ndugu na dada zangu wa kiroho, walihakikisha kwamba sikosi mikutano na kwamba ninashiriki kwa ukawaida katika kazi ya kuhubiri.

Hata hivyo, kadiri wakati ulivyopita, ilionekana wazi kwamba nilihitaji kutunzwa muda wote katika vituo vya watu wenye mahitaji ya pekee. Baada ya kutafuta kwa muda mrefu, hatimaye nilifaulu kupata kituo kinachofaa katika jiji la Valencia, kilomita 160 upande wa kaskazini wa Alicante. Kituo hicho kimekuwa makao yangu ya kudumu.

Ingawa ni mgonjwa wa kitandani, nimeazimia kuwahubiria wengine

Ingawa mimi ni mgonjwa wa kitandani, niliazimia kufanya maendeleo. Nilitumia pensheni ya walemavu na pesa nyingine kununua kompyuta niliyoweka jirani na kitanda changu. Nilinunua pia simu ya mkononi. Kwa hiyo, kila asubuhi wafanyakazi hunisaidia kuwasha kompyuta na simu yangu. Ili kutumia kompyuta, ninatumia gia ninayoiongoza kwa kutumia kidevu changu. Pia, nina fimbo maalumu ninayoishika kwa kutumia mdomo. Fimbo hii hunisaidia kuandika barua kwenye kompyuta na kupiga simu.

Ninaweza kupiga simu kwa kutumia fimbo maalumu

Teknolojia hii imenisaidiaje? Kwanza kabisa, imeniwezesha kutumia tovuti ya jw.org na Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO. Kwa kweli, teknolojia hiyo imethibitika kuwa kifaa muhimu sana kwangu! Mara nyingi mimi hutumia saa kadhaa kila siku kujifunza na kufanya utafiti katika machapisho yanayotegemea Biblia ili niweze kuendelea kujifunza kuhusu Mungu na sifa zake nzuri. Ninapohisi upweke au kuvunjika moyo kwa njia fulani, sikuzote kumekuwa na habari yenye kutia moyo kwenye tovuti.

Kompyuta yangu inaniwezesha pia kusikiliza na kushiriki katika mikutano ya kutaniko. Ninaweza kutoa maelezo, sala, hotuba na hata kusoma gazeti la Mnara wa Mlinzi ninapokuwa na mgawo huo. Ingawa siwezi kuhudhuria mikutano hiyo kihalisi, bado ninahisi kwamba mimi ni sehemu ya kutaniko.

Kuwa na simu pamoja na kompyuta huniwezesha pia kushiriki kikamili katika kazi ya kuhubiri. Ni kweli kwamba, siwezi kwenda nyumba kwa nyumba kama ambavyo Mashahidi wa Yehova wengi hufanya. Lakini hilo halinizuii kuhubiri. Kwa kutumia vifaa hivi ninaweza kuwahubiria wengine. Kwa kweli, ninafurahia sana mazungumzo ya simu hivi kwamba wazee wa kutaniko letu wameniomba kuratibu kampeni za mahubiri kwa kutumia simu. Kampeni hizi huwasaidia sana washiriki wa kutaniko ambao kwa sababu ya kuugua, hawezi kutoka nje ili kushiriki utumishi.

Nikiongoza funzo la Biblia

Hata hivyo, maisha yangu hayategemei tu teknolojia. Kila siku, rafiki zangu wapendwa hunitembelea. Wao hunitembelea pamoja na ndugu zao wa ukoo na wale wanaopendezwa na ujumbe wa Biblia. Mara nyingi, wao huniomba niongoze mazungumzo ya Biblia pamoja na watu hao. Pindi nyingine, familia fulani hunitembelea na kunialika kushiriki katika ibada yao ya familia. Ninafurahi sana watoto wanapoketi kando ya kitanda changu na kuniambia kwa nini wanampenda Yehova.

Nikifurahia ibada ya familia pamoja na rafiki zangu

Ninashukuru sana ninapotembelewa na watu mbalimbali. Mara nyingi chumba changu hujaa wageni wanaotia ndani marafiki wanaokuja kunitembelea kutoka maeneo ya jirani na mbali. Kama unavyoweza kuwazia, upendo wa namna hii umewashangaza wafanyakazi wa kituo changu. Kila siku, ninamshukuru Yehova kwa kuniwezesha kuwa sehemu ya undugu wa aina hiyo.

PAMBANO LAENDELEA

Mtu yeyote anaponisalimu, mimi humjibu, “Nipo, ninaendelea kupambana!” Bila shaka, ninajua kwamba siko peke yangu katika shindano hilo. Iwe ni hali au udhaifu wetu, Wakristo wote wako katika pigano, yaani, “pigano zuri la imani.” (1 Timotheo 6:12) Ni nini ambacho kimenisaidia kupambana kwa miaka mingi? Ninasali kila siku na kumshukuru Yehova kwa kunipa kusudi la maisha. Ninajitahidi kuwa na mengi ya kufanya katika kumtumikia Mungu, huku nikikaza macho kwenye tumaini zuri lililo mbele.

José María

Mara nyingi mimi hufikiria jinsi ulimwengu mpya utakavyokuwa na jinsi itakavyokuwa nitakapoweza kukimbia na kuruka tena. Nyakati fulani, mimi humtania rafiki yangu, José María, anayeugua ugonjwa wa polio, kuhusu kukimbia pamoja mbio za masafa marefu. Nilimuuliza hivi: “Ni nani atakayeshinda?” Alinijibu hivi: “Jambo muhimu si yule atakayeshinda, jambo muhimu ni kuwa katika Paradiso ili kukimbia mbio hizo.”

Halikuwa jambo rahisi kwangu kukubaliana na udhaifu wangu. Ninajua kwamba nilipokuwa kijana nilifanya jambo la kipumbavu lililosababisha madhara makubwa. Hata hivyo, ninamshukuru sana Yehova kwamba hajaniacha. Amenipa vitu vingi, yaani, familia kubwa ya kiroho, tumaini la kuishi, shangwe ya kuwasaidia wengine, na tumaini zuri la wakati ujao. Ikiwa ningesema hisia zangu kwa sentensi moja tu, nadhani nitasema hivi: Yehova amenipa zaidi ya ninavyostahili.