Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 HABARI KUU | JE, SHETANI NI KIUMBE HALISI?

Je, Shetani Ni Alama tu ya Uovu?

Je, Shetani Ni Alama tu ya Uovu?

Ni rahisi kudhani kwamba Shetani tunayesoma kumhusu katika Biblia ni alama tu ya uovu. Lakini je, hivyo ndivyo Biblia inavyofundisha? Ikiwa ndivyo, kwa nini Biblia inamtaja Shetani akizungumza na Yesu Kristo na hata Mungu Mweza-Yote mwenyewe? Tuchunguze mifano miwili ya mazungumzo hayo.

SHETANI ALIPOZUNGUMZA NA YESU

Yesu alipoanza huduma yake, Shetani alimshawishi kwa mambo matatu. Kwanza, Shetani alijitahidi kumshawishi Yesu atumie vibaya nguvu alizopewa na Mungu ili kukabiliana na njaa yake. Kisha Ibilisi alitaka Yesu ahatarishe uhai wake na kujitafutia sifa. Mwishowe, Shetani alimwahidi Yesu kwamba angempa mamlaka juu ya falme zote za dunia ikiwa angetenda tendo dogo la ibada. Yesu alipinga vishawishi vyote hivyo, na kila mara alinukuu Maandiko.—Mathayo 4:1-11; Luka 4:1-13.

Yesu alikuwa akizungumza na nani? Je, alikuwa akizungumza na uovu uliokuwa ndani yake mwenyewe? Kulingana na Maandiko, Yesu “amejaribiwa katika mambo yote kama sisi wenyewe, lakini bila kuwa na dhambi.” (Waebrania 4:15) Biblia pia inasema: “Yeye hakufanya dhambi, wala udanganyifu haukupatikana kinywani mwake.” (1 Petro 2:22) Yesu aliendelea kuwa mkamilifu, na alidumisha utimilifu. Hakuruhusu uovu wowote usitawi ndani yake. Ni wazi kwamba Yesu hakuwa akizungumza na uovu wowote ulio ndani yake, badala yake alikuwa akizungumza na kiumbe halisi.

Mazungumzo hayo yanathibitisha zaidi kwamba Shetani ni kiumbe halisi.

  • Kumbuka kwamba Shetani aliahidi kumpa Yesu falme zote za dunia ikiwa angefanya tendo la ibada. (Mathayo 4:8, 9) Ahadi hiyo haingekuwa na maana yoyote kama hakuna Shetani. Zaidi ya hayo, Yesu hakupinga mamlaka ya Shetani.

  • Baada ya Yesu kupinga vishawishi hivyo, Ibilisi “akamwacha mpaka wakati mwingine unaofaa.” (Luka 4:13) Je, katika kisa hiki Shetani ni uovu tu, au ni adui mwenye nguvu?

  • Ona kwamba “malaika wakaja na kuanza kumhudumia.” (Mathayo 4:11) Je, malaika hao ni viumbe wa kiroho waliomfariji na kumsaidia Yesu? Bila shaka! Kama ndivyo, kwa nini tuseme kwamba Shetani ni uovu tu?

 SHETANI ALIPOZUNGUMZA NA MUNGU

Kisa hiki cha pili kinamhusu Ayubu, mtu aliyemwogopa Mungu. Simulizi hilo linataja pindi mbili ambazo Ibilisi alizungumza na Mungu. Katika pindi hizo mbili, Mungu alimsifu Ayubu kwa sababu ya utimilifu wake. Shetani alidai kwamba Ayubu alimtumikia Mungu kwa sababu za kichoyo, pia alisema Mungu alimpa mali Ayubu ili amtumikie. Ni kana kwamba Ibilisi alidai alimjua vizuri Ayubu kuliko Mungu alivyomjua. Yehova alimruhusu Shetani kuangamiza mali za Ayubu, kuua watoto wake, na hata kudhoofisha afya yake. * Baadaye, ilikuwa wazi kwamba Yehova alikuwa sahihi kumsifu Ayubu, na Shetani alithibitika kuwa mwongo. Mungu alimbariki Ayubu kwa sababu ya utimilifu wake.—Ayubu 1:6-12; 2:1-7.

Katika mazungumzo yake na Shetani, je, Yehova Mungu alikuwa akizungumza na uovu ulio ndani yake mwenyewe? Biblia inasema hivi: “Mungu wa kweli, njia yake ni kamilifu.” (2 Samweli 22:31) Pia, Neno la Mungu linasema hivi: “Mtakatifu, mtakatifu, mtakatifu ni Yehova Mungu, Mweza-Yote.” (Ufunuo 4:8) Utakatifu humaanisha kuwa safi, kutakata, kutokuwa na dhambi. Yehova ni mkamilifu na hana dhambi. Kwa hiyo hawezi kamwe kuwa na uovu ndani yake.

Baada ya kuzungumza na Mungu, Shetani alimsababishia Ayubu madhara halisi

Hata hivyo, wengine husema kwamba hata Ayubu hakuwa mtu halisi, kwa hiyo mazungumzo hayo yalikuwa hadithi tu. Lakini hivyo ndivyo ilivyo? Mistari mingine ya Biblia huthibitisha kwamba Ayubu alikuwa mtu halisi. Kwa mfano, kwenye andiko la Yakobo 5:7-11, tunaona kwamba Ayubu anatumika kama mfano wa kuwahimiza Wakristo kuvumilia hali ngumu na kuwapa faraja kwamba Yehova huwathawabisha wanaovumilia. Kisa cha Ayubu kingekuwa na umuhimu gani ikiwa Ayubu hakuwa mtu halisi na matatizo yaliyompata hayakutukia? Zaidi ya hayo, kwenye andiko la Ezekieli 14:14, 20, Ayubu anatajwa pamoja na Noa na Danieli katika orodha ya watu watatu waadilifu. Kama Noa na Danieli, Ayubu alikuwa mtu halisi, mwenye imani yenye nguvu. Ikiwa Ayubu alikuwa halisi, kwa nini Shetani ambaye alikuwa chanzo cha mateso ya Ayubu asiwe halisi?

Kwa kweli, Biblia inamtaja Shetani kuwa kiumbe halisi wa roho. Hata hivyo, huenda ukajiuliza, ‘Je, kweli Shetani anaweza kunidhuru mimi na familia yangu katika ulimwengu huu wa leo?’

NAMNA GANI WAKATI WETU?

Wazia ikiwa kundi la wahalifu lingevamia mji wenu. Bila shaka usalama ungepungua na maadili ya mji wenu yangeporomoka. Sasa fikiria hali inayofanana na hiyo: Shetani na roho wake waovu—viumbe wa roho ambao kama Shetani, walimwasi Mungu—wametupwa duniani. Kumekuwa na matokeo gani? Fikiria mambo unayoona kwenye taarifa za habari nchini kwenu na duniani pote.

  • Je, unaona kuongezeka kwa ujeuri licha ya jitihada za duniani pote za kuzuia hali hiyo?

  • Je, unaona kuongezeka kwa vitumbuizo vyenye mambo ya uchawi ingawa wazazi wengi wanavichukia?

  • Je, unaona uharibifu mkubwa wa mazingira, licha ya jitihada nyingi za kuzuia hali hiyo?

  • Je, inawezekana kuna tatizo kubwa katika jamii ya wanadamu—na kwamba kuna nguvu fulani inayowaongoza wanadamu kwenye majanga?

Tafadhali ona kile ambacho Biblia inasema kuhusu chanzo cha matatizo yetu: “Yule joka mkubwa akatupwa chini, yule nyoka wa zamani, yeye anayeitwa Ibilisi na Shetani, anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa; akatupwa chini duniani, na malaika zake wakatupwa chini pamoja naye. . . . Ole wa dunia na wa bahari, kwa sababu Ibilisi ameshuka kwenu, akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.” (Ufunuo 12:9, 12) Baada ya kuchunguza uthibitisho, watu wengi wanakubali kwamba Shetani ni kiumbe hatari, na ndiye anayeupotosha ulimwengu.

Huenda ukajiuliza jinsi unavyoweza kupata ulinzi. Ni vizuri kufanya hivyo. Makala inayofuata itatoa msaada unaofaa.

^ fu. 12 Yehova ni jina la Mungu kama linavyofunuliwa katika Biblia.