Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tuliumbwa Tuishi Milele

Tuliumbwa Tuishi Milele

NI NANI kati yetu asiyetamani kuishi maisha marefu yaliyojaa furaha? Wazia jinsi ambavyo maisha yangekuwa ikiwa tungeishi milele tukiwa na afya kamili na furaha! Tungekuwa na nafasi ya kutosha ya kushirikiana na wapendwa wetu, kutembelea sehemu mbalimbali duniani, kujifunza fani tofauti-tofauti, kuwa na hekima zaidi, na kujifunza kwa kina jambo lolote linalotuvutia mpaka tunapohisi tumeridhika.

Je, ni vibaya kutamani maisha kama hayo? La hasha! Maandiko yanatueleza kwamba Mungu ameweka tamaa hiyo ndani ya mioyo yetu. (Mhubiri 3:11) Vilevile, Maandiko yanasema “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Je, kweli Mungu mwenye upendo anaweza kutuumba tukiwa na tamaa ya kuishi milele na wakati huohuo aondoe kabisa uwezekano wa kukidhi tamaa hiyo?

Kwa kweli, hakuna anayependa kufa. Haishangazi kwamba Biblia inakiita kifo “adui.” (1 Wakorintho 15:26) Nyakati fulani kinawahi; nyakati nyingine kinakawia. Lakini lazima kije. Wazo la kifo huwanyima watu wengi amani, na hata linawaogopesha. Je, kuna siku ambayo adui huyu ataangamizwa? Je, inawezekana kweli?

MSINGI WA KUWA NA TUMAINI

Mungu hakukusudia wanadamu wafe! Je, jambo hilo linakushangaza? Kitabu cha Mwanzo katika Biblia kinatuthibitishia kwamba Mungu alikusudia wanadamu waishi milele duniani. Yehova Mungu aliiumba dunia kwa ustadi sana ili iwe makao yanayowafaa wanadamu. Kisha akamuumba Adamu, mwanadamu wa kwanza, na kumweka katika paradiso—bustani iliyokuwa eneo la Edeni. Baada ya hapo, “Mungu akaona kila kitu alichoumba, na tazama! kilikuwa chema sana.”—Mwanzo 1:26, 31.

Adamu aliumbwa akiwa mkamilifu, kwa mfano wa Mungu. (Kumbukumbu la Torati 32:4) Hawa, mke wa Adamu, aliumbwa pia bila kasoro yoyote katika akili na mwili wake. Yehova aliwaambia: “Zaeni, muwe wengi, muijaze dunia na kuitiisha, na mtawale samaki wa baharini na viumbe wanaoruka angani na kila kiumbe aliye hai anayetembea duniani.”—Mwanzo 1:28.

Ingechukua muda kuijaza dunia. Hawa angehitaji kuwa watoto, na watoto wake nao wapate watoto wengine mpaka wakati ambapo dunia nzima ingejaa watu kama Mungu alivyokusudia. (Isaya 45:18) Je, kweli Yehova angewapa tumaini hilo ikiwa alikusudia waishi muda ambao ungetosha tu kuwaona watoto wao na labda wajukuu na bila kujua maisha yangekuwaje wakati ujao?

Pia, fikiria jukumu walilopewa la kuwatiisha wanyama. Adamu aliambiwa awape majina wanyama wote, na bila shaka angetumia muda mrefu kumaliza kazi hiyo. (Mwanzo 2:19) Lakini ili kuwatiisha, Adamu angehitaji kujifunza kuhusu kila mnyama na kujua jinsi ya kuwatunza wanyama wote. Kazi hiyo ingehitaji muda mrefu zaidi.

Kwa hiyo, agizo la Mungu la kuijaza dunia na kuwatiisha wanyama, linaonyesha kwamba wenzi wa ndoa wa kwanza waliumbwa ili waishi kwa muda mrefu. Na kwa kweli, Adamu aliishi muda mrefu sana.

KUSUDI LA MUNGU NI KWAMBA WANADAMU WAISHI MILELE KATIKA PARADISO DUNIANI

WALIISHI MAISHA MAREFU SANA

Adamu, miaka 930

Methusela, miaka 969

Noa, miaka 950

Leo, miaka 70-80

Biblia inaonyesha kwamba kuna kipindi ambacho wanadamu waliishi kwa muda mrefu sana kuliko tunavyoishi leo. Inasema: “Siku zote za maisha ya Adamu zilikuwa miaka 930.” Kisha, inaorodhesha wanaume wengine sita walioishi zaidi ya miaka 900! Walikuwa Sethi, Enoshi, Kenani, Yaredi, Methusela, na Noa. Wote hao waliishi kabla ya Gharika ya siku za Noa, na Noa alikuwa ameishi kwa miaka 600 kabla ya Gharika. (Mwanzo 5:5-27; 7:6; 9:29) Iliwezekanaje kwao kuishi muda mrefu hivyo?

Wanaume wote hao waliishi karibu na kipindi ambacho wanadamu walikuwa wakamilifu. Inaelekea hicho ndicho kilifanya waishi muda mrefu hivyo. Lakini ukamilifu una uhusiano gani na kuishi maisha marefu? Na kifo kitaangamizwaje? Ili kupata majibu, tunahitaji kwanza kuelewa kwa nini tunazeeka na kufa.