Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 HABARI KUU

Unawezaje Kuwa Rafiki Mzuri?

Unawezaje Kuwa Rafiki Mzuri?

MNAMO Desemba 25, 2010, kabla ya kujiua mwanamke fulani mwenye umri wa miaka 42 aliandika ujumbe kwenye tovuti fulani ya kijamii. Ujumbe wake ulikuwa kilio cha kuomba msaada. Ingawa alikuwa na “marafiki” zaidi ya elfu moja kwenye mtandao, hakuna hata mmoja aliyemsaidia. Siku moja baadaye, polisi walimpata akiwa amekufa. Alijiua kwa kumeza dawa nyingi kupita kiasi.

Leo, kupitia teknolojia tunaweza kupata mamia, au hata maelfu ya “marafiki” kwenye mitandao ya kijamii kwa kuongeza tu majina yao kwenye orodha yetu ya anwani katika kompyuta. Pia, tukitaka kukatisha “urafiki” na yeyote kati yao, tunafuta tu jina lake kutoka kwenye orodha yetu. Hata hivyo, msiba uliotajwa mwanzoni kuhusu yule mwanamke huko Uingereza unakazia ukweli muhimu—watu wengi hawana marafiki wa kweli. Utafiti mmoja wa hivi karibuni unaonyesha kwamba ingawa watu wanawasiliana sana, idadi ya marafiki wa kweli imepungua.

Bila shaka, kama watu wengi unakubali kwamba ni muhimu kuwa na marafiki wa kweli. Huenda pia umetambua kwamba urafiki unahusisha mengi kuliko kuongeza majina kwenye orodha ya kompyuta au simu yako. Rafiki wa kweli anapaswa kuwa na sifa zipi? Unawezaje kuwa rafiki mzuri? Ni mambo gani yanayohitajika ili kupata marafiki wa kudumu?

Chunguza kanuni nne zifuatazo, na uone jinsi Biblia inavyotoa ushauri wenye busara utakaokusaidia kuwa na sifa za rafiki mzuri.

 1. Wajali Wengine Kikweli

Urafiki wa kweli unahusisha vitendo. Kwa maneno mengine, rafiki mzuri anajua majukumu yake, na ni mwenye kujali. Kwa kweli, urafiki unahusisha pande mbili, na kila mmoja anapaswa kutimiza sehemu yake. Lakini kuna faida za kufanya hivyo. Jiulize, ‘Je, niko tayari kujitolea kutumia muda na mali zangu kwa ajili ya rafiki yangu?’ Kumbuka, ili upate rafiki mzuri, wewe mwenyewe unapaswa kuwa rafiki mzuri.

WATU HUTAKA RAFIKI WA AINA GANI?

Irene: “Sawa tu na kutengeneza bustani maridadi, unahitaji kujitahidi ili kusitawisha urafiki. Anza kwa kuwa rafiki mzuri wewe mwenyewe. Jitahidi sana kuonyesha upendo na kupendezwa na wengine. Na uwe tayari kutumia muda wako inapohitajika.”

Luis Alfonso: “Watu wengi leo wana ubinafsi badala ya ukarimu. Basi, inapendeza sana mtu anapokuonyesha upendo bila kutazamia kwamba utamlipa chochote.”

BIBLIA INASEMA NINI?

“Kama vile mnavyotaka watu wawatendee ninyi, watendeeni wao vivyo hivyo. Muwe na mazoea ya kuwapa watu, na watu watawapa ninyi.” (Luka 6:31, 38) Kwenye andiko hilo Yesu anapendekeza ukarimu na kuwajali wengine. Ukarimu kama huo hutokeza urafiki wa kweli. Ukijitolea kuwasaidia rafiki zako bila kutarajia kulipwa, watapendezwa nawe.

2. Fahamu Jinsi ya Kuwasiliana

Urafiki wa kweli hauwezi kusitawi bila mawasiliano ya kawaida. Kwa hiyo, zungumzieni mambo yanayowapendeza. Msikilize rafiki yako, na uheshimu maoni yake. Ikiwezekana, mpongeze na umtie moyo. Nyakati nyingine, huenda rafiki akahitaji ushauri au hata kurekebishwa, na huenda isiwe rahisi kufanya hivyo. Hata hivyo, rafiki mshikamanifu anajua jinsi ya kumkosoa mwenzake na kutoa ushauri kwa busara.

WATU HUPENDA RAFIKI WA AINA GANI?

Juan: “Rafiki wa kweli anapaswa kujieleza kwa uhuru na asikasirike usipokubaliana na maoni yake.”

Eunice: “Mimi huwathamini sana marafiki ambao wako tayari kutumia muda pamoja nami na kunisikiliza, hasa ninapokuwa na matatizo.”

Silvina: “Marafiki wa kweli watakuambia ukweli—hata wakijua kwamba utaumia—kwa sababu wanakujali.”

BIBLIA INASEMA NINI?

“Kila mtu lazima awe mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa ghadhabu.” (Yakobo 1:19) Marafiki wa kweli hupenda kusikilizwa. Hata hivyo, kutawala mazungumzo kunaonyesha kwamba tunafikiri maoni yetu ni bora kuliko ya wengine. Kwa hiyo, sikiliza kwa makini rafiki anapokueleza maoni yake ya moyoni na mahangaiko yake. Pia, usikasirike akikuambia ukweli. Andiko la Methali 27:6, linasema: “Vidonda vinavyosababishwa na mpenzi ni vya uaminifu.”

 3. Usitazamie Mengi Mno

Kadiri tunavyozidi kuwa karibu na rafiki yetu ndivyo inavyokuwa rahisi kutambua makosa yake. Kama sisi, rafiki zetu si wakamilifu. Kwa hiyo, hatupaswi kutarajia ukamilifu kutoka kwa rafiki zetu. Badala yake, ni vizuri kupendezwa na sifa zao nzuri na kutokazia fikira makosa yao.

WATU HUPENDA RAFIKI WA AINA GANI?

Samuel: “Mara nyingi tunadai mengi kutoka kwa wengine kuliko yale tunayoweza kutimiza. Tukitambua makosa yetu na kwamba tunahitaji kusamehewa, itakuwa rahisi kuwasamehe wengine.”

Daniel: “Kubali kwamba rafiki zako watafanya makosa. Matatizo yanapotokea ni vizuri kuyatatua haraka na kujitahidi kuyasahau.”

BIBLIA INASEMA NINI?

Je uko tayari kusamehe?Wakolosai 3:13, 14

“Sisi sote hujikwaa mara nyingi. Ikiwa yeyote hajikwai katika neno, huyo ni mtu mkamilifu, anayeweza kuuongoza kwa lijamu mwili wake wote pia.” (Yakobo 3:2) Kutambua ukweli huo kutatusaidia kuwaelewa rafiki zetu. Hilo litafanya tupuuze kasoro ndogo na mambo yanayoweza kutuudhi. Biblia inasema hivi: “Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine. . . . Lakini, zaidi ya mambo haya yote, jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.”Wakolosai 3:13, 14.

 4. Uwe na Marafiki wa Aina Mbalimbali

Ni kweli kwamba tunahitaji kuchagua marafiki wetu kwa uangalifu. Lakini haimaanishi kwamba tunapaswa kuwa tu na marafiki wa umri fulani au malezi kama yetu. Kupendezwa na watu wa umri, malezi, na mataifa mbalimbali kunaweza kuboresha maisha yetu.

WATU HUPENDA RAFIKI WA AINA GANI?

Unai: “Kuwa na marafiki wa umri na mapendezi kama yetu, ni sawa na kuvaa nguo za rangi moja unayoipenda kila siku. Hata iwe unaipenda rangi hiyo kadiri gani, mwishowe itakuchosha.”

Funke: “Kuwa na marafiki wa aina mbalimbali kumenisaidia kuwa mtu mkomavu. Nimejifunza kuishi na watu wa umri na malezi mbalimbali, na hilo limenifanya niweze kushughulika na watu na hali tofauti-tofauti. Na rafiki zangu wanapendezwa na hilo.”

Je unapendezwa na watu wote bila kuwabagua?2 Wakorintho 6:13

BIBLIA INASEMA NINI?

“Kwa hiyo, yakiwa kama malipo—mimi nasema kana kwamba ni kwa watoto—ninyi, pia, panukeni.” (2 Wakorintho 6:13) Biblia inatuhimiza tuwe na marafiki wa aina mbalimbali. Kukubali maoni ya wengine na kutobagua watu kunaweza kuboresha maisha yako, na pia kufanya watu wapendezwe nawe.