Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | KULEA WATOTO

Jinsi ya Kumtia Nidhamu Kijana Wako

Jinsi ya Kumtia Nidhamu Kijana Wako

KIKWAZO

Kulingana na sheria ya familia yako, simu za mkononi zinapaswa kuzimwa saa tatu usiku, lakini mara mbili katika juma hili ulimkuta binti yako akituma ujumbe usiku wa manane. Au mwana wako anapaswa kurudi nyumbani saa nne usiku, lakini jana usiku—kwa mara nyingine tena—alirudi nyumbani baada ya saa tano usiku.

Ni kweli kwamba kijana wako amefanya kosa. Hata hivyo, kwanza unahitaji kujua ni kwa nini anavunja sheria zako. Hata hivyo, utapendezwa kujua kwamba ingawa jambo hilo linaweza kuonekana kuwa ukaidi, huenda isiwe hivyo.

KWA NINI JAMBO HILI HUTUKIA

Mipaka isiyo wazi. Vijana fulani hupuuza sheria ili waone kama watatiwa nidhamu. Kwa mfano, ikiwa mzazi amesema kwamba atamwadhibu kijana kama atafanya kosa fulani, huenda kijana akajaribu kukiuka mipaka iliyowekwa ili kuona ikiwa mzazi atamtia nidhamu. Je, hilo linamaanisha vijana hao wanakuwa waasi sugu? Si lazima iwe hivyo. Ukweli ni kwamba, ni rahisi kwa vijana kukosa kutii sheria ikiwa wazazi wanakuwa vigeugeu kuhusu nidhamu waliyosema watatoa, au ikiwa vijana hawajawekewa mipaka iliyo wazi.

Usiwe mkali sana. Wazazi fulani hujaribu kuwadhibiti vijana wao kwa kuwawekea sheria nyingi kupita kiasi. Kijana asipotii, mzazi anakasirika na kumwekea sheria nyingi hata zaidi. Hata hivyo, jambo hilo hufanya mambo yawe mabaya zaidi. Kitabu Parent/Teen Breakthrough kinasema hivi: “Kadiri unavyojaribu kumdhibiti kijana wako, ndivyo anavyozidi kuasi.” Kitabu hicho kinaongezea hivi: “Kujaribu kumdhibiti ni sawa na kujaribu kupaka siagi ngumu kwenye mkate laini: mkate huo utapasuka vipande-vipande, na suluhisho si kupaka siagi kwa nguvu.”

Nidhamu inayofaa inaweza kusaidia. Tofauti na “adhabu”—ambayo humaanisha kumtesa mtu—“nidhamu” humaanisha kufundisha. Kwa hiyo unawezaje kumfundisha kijana wako atii sheria zako?

 MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Eleza mambo waziwazi. Vijana wanahitaji kujua mambo hususa wanayotazamiwa kufanya na matokeo ya kutokutii.—Kanuni ya Biblia: Wagalatia 6:7.

Dokezo: Andika orodha ya sheria za nyumba yenu. Kisha jiulize: ‘Je, nimeweka sheria nyingi sana? Je, nimeweka sheria chache sana? Je, baadhi ya sheria hizo hazihitajiki tena? Je, ninahitaji kuzirekebisha kulingana na kiwango cha ukomavu wa kijana wangu?’

Usiwe kigeugeu. Huenda vijana wakachanganyikiwa ikiwa juma lililopita hawakutiwa nidhamu kwa kufanya kosa fulani, lakini juma hili wanatiwa nidhamu kwa kufanya kosa hilohilo.—Kanuni ya Biblia: Mathayo 5:37.

Dokezo: Jaribu kutoa nidhamu inayofaana kabisa na “kosa” lililofanywa. Kwa mfano, ikiwa kijana amechelewa kurudi nyumbani, nidhamu inayofaa inaweza kuwa kumwekea sheria ya kurudi nyumbani mapema zaidi ya saa uliyomwekea awali.

Uwe na usawaziko. Uwe mzazi mwenye kubadilika kulingana na hali kwa kumpa kijana wako uhuru zaidi kadiri anavyostahili.—Kanuni ya Biblia: Wafilipi 4:5.

Dokezo: Wewe na kijana wako zungumzieni pamoja sheria zilizowekwa. Hata unaweza kumwomba kijana wako apendekeze nidhamu anayopaswa kupewa kwa kuvunja sheria fulani. Ni rahisi zaidi kwa vijana kutii sheria ambazo wao wenyewe wameshiriki kuzitunga.

Msaidie akomae. Lengo lako si tu kumfanya kijana wako atii amri zako, bali ni kumsaidia akuze dhamiri njema—uwezo wa ndani wa kutambua mema na mabaya. (Ona sanduku “Msaidie Mtoto Wako Asitawishe Sifa Nzuri.”)—Kanuni ya Biblia: 1 Petro 3:16.

Dokezo: Tafuta msaada katika Biblia. Hicho ndicho chanzo bora kabisa cha “nidhamu ambayo humpa mtu ufahamu,” na hekima yake inaweza “kuwapa werevu wale wasio na uzoefu, kumpa kijana ujuzi na uwezo wa kufikiri.”—Methali 1:1-4.