Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

KUKABILIANA NA HUZUNI YA KUFIWA

Huzuni ya Kufiwa​—Jinsi ya Kukabiliana Nayo

Huzuni ya Kufiwa​—Jinsi ya Kukabiliana Nayo

Leo, kuna ushauri mwingi sana wa jinsi ya kukabiliana na huzuni ya kufiwa, na ushauri fulani unaweza kuwa na matokeo zaidi kwako kuliko mwingine. Huenda hiyo ni kwa sababu kila mtu huomboleza kwa njia tofauti, kama makala iliyopita ilivyosema. Ushauri unaomfaa mtu mmoja huenda usimfae mwingine.

Hata hivyo, kuna mapendekezo ya msingi ambayo yamewasaidia watu wengi. Wataalamu wengi huyarejelea, na yanapatana na kanuni zisizopitwa na wakati ambazo zimeandikwa katika Biblia, kitabu cha kale kilichojaa hekima.

1: KUBALI MSAADA WA FAMILIA NA MARAFIKI

  • Baadhi ya washauri wanasema kwamba kukubali msaada wa wengine ndiyo njia bora ya kukabiliana na huzuni ya kufiwa. Hata hivyo, nyakati nyingine huenda ukataka kuwa peke yako. Huenda hata ukawakasirikia wale wanaojaribu kukusaidia. Ni kawaida kuhisi hivyo.

  • Usihisi kwamba unapaswa kuwa na wengine nyakati zote, lakini pia usijitenge nao kupita kiasi. Isitoshe, huenda ukahitaji msaada wao baadaye. Kwa fadhili, wajulishe mambo unayohitaji wakati huo na yale usiyohitaji.

  • Ikitegemea mahitaji yako, amua utatumia kiasi gani cha muda ukiwa peke yako na kiasi gani ukiwa na wengine.

KANUNI: “Wawili ni afadhali kuliko mmoja . . . Kwa maana mmoja wao akianguka, mwenzake anaweza kumwinua.”—Mhubiri 4:9, 10.

2: KULA CHAKULA CHENYE LISHE NA UTENGE MUDA WA MAZOEZI

  • Chakula chenye lishe kitakuimarisha na kukupa nguvu unapopitia kipindi hicho cha huzuni. Jitahidi kula aina tofauti-tofauti za matunda, mboga za majani, na vyakula vyenye protini visivyo na mafuta mengi.

  • Kunywa maji mengi na vinywaji vingine vyenye virutubisho.

  • Ikiwa huna hamu ya chakula, kula kiasi kidogo kila baada ya muda mfupi. Unaweza pia kumuuliza daktari wako ikiwa inafaa utumie vidonge vinavyoongeza virutubisho mwilini. *

  • Mazoezi ya kutembea na ya aina nyingine yanaweza kupunguza hisia mbaya. Kufanya mazoezi kutakupatia nafasi ya kutafakari kuhusu pengo lililoachwa au kukusaidia kuondoa mawazo hayo akilini.

KANUNI: “Hakuna mtu anayeuchukia mwili wake, bali huulisha na kuutunza.”—Waefeso 5:29.

3: LALA VYA KUTOSHA

  • Kwa kawaida, kulala ni muhimu. Lakini usingizi ni muhimu hata zaidi kwa wale waliofiwa kwa sababu, huzuni ya kufiwa huongeza uchovu.

  • Epuka kutumia kwa wingi vinywaji vyenye kafeini au kileo kwa sababu vinaweza kufanya ukose usingizi.

KANUNI: “Ni afadhali konzi moja ya pumziko kuliko konzi mbili za kazi ngumu na kukimbiza upepo.”—Mhubiri 4:6.

4: UWE TAYARI KUBADILIKA

  • Kumbuka kwamba kila mtu hukabiliana na huzuni ya kufiwa kwa njia tofauti. Hivyo, jitahidi kujua njia inayokufaa wewe binafsi.

  • Baadhi ya watu huona kwamba wanapoeleza hisia zao kwa wengine wanahisi vizuri zaidi, lakini wengine hupendelea kutojieleza. Hata wataalamu wana maoni yanayotofautiana kuhusu umuhimu wa mtu kueleza hisia zake baada ya kufiwa. Ikiwa ungependa kueleza jinsi unavyohisi lakini unasita, unaweza kuanza kwa kufunua hatua kwa hatua hisia zako kwa rafiki yako wa karibu.

  • Baadhi ya watu wametambua kwamba kulia huwasaidia kupunguza huzuni waliyo nayo, ilhali wengine hufanikiwa kukabiliana na huzuni yao bila kulia sana.

KANUNI: “Moyo hujua uchungu wake wenyewe.”—Methali 14:10.

5: EPUKA MAZOEA YENYE MADHARA

  • Baadhi ya watu waliofiwa huamua kunywa pombe kupita kiasi au kutumia dawa za kulevya ili kupunguza uchungu. Njia hiyo ya “kutuliza mawazo” ni yenye madhara. Utulivu wowote unaopatikana kwa njia hiyo haudumu, badala yake, mazoea hayo huleta matatizo makubwa. Tuliza mawazo yako kwa kutumia mbinu zisizosababisha madhara.

KANUNI: “Acheni tujisafishe kila unajisi.”—2 Wakorintho 7:1.

6: JISHUGHULISHE NA MAMBO TOFAUTI

  • Watu wengi wametambua kwamba kujishughulisha na mambo yatakayohamisha akili zao na hivyo kufanya wasifikirie sana kuhusu kifo cha mpendwa wao, huwasaidia kupunguza huzuni waliyo nayo.

  • Unaweza kufanya hivyo kwa kuanzisha au kuimarisha urafiki na watu wengine, kujifunza ustadi mpya, au kufanya mambo mengine unayofurahia.

  • Kadiri muda unavyopita, utaona hali ikibadilika. Utagundua kwamba muda unaotumia kufikiria kifo cha mpendwa wako unazidi kupungua, ishara ya kwamba umeanza kurudia hali yako ya kawaida.

KANUNI: “Kuna wakati uliowekwa wa kila jambo, . . . wakati wa kulia na wakati wa kucheka; wakati wa kuomboleza kwa sauti na wakati wa kucheza dansi.”—Mhubiri 3:1, 4.

7: UWE NA RATIBA YA KILA SIKU

  • Rudia ratiba yako haraka iwezekanavyo.

  • Ukifuata ratiba hususa ya muda wa kulala, kufanya kazi, na mambo mengine, unaweza kuanza kurudia hali yako ya kawaida.

  • Kuwa na mambo mengi mazuri ya kufanya kutakusaidia kupunguza maumivu ya kihisia.

KANUNI: “Hataona kwa urahisi jinsi siku za maisha yake zinavyopita, kwa sababu Mungu wa kweli humshughulisha na shangwe ya moyo wake.”—Mhubiri 5:20.

8: SUBIRI MUDA UPITE KABLA YA KUFANYA MAAMUZI MAKUBWA

  • Watu wengi wanaofanya maamuzi makubwa muda mfupi baada ya kufiwa, hujutia maamuzi hayo baadaye.

  • Ikiwezekana, subiri muda upite kabla ya kuhama, kubadili kazi, au kutupa vitu vya mpendwa wako aliyekufa.

KANUNI: “Mipango ya wenye bidii hakika huleta mafanikio, lakini wote walio na haraka kwa hakika watakuwa maskini.”—Methali 21:5.

9: JIKUMBUSHE KUMHUSU MPENDWA WAKO

  • Watu wengi waliofiwa huhisi vizuri wanapofanya mambo yanayowasaidia kumkumbuka mpendwa wao aliyekufa.

  • Huenda kukusanya picha au vitu vinavyokukumbusha mambo fulani kuhusu mpendwa wako, au kuandika matukio yanayomhusu unayopenda kubaki nayo akilini, kukakupatia faraja.

  • Tunza vitu vinavyokukumbusha mambo mliyofurahia, na utakapohisi una nguvu, vipitie ili kujikumbusha kuhusu nyakati hizo.

KANUNI: “Kumbukeni siku za zamani.”—Kumbukumbu la Torati 32:7.

10: BADILI MAZINGIRA

  • Ikiwezekana, chukua likizo usafiri.

  • Ikiwa hali hazikuruhusu kuchukua likizo ndefu, unaweza kutumia siku moja au mbili kufanya mambo yanayokufurahisha, kama vile kutembelea maeneo yenye kuvutia au makumbusho.

  • Kubadili mazingira, hata kama ni kwa muda mfupi, kunaweza kukusaidia.

KANUNI: “Twendeni faraghani mahali pasipo na watu ili mpumzike kidogo.”—Marko 6:31.

11: WASAIDIE WENGINE

  • Kumbuka kwamba unapowasaidia wengine unahisi vizuri na hivyo kupunguza huzuni yako.

  • Unaweza kuanza kwa kuwasaidia watu ambao wameathiriwa na kifo cha mpendwa wako, kama vile marafiki au watu wa ukoo ambao huenda wakahitaji mtu wa kuwafariji.

  • Kuwasaidia na kuwafariji wengine kutakusaidia upate tena shangwe na kusudi.

KANUNI: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35.

12: CHANGANUA UPYA MAMBO UNAYOTANGULIZA

  • Kufiwa kunaweza kukusaidia kutambua mambo yaliyo muhimu zaidi maishani.

  • Tumia fursa hiyo kuchunguza jinsi unavyoishi.

  • Baada ya kujichunguza, fanya mabadiliko yanayohitajika.

KANUNI: “Ni afadhali kwenda katika nyumba yenye maombolezo kuliko kwenda katika nyumba yenye karamu, kwa sababu huo ndio mwisho wa kila mwanadamu, na walio hai wanapaswa kuweka moyoni jambo hilo.”—Mhubiri 7:2.

Kwa kweli, hakuna chochote kitakachoondoa kikamili uchungu ulio nao. Hata hivyo, watu wengi ambao wamefiwa wanakubali kwamba kutumia mapendekezo kama yaliyotajwa kwenye makala hii, kumewasaidia kupunguza huzuni yao. Bila shaka, kuna mambo mengine, zaidi ya yale yaliyotajwa, ambayo yanaweza kukusaidia. Lakini ikiwa utatumia baadhi ya mapendekezo haya, uchungu ulio nao utapungua kwa kiwango kinachoridhisha.

^ fu. 13 Gazeti la Amkeni! halipendekezi matibabu fulani hususa.