Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Kutoka 20:12—“Mheshimu Baba Yako na Mama Yako”

Kutoka 20:12—“Mheshimu Baba Yako na Mama Yako”

 “Mheshimu baba yako na mama yako ili uishi muda mrefu katika nchi ambayo mimi Yehova Mungu wako ninakupa.”—Kutoka 20:12, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Waheshimu baba yako na mama yako; siku zako zipate kuwa nyingi katika nchi upewayo na BWANA, Mungu wako.”—Kutoka 20:12, Union Version.

Maana ya Kutoka 20:12

 Mungu aliwaamuru Waisraeli wa kale wawaheshimu wazazi wao. Kwa kuongezea ahadi juu ya amri hiyo, alikuwa akiwapa sababu nyingine ya kuitii. Ingawa Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli, inayoitwa Sheria ya Musa, haitumiki leo, viwango vyake havijabadilika. Kanuni zinazofanyiza Sheria ya Mungu bado zinatumika na kwa sababu hiyo ni muhimu kwa Wakristo.—Wakolosai 3:20.

 Watoto—iwe ni vijana au wazee—wanawaheshimu wazazi wao kwa kuwatii. (Mambo ya Walawi 19:3; Methali 1:8) Hata watoto wanapokuwa na familia zao, bado wanaendelea kuwapenda na kuwasaidia wazazi wao. Kwa mfano, wanahakikisha kwamba wazazi wao wanatunzwa vizuri wanapozeeka, na hata wanawapa msaada wa kifedha inapohitajika.—Mathayo 15:4-6; 1 Timotheo 5:4, 8.

 Ona kwamba watoto Waisraeli walipaswa kuwaheshimu baba na mama zao, na hivyo kuonyesha kwamba wanatambua fungu muhimu ambalo mama anatimiza katika familia. (Methali 6:20; 19:26) Leo watoto wanapaswa kufanya vivyo hivyo.

 Amri ya kuwaheshimu wazazi ilikuwa na mipaka. Watoto Waisraeli hawakupaswa kuwatii wazazi, au mwanadamu mwingine yeyote, ikiwa kufanya hivyo kulimaanisha kutomtii Mungu. (Kumbukumbu la Torati 13:6-8) Vivyo hivyo leo, Wakristo ‘wanamtii Mungu kuwa mtawala badala ya wanadamu.’—Matendo 5:29.

 Katika Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli, aliahidi kwamba watoto ambao waliwaheshimu wazazi wangeishi “muda mrefu na kufanikiwa” katika nchi waliyopewa na Mungu. (Kumbukumbu la Torati 5:16) Hawangeadhibiwa kama watoto ambao walipuuza sheria ya Mungu na kuasi wazazi wao. (Kumbukumbu la Torati 21:18-21) Kanuni zinazotegemea sheria hizo hazijabadilika kwa sababu tu ya wakati kupita. (Waefeso 6:1-3) Iwe sisi ni vijana au wazee, tunawajibika mbele za Muumba wetu. Na kupatana na ahadi yake, watoto wanaomtii na kuwatii wazazi wao watakuwa na maisha marefu. Kwa kweli, watakuwa na tumaini la kuishi milele.—1 Timotheo 4:8; 6:18, 19.

Muktadha wa Kutoka 20:12

 Amri iliyo kwenye Kutoka 20:12 imewekwa sehemu muhimu katika mpangilio wa zile Amri Kumi. (Kutoka 20:1-17) Amri zinazoitangulia zilieleza wajibu wa Waisraeli mbele za Mungu, kama vile umuhimu wa kumwabudu yeye peke yake. Amri zilizofuata zilieleza wajibu wao kwa wanadamu wenzao, kutia ndani amri ya kuwa mwaminifu kwa mwenzi wa ndoa na kutoiba. Hivyo, amri inayosema “mheshimu baba yako na mama yako” imeonwa kuwa daraja linalofaa kati ya sehemu hizo mbili za amri hizo.

Soma Kutoka sura ya 20 pamoja na maelezo ya chini, marejeo ya pambizoni, na picha.