Hamia kwenye habari

Mbingu Ni Nini?

Mbingu Ni Nini?

Jibu la Biblia

 Katika Biblia, neno “mbingu” linatumiwa kumaanisha mambo matatu: (1) mbingu halisi; (2) makao ya kiroho; na (3) cheo kilichokwezwa au kutukuka. Katika kila kisa, muktadha unatusaidia kutambua ni maana gani iliyokusudiwa. a

  1.   Mbingu halisi. Katika kisa hiki, “mbingu” zinawakilisha angahewa, mahali ambapo upepo unavuma, ndege wanaruka, mawingu yanatokeza mvua na theluji, na umeme. (Zaburi 78:26; Methali 30:19; Isaya 55:10; Luka 17:24) Inaweza pia kumaanisha anga za juu, mahali ambapo kuna “jua na mwezi na nyota.”​—Kumbukumbu la Torati 4:19; Mwanzo 1:1.

  2.   Makao ya kiroho. Neno “mbingu” pia linawakilisha mbingu za kiroho, au makao ya kiroho, eneo ambalo liko juu zaidi na nje ya ulimwengu halisi wa kimwili. (1 Wafalme 8:​27; Yohana 6:​38) Mbingu hizo za kiroho ni makao ya Yehova Mungu, ambaye ni “Roho.” Pia ni makao ya malaika ambao ni viumbe wa roho walioumbwa na Mungu. (Yohana 4:​24; Mathayo 24:36) Nyakati nyingine, “mbingu” hurejelewa kama viumbe hai kuwakilisha malaika waaminifu, “kutaniko la watakatifu.”​—Zaburi 89:5-7.

     Biblia pia inatumia neno “mbingu” kurejelea hasa sehemu fulani ya makao ya kiroho ambapo Yehova mwenyewe anakaa, “makao yake.” (1 Wafalme 8:​43, 49; Waebrania 9:​24; Ufunuo 13:6) Kwa mfano, Biblia ilitabiri kwamba Shetani na malaika waovu wangetupwa kutoka mbinguni, na hawangeruhusiwa tena kuingia mbele ya Yehova. Hata hivyo, bado wangeendelea kuwa katika makao ya kiroho.​—Ufunuo 12:​7-9, 12.

  3.   Cheo kilichokwezwa au kutukuka. Maandiko yanatumia neno “mbingu” kuwakilisha cheo kilichokwezwa, hasa kuhusiana na mamlaka ya kutawala. Mamlaka hiyo ni kama ile ya:

Mbinguni kukoje?

 Makao ya kiroho yana utendaji mwingi sana. Yana mamia ya mamilioni ya viumbe wa roho ‘wanaolitenda neno lake Yehova.’​—Zaburi 103:20, 21; Danieli 7:​10.

 Biblia inafafanua mbinguni kuwa mahali palipo na nuru nyingi sana. (1 Timotheo 6:​15, 16) Nabii Ezekieli alipokea maono ya kimbingu yaliyokuwa na “mwangaza” uliong’aa sana, naye Danieli aliona maono ya mbinguni yaliyokuwa na “mto wa moto.” (Ezekieli 1:26-28; Danieli 7:9, 10) Mbinguni ni mahali patakatifu, au safi, na maridadi.​—Zaburi 96:6; Isaya 63:15; Ufunuo 4:​2, 3.

 Mandhari inayofafanuliwa katika Biblia kuhusu mbinguni ni yenye kustaajabisha. (Ezekieli 43:​2, 3) Hata hivyo, haiwezekani kwa wanadamu kuelewa jinsi mbinguni kulivyo kikamili, kwa kuwa hisi zetu hazina uwezo wa kuelewa kabisa makao ya kiroho yalivyo.

a Inaonekana kwamba neno la Kiebrania linalotafsiriwa “mbingu” linatokana na shina la neno linalomaanisha “iliyokwezwa,” au “iliyoinuliwa.” (Methali 25:3) Ona kitabu The New Brown, Driver, and Briggs Hebrew and English Lexicon of the Old Testament, ukurasa wa 1029.

b Kitabu McClintock and Strong’s Cyclopedia kinasema kwamba mbingu mpya za Isaya 65:17 zinawakilisha “serikali mpya, ufalme mpya.”​—Buku la 4, ukurasa wa 122.