Hamia kwenye habari

Yule Malaika Mkuu Mikaeli Ni Nani?

Yule Malaika Mkuu Mikaeli Ni Nani?

Jibu la Biblia

 Mikaeli, anayetajwa katika dini fulani kuwa “Mtakatifu Mikaeli,” ni jina ambalo Yesu alipewa kabla na baada ya kuishi duniani. a Mikaeli alibishana na Shetani baada ya Musa kufa na pia alimsaidia malaika kumfikishia nabii Danieli ujumbe wa Mungu. (Danieli 10:13, 21; Yuda 9) Mikaeli anatenda kupatana na maana ya jina lake​—“Ni Nani Aliye Kama Mungu?”​—kwa kutetea utawala wa Mungu na kupigana na maadui wa Mungu.​—Danieli 12:1; Ufunuo 12:7.

 Fikiria kwa nini inapatana na akili kufikia mkataa kwamba Yesu ndiye malaika mkuu, Mikaeli.

  •   Mikaeli ndiye “yule malaika mkuu.” (Yuda 9) Jina la cheo “malaika mkuu,” linapatikana katika mistari miwili tu katika Biblia. Katika pindi zote, neno hilo linaandikwa kwa umoja, kuonyesha kwamba kuna malaika mmoja tu mkuu aliye na jina hilo la cheo. Mstari mmoja unaonyesha kwamba Bwana Yesu aliyefufuliwa “atashuka kutoka mbinguni akiwa na mwito wenye amri, kwa sauti ya malaika mkuu.” (1 Wathesalonike 4:16) Yesu ana “sauti ya malaika mkuu” kwa kuwa yeye ndiye malaika mkuu, Mikaeli.

  •   Mikaeli anaongoza jeshi la malaika. “Mikaeli na malaika zake wakapigana na yule joka mkubwa,” Shetani. (Ufunuo 12:7) Mikaeli ana mamlaka kuu katika ulimwengu wa roho, kwa kuwa anaitwa “mmoja wa hao wakuu wa mbele” na “yule mkuu.” (Danieli 10:13, 21; 12:1) Majina hayo ya cheo yanaonyesha kwamba Mikaeli ndiye “amiri-jeshi mkuu wa jeshi la malaika,” kama msomi wa Agano Jipya, David E. Aune anavyomwita.

     Biblia inataja jina moja tu lingine la mtu aliye na mamlaka juu ya jeshi la malaika. Inasema kuhusu “ufunuo wa Bwana Yesu kutoka mbinguni pamoja na malaika zake wenye nguvu katika mwali wa moto, anapoleta kisasi.” (2 Wathesalonike 1:7, 8; Mathayo 16:27) Yesu “alienda zake mbinguni; na malaika na mamlaka na nguvu vilitiishwa kwake.” (1 Petro 3:21, 22) Haipatani na akili kwa Mungu kumfanya Yesu awe kiongozi wa malaika na wakati uleule Mikaeli awe kiongozi wa malaika kana kwamba wao ni wapinzani. Badala yake, inapatana na akili kufikia mkataa kwamba majina yote mawili, Yesu na Mikaeli, ni ya mtu yuleyule.

  •   Mikaeli “atasimama” katika “wakati wa taabu” kubwa sana. (Danieli 12:1) Katika kitabu cha Danieli, neno “simama” mara nyingi linatumiwa kurejelea mfalme anayeinuka ili kuchukua hatua ya pekee. (Danieli 11:​2-4, 21) Yesu Kristo, anayetambulishwa kuwa “Mwana wa Mungu,” atachukua hatua ya pekee akiwa “Mfalme wa wafalme” ili kuwaangamiza maadui wote wa Mungu na kuwalinda watu wa Mungu. (Ufunuo 19:11-​16) Atafanya hivyo wakati wa kipindi cha “dhiki kuu ya namna ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, hapana, wala haitatukia tena.”​—Mathayo 24:21, 42.

a Biblia inawataja watu wengine waliokuwa na zaidi ya jina moja, kutia ndani Yakobo (anayeitwa pia Israeli), Petro (anayeitwa pia Simoni), na Thadayo (anayeitwa pia Yuda).​—Mwanzo 49:1, 2; Mathayo 10:2, 3; Marko 3:18; Matendo 1:13.