Hamia kwenye habari

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | KULEA WATOTO

Wafundishe Watoto Wako Kuonyesha Shukrani

Wafundishe Watoto Wako Kuonyesha Shukrani

 Utafiti unaonyesha kwamba watu wenye shukrani wana furaha zaidi, wana afya nzuri zaidi, wana uwezo mkubwa zaidi wa kukabiliana na matatizo, na wanakuwa na marafiki wa kudumu. Mtafiti Robert A. Emmons anasema kwamba kuwa na shukrani “kunamlinda mtu dhidi ya mambo yenye kudhuru kama vile wivu, chuki, pupa, na kufunga kinyongo.” a

 Watoto wananufaikaje wanapokuwa na shukrani? Vijana 700 hivi walipofanyiwa uchunguzi ulioendelea kwa miaka 4, ilionekana kwamba kulikuwa na uwezekano mdogo zaidi wa wale waliokuwa na mtazamo wa kuonyesha shukrani kuiba mtihani, kutumia dawa za kulevya na kileo, au kuwa na tabia mbaya.

  •   Watoto wanaoamini lazima wapewe vitu wanakosa shukrani. Watoto wengi wanafikiri kwamba vitu vizuri wanavyopewa ni haki yao. Mtoto anapokuwa na mtazamo kwamba mambo mazuri anayopata ni msharaha wake, badala ya kuyaona kuwa zawadi, hawezi kuwa na shukrani.

     Mtazamo huo umeenea sana leo. Mama fulani anayeitwa Katherine anasema hivi: “Ulimwengu wetu unawafundisha watu kuhisi kwamba wanastahili kila kitu. Vyombo vya habari hutuonyesha picha nyingi, kisha vinatuambia eti ‘tunastahili’ kupata vitu hivyo na kwamba tunapaswa kuwa wa kwanza kuvipata.”

  •   Watoto wanaweza kufundishwa kuwa na shukrani wanapokuwa wadogo. Mama mmoja anayeitwa Kaye anasema hivi: “Watoto wanaweza kufundishika. Kuwafundisha mazoea mazuri wanapokuwa wadogo ni sawa na kutumia matawi kushikilia mmea ili ukue ukiwa wima.”

Jinsi ya kuwafundisha kuwa na shukrani

  •   Wafundishe maneno ya kusema. Hata watoto wadogo wanaweza kujifunza kusema asante mtu anapowapa zawadi au kuwaonyesha fadhili. Kadiri wanavyokua na kukomaa, hatua kwa hatua watathamini zaidi ukarimu wa wengine.

     Kanuni ya Biblia: “Mjionyeshe kuwa wenye shukrani.”—Wakolosai 3:15.

     “Mjukuu wetu mwenye umri wa miaka 3 husema ‘asante’ kila wakati, naye husema ‘tafadhali’ anapoomba kitu. Alijifunza kutoka kwa wazazi wake. Tabia yao na jinsi wanavyotoa shukrani kumemfundisha jinsi ya kuwa mwenye shukrani.”—Jeffrey.

  •   Wafundishe matendo yanayofaa. Kwa nini usiwafundishe watoto wako kuandika kadi ya shukrani, wanapopewa zawadi na mtu fulani? Pia, ukiwagawia watoto wako kazi za nyumbani, utawasaidia kuelewa kazi nyingi inayofanywa ili kutunza familia.

     Kanuni ya Biblia: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35.

     Matineja wetu wawili wanaisaidia familia kwa kupanga milo, kupika na kufanya kazi nyingine za nyumbani. Hilo linawasaidia kuelewa kazi nyingi ambayo sisi wazazi tunafanya na hivyo wanakuwa na shukrani zaidi wanapofanyiwa mambo hayo.”—Beverly.

  •   Wafundishe mtazamo unaofaa. Kutoa shukrani kunaweza kulinganishwa na mmea unaonawiri katika udongo mzuri. Udongo huo unaweza kulinganishwa na unyenyekevu. Watu wanyenyekevu wanatambua kwamba wanahitaji msaada ili wafaulu katika jambo lolote, na hilo hufanya wawashukuru wengine kwa msaada wowote wanaopata.

     Kanuni ya Biblia: “Kwa unyenyekevu mwaone wengine kuwa bora kuliko ninyi, huku mkiangalia, si faida zenu wenyewe, bali pia faida za wengine.”—Wafilipi 2:3, 4.

     “Mara kwa mara tunacheza ‘mchezo wa kuonyesha shukrani’ wakati wa mlo. Kila mtu husimulia jambo ambalo linamfanya awe na shukrani. Hilo linawachochea watu kuwa na mawazo yanayofaa, yenye shukrani, badala ya mawazo yasiyofaa, ya ubinafsi.”—Tamara.

 Dokezo: Weka mfano. Watoto watajifunza kuwa na shukrani wakikusikia wewe ukiwashukuru wengine na wao pia kwa ukawaida.

a Nukuu limetolewa kwenye kitabu Thanks! How Practicing Gratitude Can Make You Happier.