Hamia kwenye habari

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | NDOA

Ponografia Inaweza Kuiharibu Ndoa Yako

Ponografia Inaweza Kuiharibu Ndoa Yako

 Siri ilifichuka, mke wake aligundua kwamba ana tabia hiyo. Mume huyo alimsihi mke wake amsamehe. Alimwahidi kwamba ataacha zoea hilo, na aliacha—kwa muda. Hata hivyo alirudia, na mzunguko huo wa kugunduliwa na kuomba msamaha ukaanza tena.

 Je, unakabili hali kama hiyo? Ikiwa ndivyo, ni muhimu utambue jinsi zoea lako la kutazama ponografia linavyomuumiza mwenzi wako na pia ujue jinsi unavyoweza kuacha kabisa zoea hilo. a

Katika makala hii

 Unachopaswa kujua

 Ponografia inaweza kuharibu kabisa ndoa. Inaweza kumfanya mwenzi asiye na hatia awe na kinyongo na aache kumwamini mwenzi wake. b

 Ikiwa mume anatazama ponografia, huenda mke wake akahisi:

  •   Amesalitiwa. Mke anayeitwa Sarah, anasema, “Nilihisi kana kwamba mume wangu amefanya uzinzi tena na tena.”

  •   Hafai. Mke mmoja anasema kwamba zoea la mume wake la kutazama ponografia lilimfanya ahisi kwamba “havutii na kwamba amefedheshwa.”

  •   Hawezi tena kumwamini mwenzi wake. Mke anayeitwa Helen, anasema, “Ninatilia shaka kila jambo ambalo mume wangu anafanya.”

  •   Wasiwasi. Mke anayeitwa Catherine, anakiri, “Kila wakati, nilifikiria tu kuhusu zoea la mume wangu.”

 Jambo la kufikiria: Biblia inasema kwamba mume anapaswa kumpenda mke wake. (Waefeso 5:25) Je, kweli anampenda mke wake ikiwa anamfanya awe na hisia ambazo zimetajwa hapo juu?

 Unachoweza kufanya

 Si rahisi kuacha zoea la kutazama ponografia. Mke mmoja anayeitwa Stacey, anasema, “Mume wangu aliacha sigara, bangi, na pombe, lakini bado anapambana na kuacha zoea la kutazama ponografia.”

 Ikiwa uko katika hali kama hiyo, madokezo yafuatayo yanaweza kukusaidia kuacha kabisa zoea hilo.

  •   Elewa madhara ya ponografia. Ponografia humchochea mtu kutenda kwa ubinafsi ili atosheleze tamaa zake mwenyewe na hilo hudhoofisha upendo, uaminifu, na ushikamanifu, sifa zinazohitajika ili kuwa na ndoa yenye furaha. Isitoshe, kutazama ponografia kunamvunjia heshima Mwanzilishi wa ndoa, Yehova Mungu.

     Kanuni ya Biblia: “Ndoa na iheshimiwe kati ya wote.”​—Waebrania 13:4.

  •   Usiwalaumu wengine kwa sababu ya mambo unayofanya. Usiseme, ‘Nisingehitaji kutazama ponografia ikiwa mke wangu angenionyesha upendo zaidi.’ Si haki kumlaumu mke wako na kufanya hivyo kunakupa tu kisingizio cha kutazama tena ponografia mke wako asipokuridhisha.

     Kanuni ya Biblia: “Kila mtu hujaribiwa kwa kuvutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe.”​—Yakobo 1:14.

  •   Uwe mnyoofu na umweleze mwenzi wako mambo waziwazi. Mume anayeitwa Kevin, anasema: “Mimi huzungumza na mke wangu kila siku. Ninamweleza nilichofanya siku hiyo nilipokabili kishawishi cha kutazama kitu kisichofaa, ikiwa nilijidhibiti au niliendelea kutazama. Ninapomweleza mambo waziwazi, yeye hahisi kwamba ninamficha chochote.”

     Kanuni ya Biblia: “Tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.”​—Waebrania 13:18.

  •   Uwe macho. Mtu anaweza kurudia zoea hilo hata baada ya miaka mingi ingawa huenda akahisi kwamba tayari ameshinda zoea hilo. Kevin, aliyetajwa hapo juu anasema: “Sikutazama ponografia kwa miaka kumi basi nilikuwa na uhakika kwamba tatizo langu lilikuwa limekwisha. Lakini uraibu huo ulikuwa umezama tu, ukisubiri hali ambazo zingeuruhusu uibuke tena.”

     Kanuni ya Biblia: “Yule anayefikiri amesimama na ajihadhari asije akaanguka.”​—1 Wakorintho 10:12.

  •   Unaposhawishiwa, tua kidogo. Ingawa huenda usiweze kuzuia tamaa mbaya, unaweza kuchagua ikiwa utatenda kupatana na tamaa hiyo au la. Tamaa hiyo itapita—na huenda ikapita haraka zaidi ukijifunza kugeuza au kubadili fikira zako na kuanza kufikiria mambo mengine, tamaa hiyo inapokuja.

     Kanuni ya Biblia: “Kila mmoja wenu anapaswa kujua jinsi ya kuudhibiti mwili wake mwenyewe katika utakatifu na heshima, si kwa hamu yenye pupa ya ngono.”​—1 Wathesalonike 4:4, 5.

  •   Epuka hali ambazo zinaweza kukufanya urudie zoea hilo. Kitabu, Willpower’s Not Enough, kinasema hivi: “Unapokuwa katika hali hatari, ni kana kwamba umewasha kiberiti. Unachohitaji tu ni mafuta kidogo. . . ya kuwasha moto wenyewe.”

     Kanuni ya Biblia: “Jambo lolote ovu lisinitawale.”​—Zaburi 119:133.

  •   Usikate tamaa. Inaweza kuchukua muda mrefu—hata miaka—kumfanya mwenzi wako akutumaini tena. Hata hivyo, inawezekana kwa sababu wenzi wengi wa ndoa wamefaulu.

     Kanuni ya Biblia: “Upendo ni wenye subira.”​—1 Wakorintho 13:4.

a Ingawa makala hii imeelekezwa kwa waume, kanuni ambazo zimezungumziwa zinaweza pia kuwasaidia wake wanaotazama ponografia.

b Baadhi ya wenzi wa ndoa wanadai kwamba kutazama ponografia pamoja kunaweza kuboresha uhusiano wao. Hata hivyo, kufanya hivyo hakupatani na kanuni za Biblia.​—Methali 5:15-20; 1 Wakorintho 13:4, 5; Wagalatia 5:22, 23.