Hamia kwenye habari

Kushoto: Baadhi ya machapisho yaliyotafsiriwa katika Kipapiamento tangu mwaka wa 1948. Kulia: Majengo maridadi ya Willemstad yaliyo Kurasao, moja kati ya visiwa ambako Kipapiamento kinazungumzwa

DESEMBA 11, 2023
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Miaka Sabini na Tano ya Kutafsiri Kweli za Biblia Katika Lugha ya Kipapiamento

Miaka Sabini na Tano ya Kutafsiri Kweli za Biblia Katika Lugha ya Kipapiamento

Kufikia 2023, Mashahidi wa Yehova wametimiza miaka 75 tangu walipoanza kutafsiri machapisho katika Kipapiamento. Kipapiamento ni lugha ya Krioli inayotokana na lugha za Kiholanzi, Kireno, na Kihispania. Leo, watu 350,000 hivi wanaoishi katika visiwa vya Aruba, Bonaire, na Kurasao vinavyojulikana kama visiwa ABC wanazungumza Kipapiamento.

Kazi ya kuhubiri ilianza katika visiwa hivi mwishoni mwa miaka ya 1920. Kufikia mwaka wa 1946, wamishonari waliohitimu Gileadi walienda Kurasao, tayari kulikuwa na makutaniko kadhaa katika kisiwa hicho. Hata hivyo, hakukuwa na machapisho yaliyotafsiriwa katika Kipapiamento. Mikutano ya kutaniko ilifanywa katika Kiingereza na Kipapiamento kwa kutumia machapisho ya Kiholanzi, Kiingereza, na Kihispania. Ingawa akina ndugu walitambua uhitaji wa kuwa na machapisho yanayotegemea Biblia katika Kipapiamento, kulikuwa na changamoto kadhaa. Kwa mfano, hakukuwa na kamusi za Kipapiamento na hakukuwa na viwango vya uandishi na kwa ajili ya sarufi. Ndugu Bill Yeatts alikuwa mmoja kati ya wamishonari wa kwanza kupewa mgawo katika visiwa hivyo, na alisaidia pia kazi ya kutafsiri. Kwenye 2002 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova alisema hivi: “Tulipotangaza habari za Ufalme, tulihitaji kuandika au kusema mambo ambayo hayajawahi kuandikwa au kusemwa katika Kipapiamento. Haikuwa kazi rahisi kuweka viwango ambavyo tungetumia.” Licha ya changamoto hizi akina ndugu waliendelea na kazi ya kutafsiri.

Chapisho la kwanza kutafsiriwa katika Kipapiamento lilikuwa kijitabu The Joy of All the People, ambacho kilikamilika katika mwaka wa 1948. Baadaye, machapisho mengi zaidi yalitafsiriwa, kutia ndani gazeti la Mnara wa Mlinzi na gazeti la Amkeni! Vitabu vya Biblia ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya vinaendelea kutolewa katika Kipapiamento kadiri vinavyokuwa vimetafsiriwa. Kitabu cha kwanza kutafsiriwa kilikuwa kitabu cha Ruthu ambacho kilitolewa Oktoba 1, 2021.

Akina dada wakishiriki mahubiri ya umma kwenye kisiwa cha Aruba

Matokeo ya jitihada hizi yanaonekana wazi kutokana na ongezeko kubwa la wahubiri katika visiwa hivi. Mwaka 1956, kutaniko la kwanza la Kipapiamento lilianzishwa na kulikuwa na wahubiri 16. Leo, zaidi ya wahubiri 1,600 wanatoa ibada kwa pamoja katika makutaniko 25 ya Kipapiamento. Na zaidi ya mafunzo 1,200 ya Biblia yaliongozwa katika mwaka wa 2023.

Tuna uhakika kwamba Yehova ataendelea kubariki jitihada za ndugu na dada wanaohubiri katika Kipapiamento kadiri wanavyoacha nuru yao iangaze na kumletea utukufu Yehova.​—Mathayo 5:16.