Hamia kwenye habari

Shule ya mapainia iliyofanyiwa kwenye Jumba la Ufalme katika mji wa Sambir (juu) na shule nyingi iliyofanyiwa kwenye chumba cha chini ya ardhi huko Zhytomyr (chini)

FEBRUARI 1, 2023
UKRAINIA

RIPOTI YA 16 | Upendo wa Kindugu Unaendelea Kuonyeshwa Licha ya Mashambulizi Nchini Ukrainia

Shule za Utumishi wa Painia Zaanza Tena

RIPOTI YA 16 | Upendo wa Kindugu Unaendelea Kuonyeshwa Licha ya Mashambulizi Nchini Ukrainia

Kuanzia Desemba 26, 2022, mapainia wa pekee na mapainia wa kawaida wamefaulu kuhudhuria Shule ya Utumishi wa Painia katika maeneo salama. Ikitegemea hali za eneo ambalo wamo, mapainia fulani wanahudhuria uso kwa uso na wengine kupitia Zoom. Licha ya changamoto kama vile makombora yanayoangushwa na ndege, kupotea kwa umeme, matatizo ya kiuchumi, na matatizo ya Intaneti, ndugu na dada zetu wamefanya kila wawezacho ili kuhudhuria shule hizo na kupata elimu hiyo ya pekee. Wamepata baraka nyingi za kiroho.

Kikundi cha akina dada wanaohudhuria shule ya mapainia kupitia Zoom katika kipindi ambacho umeme umekatwa. Wanatumia vifaa kadhaa vya kielektroni kwa kutumia betri

Natalia kutoka Kryvyi Rih anasema: “Shule hiyo imeniokoa kama boya linavyofanya. Imenisaidia nisizame katika bahari ya wasiwasi na woga.” Naye Anastasia kutoka Chernivtsi anasema: “Shule hiyo ilinihakikishia kwamba Yehova ananipenda sana. Mwaka uliopita ulikuwa umejaa matukio mabaya sana, lakini shule hii ilinifariji sana. Imenichochea kuendelea kufanya yote ninayoweza ili nipate baraka za Yehova.”

Svitlana, painia kutoka Kitsman, alikuwa na wasiwasi mwingi kuhusu kuhudhuria shule alipopokea mwaliko. Anasema: “Nilimweleza Yehova kuhusu mahangaiko yangu kutia ndani mahangaiko ya kiuchumi. Nilimtumaini na sijajutia. Nilihisi Yehova ananipenda na ananijali.” Jitihada za Svitlana zimemchochea mume wake ambaye si Shahidi wa Yehova, kuanza kuhudhuria mikutano pamoja naye.

Victoria anapokabili matatizo ya Intaneti, anaenda kwenye kituo cha treni kilicho karibu ambapo mtandao unapatikana ili ajiunge tena na shule ya mapainia

Pindi mbili, wanafunzi walio Zhytomyr walilazimika kujificha kwenye chumba cha chini ya ardhi kwa sababu ya milio ya ving’ora vilivyokuwa vikiwatahadharisha kuhusu makombora yanayoangushwa na ndege. Hata ingawa walikuwa wanatumia jiko maalum la kuni ili kupasha joto chumba, waliendelea na darasa lao. Licha ya changamoto hizo, Valentyna, ambaye alihamia Zhytomyr hivi karibuni, anasema: “Sitawahi kusahau shule hii. Nilihisi kana kwamba niko chini ya mabawa ya Yehova yenye nguvu.”

Kama ilivyokuwa katika nchi nyingi, mapainia nchini Ukrainia walifurahi sana waliposikia kuhusu punguzo la takwa la saa. Yulia aliposikia tangazo hilo alisema: “Ninahisi moyo wangu umejaa upendo kwa Yehova. Asubuhi ya leo nilimwomba Yehova anisaidie niweze kuendelea na utumishi huu. Sikujua jinsi ambavyo angejibu sala yangu, lakini nilijua kwamba atajibu. Niliposikia kwamba takwa la saa limepunguzwa, nilithamini hata zaidi yote ambayo Yehova ananifanyia. Habari hizo zilikuwa kitinda-mlo kizuri sana baada ya shule.”

Kufikia Januari 24, 2023, hizi ndizo takwimu zilizotufikia kutoka Ukrainia. Takwimu hizo zinategemea ripoti za uhakika tulizopata kutoka kwa ndugu walio katika maeneo hayo. Hata hivyo, huenda idadi halisi ikawa kubwa zaidi kwa sababu ni vigumu kudumisha mawasiliano mazuri katika maeneo yote nchini.

Athari Ambazo Ndugu na Dada Zetu Wamepata

  • Wahubiri 47 wamekufa

  • Wahubiri 97 wamejeruhiwa

  • Wahubiri 8,953 wamelazimika kuacha makao yao

  • Nyumba 590 zimeharibiwa kabisa

  • Nyumba 645 zimepata uharibifu mkubwa

  • Nyumba 1,722 zimepata uharibifu mdogo

  • Majumba 8 ya Ufalme yameharibiwa kabisa

  • Majumba 17 ya Ufalme yamepata uharibifu mkubwa

  • Majumba 76 ya Ufalme yamepata uharibifu mdogo

Jitihada za Kutoa Msaada

  • Halmashauri 26 za Kutoa Msaada zinashughulikia hali nchini Ukrainia

  • Nyumba 46 zimerekebishwa

  • Majumba 5 ya Ufalme yamerekebishwa

  • Watu 54,445 wamesaidiwa moja kwa moja na halmashauri hizo kupata makao salama zaidi

  • Wahubiri 27,655 wamekimbilia nchi nyingine na wanasaidiwa na waamini wenzetu